DOREEN BLOG

HABARI, MICHEZO NA BURUDANI

Adbox

Tuesday, 9 December 2025

JESHI LA POLISI LAKANUSHA TAARIFA ZA UPOTOSHAJI MTANDAONI, LATHIBITISHA USALAMA NCHINI KUWA SHWARI

12/09/2025 02:29:00 pm


Na Mwandishi wetu, Dodoma

Jeshi la Polisi nchini limekanusha taarifa zinazoenezwa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu kuwepo kwa maandamano leo Desemba 9, 2025, na kusisitiza kuwa hadi majira ya mchana hali ya usalama nchini kote ni shwari.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi, Makao Makuu ya Polisi Dodoma,David Misime vyombo vya ulinzi na usalama vinaendelea kuimarisha ulinzi na kulinda maisha ya wananchi pamoja na mali zao kama ilivyo jukumu lao la msingi.

Polisi imeeleza kuwa picha na video zinazosambazwa mitandaoni zikidaiwa kuonyesha maandamano yanayoendelea leo si sahihi, bali ni matukio ya zamani na kwamba baadhi ya picha hizo zinatoka katika matukio ya Oktoba 29, 30 na 31 mwaka 2025, huku zingine zikitoka miaka ya nyuma ikiwemo tukio la Juni mwaka huu ambalo lilihusisha sherehe za jando za jamii ya Wamaasai zilizofanyika katika msitu wa TANAPA jijini Arusha.

Jeshi hilo limekumbusha kuwa maandamano yaliyokuwa yanatajwa kama “maandamano ya amani” yalipigwa marufuku tangu Desemba 5, 2025, baada ya kubainika hayakukidhi matakwa ya kisheria ikiwemo Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Sheria ya Polisi na Polisi Wasaidizi, Sura ya 322.

Aidha, Polisi imetoa wito kwa wananchi kuendelea kufuata sheria za nchi na kupuuza taarifa za upotoshaji, kwa manufaa ya amani na usalama wa Taifa.

WAFUNGWA 1,036 WAPATA MSAMAHA WA RAIS SAMIA

12/09/2025 11:44:00 am

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan leo Disemba 09, 2025, Tanzania ikiadhimisha miaka 64 ya uhuru wa Tanzania bara, ametangaza kuwasamehe wafungwa 1,036, wafungwa 22 kati yao wakiachiliwa huru na wengine 1,014 wakipunguziwa adhabu zao.

Kulingana na taarifa iliyosainiwa na Waziri wa mambo ya ndani ya nchi Mhe. George Simbachawene, Ikulu imeeleza kuwa ni matarajio ya serikali kuwa wafungwa walioachiwa huru watarejea tena katika jamii kushirikiana na wananchi katika ujenzi wa Taifa na kujiepusha kutenda makosa ili wasirejee tena gerezani.

Miongoni mwa waliosamehewa  ni wafungwa wagonjwa wenye magonjwa ya kudumu au sugu ambao wapo katika hatua za mwisho pamoja na wafungwa wazee wenye umri wa miaka 70 au zaidi- Vyote vikitakiwa kuthibitishwa na jopo la waganga wa Wilaya na Mikoa.

Aidha wengine walionufaika na msamaha huo ni wafungwa wa kike walioingia na ujauzito gerezani au wenye watoto wanaonyonya au wasionyonya waliohukumiwa kifungo cha mwaka mmoja na kuendelea pamoja na wafungwa wenye ulemavu wa mwili na akili wasio na uwezo wa kufanya kazi.

Aidha wamesamehewa pia wafungwa waliohukumiwa adhabu ya kuwekwa kizuizini (under president's pleasure) ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka kumi au zaidi

Prf. Kitila :Serikali imepanga kufanya mageuzi makubwa katika uongozi wa mashirika ya umma

12/09/2025 11:43:00 am

Serikali imepanga kufanya mageuzi makubwa katika uongozi wa mashirika ya umma, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa watendaji wakuu na wajumbe wa bodi za wakurugenzi wanapatikana kwa njia ya ushindani ili kuongeza uwazi, uadilifu na ushiriki mpana wa Watanzania wenye sifa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, amesema mfumo huo mpya utaanza kutumika kuanzia Julai 1, 2026 mara baada ya kupitishwa kwa sheria mpya inayoandaliwa na serikali.

Amesema uamuzi huo ni sehemu ya mpango mpana wa kuboresha utendaji wa mashirika ya umma, kuweka uwazi katika uteuzi wa viongozi, na kuondoa utaratibu wa uteuzi wa moja kwa moja uliokuwa ukilalamikiwa na wadau kwa kukosa ushindani wa wazi. 

“Kama ni Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO utaomba, uta-apply, na utashindanishwa. Kama unataka kuwa mjumbe wa bodi ya TPA au TISEZA utapitia mchakato wa ushindani. Watanzania wote wenye sifa wataomba, na uchaguzi utafanywa kwa ‘competitive recruitment,” amesema.
Katika maelezo yake kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Prof. Mkumbo amesema mageuzi hayo yanakwenda sambamba na hatua kadhaa zinazolenga kuongeza tija ya mashirika ya umma na kuimarisha mchango wake katika uchumi wa taifa na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Prof. Mkumbo amesema serikali inaunda mfumo mpya na imara wa kupima maendeleo ya mashirika ya umma kwa kuzingatia tija ya kiuchumi na ubora wa huduma. Mashirika hayo yatapewa vigezo vipya vya kupimwa na kila moja litahesabiwa kwa kiwango kinachochangia kwenye uchumi na ustawi wa wananchi.

Amesema sheria mpya itayataka baadhi ya mashirika ya umma ya kibiashara kujisajili katika Soko la Hisa  ili Watanzania waweze kununua hisa na kumiliki mashirika yao, kupanua uwazi katika uendeshaji, na kuongeza uwajibikaji kwa menejimenti na bodi.

Serikali yaweka kipaumbele katika kuhuisha majengo na kupanga upya miji mikubwa

12/09/2025 11:43:00 am

Serikali imeweka kipaumbele katika kuhuisha majengo na kupanga upya miji mikubwa, hatua inayolenga kuongeza thamani ya makazi, kuboresha matumizi ya ardhi na kuvutia uwekezaji katika kipindi cha pili cha miaka mitano ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo amesema mpango huo utahusisha ubia kati ya wananchi na sekta binafsi ili kubomoa nyumba chakavu, kujenga majengo mapya ya ghorofa na kuwapa wakazi sehemu za makazi na biashara ndani ya miradi hiyo.

Akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam siku ya Jumatatu, Prof. Mkumbo amesema Serikali tayari imeainisha maeneo matatu ya kuanzia Vingunguti, Buguruni na Manzese kwa mkoa wa Dar es Salaam ambapo michakato ya kuwavutia wawekezaji itatangazwa rasmi, huku wakazi waliopo wakihakikishiwa kunufaika moja kwa moja kupitia mfumo wa kupata ‘floor’ zao za makazi na biashara katika majengo mapya.

Waziri huyo amesema mageuzi ya miji ni sehemu ya mkakati mpana wa kufungua fursa za uchumi, kuongeza ajira na kuboresha ubora wa maisha katika maeneo ya mijini. Ameeleza kuwa matumaini ya Serikali ni kuona miji ya Dar es Salaam na baadaye mingine nchini ikiwa na makazi yaliyopangwa vizuri na miundombinu ya kisasa.

Amesema sambamba na kuhuisha miji, Serikali inaelekeza nguvu katika kufungua maeneo mapya ya utalii tofauti na yale yanayofahamika sana kama Ukanda wa Kaskazini, huku akitaja Hifadhi ya Taifa ya Ruaha kama moja ya maeneo makubwa yenye uzuri wa kipekee lakini ambayo hayajafunguliwa kikamilifu. Pia ameeleza kuwa utalii wa fukwe haujatumiwa ipasavyo licha ya Tanzania kuwa na mwambao mrefu uliojaa vivutio.

Prof. Mkumbo amesema Serikali itaendelea kushirikiana na sekta binafsi ya ndani na nje ya nchi ili kuongeza uwekezaji katika utalii, ujenzi na miundombinu, hatua anayosema itachochea ukuaji wa mapato ya taifa na kupanua ajira kwa vijana.

WAZIRI MKUU AWAKINGIA KIFUA WAFANYABIASHARA WADOGO ATOA ONYO KALI KWA HALMASHAURI ZOTE NCHINI

12/09/2025 11:43:00 am

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu  Nchemba ameagiza Halmashauri zote Nchini  Majiji  kutochukuwa bidhaa halali za Wananchi  ambao ni wafanyabiashara wadogo wanaojitafutia riziki zao Barabarani kulingana na mitaji yao hata kama wakikutwa na makosa  ushughulikiwe utaratibu tu!  na sio kuua mitaji yao midogo 

"Huu utaratibu wa kuchukua bidhaa haukubaliki wafautilieni waliochukuwa bidhaa na kama hazipo hao ni wezi kama wezi wengine tusicheze na mitaji ya watu hatutapiga vita umasikini kama hatutaheshimu mitaji ya watu "  Waziri Mkuu 

Aidha ametumia jukwaa hilo kuwaambia kutangaza Ziara ya majiji yote Nchini kuangazia changamoto za wafanyabiashara hao na kuendelea kuacha utaratibu huo hapo hapo amesisitiza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan ni mtu wa haki hivyo watendaji wasimuangushe

Monday, 8 December 2025

Waziri amewaomba Watanzania kutojihusisha na maandamano yasiyokuwa rasmi kisheria Disemba 9 ,2025.

12/08/2025 02:38:00 pm

Waziri wa Mambo ya ndani Mhe. George Boniface Simbachawene amesisitiza kuwa maandamano yanayohamasishwa kufanyika kesho Jumanne Disemba 09, 2025 ni haramu na yatadhibitiwa na Vyombo vya ulinzi na usalama ikiwa yatafanyika, akitaka wote wanaotaka kuandamana kufuata sheria na miongozo iliyopo.

Kulingana na Waziri Simbachawene mbele ya  waandishi wa habari leo Jumatatu Disemba 08, 2025, amewaomba pia Watanzania kutojihusisha na maandamano hayo yasiyokuwa rasmi kisheria   kutokana pia na kushamiri kwa matukio na viashiria vya uvunjifu wa amani na uhalifu.

"Maandamano hayo yanayoitwa ya amani hayaonekani yanaombwa na nani, kwa utaratibu gani na yatafanyika wapi. Haya yanayoelezwa ni kwamba wanaeleza tu kuwa yatakuwa hayana ukomo na yatakuwa makubwa kuliko yale ya tarehe 29."

"Ndugu zangu kama yakiwa hayo ni maandamano yasiyo na ukomo, maandamano ambayo ni makubwa kuliko yale ambayo watu walichoma mali za watu, watu, walichoma vituo vya mafuta, majengo ya serikali, Vituo vya polisi na hata watu wakafa, sasa haya tunayoambiwa ni makubwa kuliko yale si maandamano kwasababu kwanza hayana kibali kwa mujibu wa sheria lakini pia hayaeleweki yanafanywa na nani." Amesema Mhe. Waziri

Kulingana na Waziri Simbachawene, maandamano rasmi kulingana na sheria, maandamano ni lazima yawe na ukomo, lazima yaombwe na mtu mahususi, yawe na ujumbe, yaseme shabaha pamoja na kueleza muelekeo wake ili Jeshi la Polisi liweze kutoa huduma yake ya ulinzi kwa waandamanaji wa tukio husika.

Mhe. Simbachawene amethibitisha kuwa maandamano ya Disemba 09 ni haramu na yasiyokubalika, akitoa rai kwa wote walioichoka amani ya Tanzania kuheshimu sheria za nchi na ikiwa vinginevyo, Vyombo vya ulinzi na usalama vitawathibiti kulingana na sheria.

Sunday, 7 December 2025

KAULI YA MSIGWA "VYOMBO VYA ULINZI NA USALAMA VIPO TIMAMU MUDA WOTE KULINDA RAIA"

12/07/2025 02:53:00 pm

Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania Bw. Gerson Msigwa amesisitiza kuwa Vyombo vya Ulinzi na usalama, wakati wote vipo tayari muda wote kuhakikisha kuwa Mipaka ya nchi, Watanzania na mali zao wanabakia salama muda wote.

"Sisi kama Nchi, Vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kama vilivyokuwa jana, kama vilivyo leo ndivyo vitakavyokuwa tarehe tisa Disemba na tarehe zitakazofuata. Wakati wote Vyombo vyetu vipo tayari kuhakikisha watu na mali zao wapo salama na mipaka yetu inabakia salama. Vipo tayari si tarehe tisa tu ni wakati wote kuhakikisha nchi inakuwa salama." Amesema Msigwa.

Akizungumza na chombo kimoja cha Habari Mkoani Dar Es Salaam, Msemaji huyo wa serikali ametoa wito pia kwa Watanzania kushiriki katika kuilinda nchi yao kwa wivu mkubwa, akiwataka kutohakikisha hakuna anayeweza kuwapangia la kufanya na badala yake wafanye mambo kwa namna ya mahitaji yao wenyewe.

Msigwa kadhalika amesisitiza kuwa serikali ya awamu ya sita ipo tayari muda wote kuwasikiliza Watanzania na kuyafanya yale yote watakayoona yanafaa kulingana na rasilimali zilizopo nchini.

355 MIKONONI MWA POLISI MKOANI MWANZA KWA WIZI NA UPORAJI WA OKTOBA 29.

12/07/2025 12:01:00 pm

Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza limefanya msako na kufanikiwa kuwakamata jumla ya wahalifu wapatao 355 ambao wamekamatwa na kufikishwa Mahakamani kwa makosa mbalimbali ikiwemo wizi na uporaji walioufanya wakati na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.

Kulingana na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishna wa Polisi Wilbroad Mutafungwa, Polisi kwa kushirikiana na Vyombo vingine vya ulinzi na usalama vimewakamata Jumla ya watu wengine 116  kwa tuhuma za uchochezi na kuhamasisha maandamano haramu wanayopanga kuyafanya Jumanne ya Disemba 09, 2025.

Kulingana na Kamanda Mutafungwa watuhumiwa 355 waliokamatwa walikutwa na Mitungi 118 ya gesi ya Kampuni ya Lake Oil Oryx na Mihan, Magodoro 40 aina ya Super Banco na Tanform pamoja na jora 18 za Vitambaa vya kushonea magodoro.

"Watuhumiwa wengine wamekamatwa na  difu 1 ya gari, Injini 3 za magari, Gear boksi, Mashine 2 za ATM, Matenki 4 ya maji, Fire Extinguisher 3, Compresser 01, Pipa 4 za Kemikali za kutengenezea magodoro, Friji 1 aina ya Voni, Kasiki 2, ndoo za rangi pamoja na mabati 14." Amesema Kamanda Mutafungwa.

Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza kando ya kueleza kuendelea na doria katika Mkoa mzima wa Mwanza, katika taarifa yake kwa umma limetoa rai kwa wananchi kutokubali kushirikishwa kwenye maandamano haramu yaliyopigwa marufuku hapo Disemba 09, 2025, Wazazi na walezi wakitakiwa kuwazuia watoto wao kutojiingiza kwenye maandamano na badala yake washirikiane na serikali kuimarisha amani na utulivu kwenye siku hiyo muhimu ya kumbukizi ya Tanzania kupata uhuru wake.

RC MTAKA ALIA NA VIJANA WA GEN_Z NCHINI, AWATAKA KULINDA AMANI YA NCHI YAO.

12/07/2025 11:06:00 am

Na Mwandishi wetu,Njombe

Mkuu wa Mkoa wa Njombe Antony Mtaka amekisihi  kikundi cha vijana wanaojiita Gen_Z kutambua kuwa wao ni kizazi  kinachobeba matumaini na sura ya taifa,hivyo wanapaswa kulinda Amani badala ya kujiingiza kwenye makundi ya kutaka kuangamiza Taifa.

Mkuu huyo wa Mkoa ametoa kauli hiyo kwenye Ibada katika Kanisa la wa Adventist Wasabato lililopo Mkoa wa Njombe ambapo ametumia Fursa hiyo kuisihi jamii hususani Vijana kutambua kuwa Amani ni Tunda la Haki ambapo ni wajibu wa kuilinda Amani ya nchi yetu kwa Wivu Mkubwa,

 “Mkoa wetu bado upo salama,hauna matishio ya kihalifu,tunaendelea kujenga mazingira thabiti ya ulinzi wa watu na mali,ili kutoa fursa kwa wananchi wetu kuendelea kufanya shughuli zao za uzalishaji mali na mahangaiko yao ya kujipatia kipato cha siku, 

"Na kuongeza " Usalama wa mkoa wetu, utatuongezea imani kwa wawekezaji wetu mbalimbali kuendelea kuamini kwamba Njombe ni mahala sahihi pa wao kuweka mitaji yao,wana Njombe tushikamane kuhakikisha tunaziepuka aina yoyote ya chokochoko zitakazoashiria uhalibifu wa mali, uwekezaji,miradi ya umma na binafsi,au uharibifu wa uhai wa wananchi wenzetu." Amesema  Rc  Mtaka.

Hata hivyo amewataka Wananchi kutoa taarifa kwenye vyombo husika pale watakapoona na  kuhisi dalili yoyote inayoashiria uvunjifu wa amani , kuhatarisha usalama wa eneo lao ,kwani ulinzi shirikishi huanza na wanajamii mmoja mmoja kwa kutoa taarifa kwa wakati.

Ikumbukwe kuwa kupitia mitandao ya kijamii kumekuwepo na baadhi ya wanaharakati walioanzisha kikundi kinacho jiita wana Gen _Z cha kuhamasisha maandamano na uvunjifu wa Amani Nchini jambo ambalo halikubaliki kwa Taifa na jamii kwa ujumla.

Mwisho.

Saturday, 6 December 2025

MKASA WA SALAH WA SUDAN NA HARAKATI MFU ZA MANGE KIMAMBI

12/06/2025 04:30:00 pm

Mwaka 2019 Alaah Salah alikuwa na umri wa miaka 22 huku akiwa mwanafunzi wa mwaka wa pili kwenye Chuo Kikuu cha Sudan. Aliongoza na kuhamasisha maandamano yaliyomtoa Omar Bashir madarakani. Mpaka sasa Omar Bashir yuko kifungoni akitumikia adhabu ya makosa ya jinai aliyotenda madarakani.

Wakati huo wengi waliingizwa barabarani bila ya kujua kuwa walikuwa wakifanikisha mradi wa aliyeitwa mwanamke shujaa na mzalendo, Salah akapata umaarufu mkubwa, akitukuzwa na Mataifa na Vyombo vya habari vya Kimagharibi, akitwikwa majina kadhaa na kumpa sifa za ujasiri na ushujaa kama mpigania haki, demokrasia na Mwanamapinduzi wa kweli.

Baada ya Mapinduzi ya mwaka 2019 upepo ukabadilika, lengo la mabeberu likatimia, Omar akapinduliwa watu wakidhani kuwa matumaini yao yanaenda kutimia, bahati mbaya ndio ukawa mwanzo wa kuiharibu nchi yao wenyewe, Jinamizi la mauaji likatanda, unyanyasaji ukatapaaa Sudan na Mwanamke Salah akapotea na haonekani tena akikemea ama kupaza sauti kuhusu unyanyasaji na ukatili unaoendelea nchini mwake.

Taifa hilo limekumbwa na moja ya migogoro ya kibinadamu mibaya zaidi duniani, zaidi ya watu milioni 15 wamelazimika kukimbia makazi yao na zaidi ya watu milioni 30 wanahitaji msaada wa kibinadamu, wakiwemo milioni 24.6 wanaokabiliwa na njaa kali, kwa mujibu wa mashirika ya Umoja wa Mataifa. Makadirio yanaonesha kuwa watu wapatao 150,000 wameuawa ndani ya mwaka wa kwanza wa mapigano pekee.

Alaah ni mfano halisi wa kile Mange Kimambi anachokifanya kwa sasa nchini Tanzania, haishi Tanzania na mara zote amedai kuwa hana la kupoteza nchini. Si ndugu wala mali zake na ndicho kinachomfanya kuwa kinara wa kuhamasisha vurugu nchini- aiweke nchi kwenye janga, apokee malipo yake na atuache Watanzania tukitaabika katikati ya machungu ya kuiharibu nchi yetu wenyewe.

Watanzania tuamke, tujifunze kwenye tone dogo la maumivu tulilolipata Oktoba 29, 2025. Tujiepushe na akina Alaah wa Tanzania wanaobebwa na kusifiwa na Vyombo vya habari vya magharibi ili kutupofusha akili na kuamini kuwa wanatutakia mema ilihali wanasimamia maslahi yao binafsi.

TAASISI ZA KIMATAIFA ZATAKIWA KUIACHA MIFUMO YA KITAIFA KUFANYA KAZI YAKE

12/06/2025 11:09:00 am

Serikali ya Tanzania katika taarifa yake kwa Vyombo vya habari leo Ijumaa Disemba 05, 2025 imetangaza kuzipokea na kuzifanyia kazi taarifa na matamko mbalimbali yaliyotolewa na nchi rafiki, mashirika ya kimataifa na Taasisi za maendeleo kuhusu Tanzania na matukio ya uvunjifu wa amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Jumatano Oktoba 29, 2025.

Kulingana na Taarifa ya Wizara ya mambo ya nje, miongoni mwa waliotoa matamko hayo ni pamoja na Ubelgiji, Canada, Denmark, Ujumbe wa Umoja wa Ulaya (EU), Finland, Ufaransa, Ghana, Ujerumani, Ireland, Italia, Uholanzi, Norway, Poland, Slovakia, Hispania, Sweden, Uswisi, Uingereza, Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa, Marekani pamoja na Taasisi ya Thabo Mbeki ya Afrika kusini.

Katika taarifa hiyo, Tanzania imeonesha kushangazwa na baadhi ya maudhui ya matamko hayo, hasa ikizingatiwa kuwa kulifanyika mazungumzo ya wazi kati ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mabalozi wanaowakilisha nchi hizo nchini, tarehe 28 Novemba 2025.

Serikali imesisitiza kuwa, pamoja na kutambua nafasi ya jumuiya ya kimataifa katika kuimarisha demokrasia na maendeleo ya kijamii na kisiasa, ni muhimu pia kuheshimu uamuzi wa kuundwa kwa Tume ya Uchunguzi itakayochunguza kwa kina matukio ya vurugu zilizotokea baada ya uchaguzi, na kuandaa ripoti kamili.

Ripoti hiyo, kwa mujibu wa Serikali ndiyo itakayoleta uelewa mpana kuhusu kilichotokea na kuwa msingi wa mashauriano na ushirikiano wa baadaye katika kujenga taifa lenye amani na umoja.

"Serikali ya Tanzania inaendelea kuwa mstari wa mbele katika ushirikiano wa kimataifa kwaajili ya amani na maendeleo na inatoa wito kwa wadau wote kuruhusu mifumo ya kitaifa kufanya kazi yake kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa," imeeleza taarifa hiyo.

Aidha, Serikali ya Tanzania imewahakikishia wadau wa maendeleo na jumuiya ya kimataifa kuwa itaendelea kujadiliana na kushirikiana nao katika masuala yote ya maslahi ya pande zote, kwa misingi ya usawa na kuheshimiana.

Friday, 5 December 2025

Dkt .Asha-Rose Migiro, awasisitiza wanawake nchinii jukumu la uongozi katika kulinda na kuimarisha amani.

12/05/2025 02:27:00 pm
Na Doreen Aloyce,Dodoma

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Asha-Rose Migiro, ametaka kuanzishwa kwa mazungumzo ya kitaifa ya maridhiano huku akiwasisitiza wanawake nchini kuchukua jukumu la uongozi katika kulinda na kuimarisha amani. Wito huo umetolewa wakati wa ufunguzi wa Jukwaa la Wanawake 2025 lililofanyika jijini Dodoma chini ya kaulimbiu “Mama ni Amani”.

Katika hafla hiyo, washiriki walioneshwa makala ya video iliyodokeza matukio ya vurugu za Oktoba 29, 2025, ikionesha kiwango cha uharibifu wa mali na taarifa za vifo, ingawa idadi kamili ya waliofariki haikutajwa. Dk. Migiro alisema matukio hayo hayalingani na utamaduni wa Tanzania wa mshikamano na utulivu, hivyo kuhitaji hatua za makusudi kurejesha hadhi ya taifa.

Amefafanua kuwa zaidi ya asilimia 50 ya Watanzania ni vijana na ndiyo maana wanawake wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika malezi, uongozi wa majadiliano ya maridhiano na kuzuia kurudiwa kwa matukio ya vurugu.

Washiriki wa jukwaa hilo walitoa maoni mbalimbali kuhusu nafasi ya mwanamke katika kudumisha amani.
Kate Kamba alisisitiza kuwa wanawake ni walimu wa kwanza wa familia na wanabeba jukumu muhimu la kujenga misingi inayoweza kuzuia machafuko ya baadaye. Alionya kuwa bila kuwekeza katika malezi bora, taifa linaweza kupoteza mwelekeo wake.

Sifa Swai, kwa upande wake, alisema changamoto za usalama wa amani zimehamia zaidi kwenye mitandao ya kijamii ambako taarifa potofu husambaa kwa kasi, hivyo kuwaathiri hasa vijana. Aliongeza kuwa misukosuko katika biashara zinazomilikiwa na wanawake huathiri moja kwa moja ustawi wa familia na inaweza kuchochea migogoro ya kijamii.

Kwa pamoja, washiriki walikazia umuhimu wa sauti ya mwanamke katika kuponya makovu ya kijamii, kudumisha umoja na kuongoza juhudi za maridhiano nchini.

WATANZANIA WAFURAHISHWA NA META KUZIFUNGIA AKAUNTI ZA MANGE NA MARIA

12/05/2025 11:12:00 am

Wanaharakati Mange Kimambi na Maria Sarungu Tsehai wenye msururu kadhaa wa lawama, malalamiko na kutajwa kuwa sababu ya uvunjifu wa maadili, amani na umoja wa Watanzania wamefungiwa akaunti zao za Meta, kampuni mama ya Teknolojia yenye kumiliki mitandao ya (Instagram, Facebook na WhatsApp).

Mange na Maria wanashutumiwa pia kwa kuchochea matukio ya uvunjifu wa amani, mabaya zaidi kuwahi kutokea kwa siku za hivi karibuni nchini Tanzania, Yakifanyika wakati na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 na kusababisha uharibifu mkubwa wa mali za umma na za binafsi, Wizi, uchomaji moto na vifo vya watu kadhaa kulikotokana na udhibiti wa tukio hilo na umiliki wa silaha kutoka kwa Vituo vya Polisi vilivyovamiwa na Makundi hayo ya kihalifu.

Meta imethibitisha taarifa hizo kwa kuandika " Akaunti hizo zimeondolewa kwa kukiuka sera yetu. Haturuhusu watu kuunda akaunti mpya zinazofanana na zile tulizoziondoa awali kwa kukiuka viwango vya juu vya Taasisi ya Meta."

Mange na Maria wanatajwa kupokea mabilioni ya fedha kutoka kwa Taasisi na watu binafsi ili kuchochea vurugu, chuki na machafuko ndani ya Tanzania, wakitumia mitandao yao ya Kijamii kuratibu na kuhamasisha machafuko na mauaji ya raia nchini Tanzania kwa kipindi kirefu hivi sasa suala ambalo limesababisha wananchi wa Tanzania kufurahishwa na uamuzi wa @meta kuzifungia akaunti zao kwa mustakabali wa amani na ulinzi wa haki za binadamu. 

Watu hawa wamepigiwa mfano kama watu halisi wanaotumia Mitandao ya Kijamii kwa namna hasi yenye kuleta hasara, ghasia na vurugu kwenye jamii kwa maslahi yao binafsi bila kujali haki za wengine.

Hii si mara ya kwanza kwa Kampuni ya Meta kuzifungia akaunti zinazokiuka miongozo ya kampuni hiyo ya teknolojia kwani Januari 2021, Meta waliifunga akaunti ya X ya Rais wa Marekani Donald Trump kwa kile walichokieleza kama hatari ya kuchochea vurugu baada ya kutoa wito kwa wafuasi wake kuvamia bunge wakijaribu kuvuruga kikao cha kuidhinisha ushindi wa Rais Mstaafu Joe Biden. Vurugu hizo zilifanyika na zilisababisha uharibifu na vifo kadhaa vya wananchi.

Aidha mwaka 2022 Mtandao wa X pia ulizifungia akaunti za gazeti maarufu nchini humo la Caravan na akaunti ya muigizaji Sushant Singh na ya Mwanaharakati Hansraj Meena kwa madai ya kukiuka masharti ya mtandao huo kutokana na kujihusisha na maandamano ya kutaka mabadiliko katika kilimo nchini humo.

Thursday, 4 December 2025

Simbachawene awataka Vijana na Wanaharakati kutafuta njia sahihi ya kudai haki ikiwemo mazungumzo mezani

12/04/2025 06:14:00 pm
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,George Simbachawene amewataka Vijana na Wanaharakati kutafuta njia sahihi ya kudai haki ikiwemo mazungumzo mezani akiwaasa kuwa vita na vurugu avijawahi kusaidia bali upelekea kupotea kwa amani huku akitolea mfano wa nchi ya Kidemokrasia ya Kongo ambayo takribani ni zaidi ya miaka thelathini wanaitafuta amani ambayo imepotea.

Ametoa kauli hiyo wakati wa Mkutano wa Pili unaohusisha Pande Tatu ikiwemo Serikali ya Tanzania, Jamhuri ya Demokrasia ya Congo na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi Duniani UNHCR ambapo pia walitumia mkutano huo kusaini nyaraka zinazoelezea Mpango wa Urejeshwaji wa Wakimbizi Elfu Themanini na Sita na Mia Mbili Hamsini na Sita waliopo hapa nchini ambapo pia Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Ndani wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo,Shabani Bihango na Mwakilishi wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi Duniani nchini Tanzania,Barbara Dotse waliishukuru Tanzania kwa kuhifadhi wakimbizi hao kwa muda unaozidi miaka thelathini.

Tuesday, 2 December 2025

matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea wakati na baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025 yalikuwa ni matukio ya kupangwa yakiwa na lengo la kuiangusha dola ya Tanzania.

12/02/2025 06:34:00 pm
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema serikali na Vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga wakati wote kukabiliana na wanaoratibu, kupanga na kufadhili matukio ya uvunjifu wa amani yaliyopangwa kufanyika aidha Disemba 09 ama Disemba 25, 2025.

Rais Samia amebainisha hayo leo Jumanne Disemba 02, 2025 wakati akizungumza na wazee wa Mkoa wa Dar Es Salaam, akikaririwa awali akisema kwamba matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea wakati na baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025 yalikuwa ni matukio ya kupangwa yakiwa na lengo la kuiangusha dola ya Tanzania.

"Ndugu zangu nilisema yaliyopita si ndwele tugange yajayo, lililopita limepita, kwa maneno tunasikia lipo jingine linapangwa lakini inshaallag Mola hatosimama nao, litapeperuka.

Lakini nataka niseme, nilimsikia mmoja kati ya waandaaji wa nje anasema ebu tarehe tisa lihairisheni subirini Krismasi kwasababu sasa hivi wamejipanga, nataka niwaambie wakati wowote wakija tumejipanga." Amesema Rais Samia.

Katika hatua nyingine Rais Samia amesema kama binadamu kukosana kupo, akikiri kuwa si kila wakati serikali inakuwa haina mapungufu, akisisitiza umuhimu wa kukaa, kuzungumza na kuondoa mapungufu 

Monday, 1 December 2025

WATANZANIA WANATAKA UWAZI NA UCHUNGUZI KAMILI- JAJI OTHMAN CHANDE

12/01/2025 05:58:00 pm

Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani wakati na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 Jaji Mkuu mstaafu Mohammed Chande Othman amesema Watanzania wanataka uchunguzi kamilifu wa Matukio ya Oktoba 29 pamoja na kutaka uwazi kwenye kutekeleza wajibu wao.

Jaji mstaafu Othman amebainisha hayo leo Jumatatu Disemba Mosi, 2025 wakati akizungumza na waandishi wa habari, akisisitiza kuwa baadhi ya Mikutano yao wataifanya hadharani na mingine faragha ili kulinda haki za watu wengine.

"Mikutano yetu mingine itafanyika kwenye hadhara na mingine itabidi tuende kwenye faragha kwenye mazingira maalumu ili kulinda haki za mtu na Tanzania sasahivi tuna sheria ya kulinda faragha za watu." Amesema Jaji Othman.

Mwenyekiti huyo wa tume ameeleza kuwa matakwa hayo ya watanzania wameyapokea na ndiyo watakayoyatumia katika kujibu hadidu za rejea katika utekelezaji wa majukumu yao ya uchunguzi wa matukio hayo ya Oktoba 29, 2025.

TUSIKUBALI KUCHONGANISHWA NA WACHACHE WENYE MASLAHI BINAFSI- MWIGULU

12/01/2025 05:12:00 pm

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba akiwa kwenye Ziara yake ya Kikazi Mkoani Arusha, amesisitiza umuhimu wa kulinda amani kwa maendeleo na ustawi wa Watanzania, akiwataka wananchi kuamka na kuwakataa wale wote wanaowachonganisha kwa maslahi yao binafsi.

Akieleza kuwafahamu baadhi ya Watanzania wanaolipwa fedha ili kuwagombanisha na kuwataka kuingia barabarani kufanya vurugu, Mhe. Nchemba ameeleza kuwa wanaohamasisha vurugu nchini wamekuwa na visingizio kadhaa vya kuwahadaa wananchi huku lengo lao likiwa ni kuwagombanisha watanzania ili kutaka kuzifaidi rasilimali za nchi.

"Zimetokea vurugu, kwa aina  ya vurugu zilivyotokea, kwanini hatushtuki? Wanatumia visingizio vingine lakini hapa kuna mchezo. Zimetolewa fedha wakapewa vijana na wale Vijana wakaandaa Vijana wenzao na kuwataka kufanya vurugu. Leo tujiulize wale wanaotoa hizo fedha watazirudishaje? Na kama ni maandamano, Kiongozi wake alikuwa nani? Waliandamana kutoka wapi kwenda wapi? Ajenda yao ilikuwa ipi? Tunachonganishwa mno, kuna jambo watu wanatafuta. Amkeni Watanzania." Amesema Waziri Mkuu.

Mhe. Mwigulu akizungumza katika Mkutano wake wa hadhara kwenye Viwanja vya Magufuli, Leganga, Usa River, Wilayani Arumeru, amesisitiza kuwa ikiwa Tanzania itapoteza amani na utulivu wake, jamii na serikali itashindwa kukabiliana na umaskini, gharama kubwa za maisha na kukabiliana na tatizo la ajira kwa Vijana, akiwataka Watanzania kutorubuniwa na kuingia kwenye Vitendo vya Uvunjifu wa amani.

Sunday, 30 November 2025

MZEE WA UPAKO AWATAKA WATANZANIA KUJIFUNZA KUTOKANA NA TUKIO LA OKTOBA 29, "HALIPASWI KURUDIWA TENA"

11/30/2025 09:28:00 pm

Mchungaji wa Kanisa la Maombezi (GRC), Anthony Lusekelo ‘Mzee wa Upako’, ametoa wito kwa Watanzania kujifunza kutokana na tukio la Oktoba 29, akisema limeleta maumivu makubwa kwa taifa na halipaswi kurudiwa tena. Amesema tukio hilo limekuwa uzoefu mpya ambao Watanzania hawakuwahi kuupitia, akiwapa pole wakazi wa Dar es Salaam, Arusha, Songwe na Mwanza ambao amesema wameguswa sana na kilichotokea.

Amesema hali hiyo imemkumbusha mazingira ya mwaka 1977/1978 wakati wa vita dhidi ya Idd Amin, akieleza kuwa tukio la Oktoba 29 lilikuwa kama “vita ya wenyewe kwa wenyewe.” Pamoja na kueleza kuwa wapo waumini wake waliopigwa risasi maeneo ya Kimara, amesema hakuna Mtanzania ambaye hajaguswa, hivyo si wakati wa kulaumiana bali kila mtu ajihoji kwa nini nchi imefika hatua hiyo huku akionya kuwa kutokujifunza kutokana na kilichotokea kunaweza kusababisha tukio jingine kubwa zaidi baada ya miaka michache ijayo.

Mzee wa Upako amesema ni lazima Watanzania, wakiwemo viongozi wa dini, wazazi, viongozi wa serikali na kisiasa, kutafakari namna ambavyo heshima ya nchi imeharibika na kwamba  ni muhimu kurejea kwenye misingi hiyo ili matukio kama ya Oktoba 29 yasijirudie tena.

MISA YAWANOA WAANDISHI WA HABARI, NAIBU WAZIRI LONDO ASEMA SERIKALI ITAENDELEA KULINDA UHURU WAO

11/30/2025 11:32:00 am

Na Doreen Aloyce, Dodoma

NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Dennis Lazaro Londo, amewahakikishia waandishi wa habari nchini kuwa Serikali itaendelea kulinda uhuru wao wa kujieleza pamoja na kuhakikisha wanatimiza majukumu yao kwa usalama na weledi.

Mhe. Londo amezungumza hayo ljijini Dodoma katika mafunzo ya waandishi wa habari  yaliyoandaliwa na Misa Tanzania yaliyowaleta pamoja Wanahabari 100 kutoka maeneo mbalimbali nchini, ambapo Londo amesema Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi itaendelea kushirikiana na wadau wa habari katika maeneo yote yanayohusu usalama kwa waandishi wa habari.

Aidha, amebainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka msukumo mkubwa katika kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi, sambamba na kulinda uhuru wa vyombo vya habari. 

" Falsafa ya Mhe. Rais kupitia “4R” zinaipa tasnia ya habari nafasi muhimu katika kulinda amani, kuimarisha umoja wa kitaifa na kuendeleza mijadala yenye tija kwa jamii." Amesema Londo.

Edwin Soko ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika – Tawi la Tanzania (MISA Tanzania),   ametahadharisha kuwa uandishi unaolenga kugawa jamii unadhoofisha misingi ya amani ambayo nchi imeijenga kwa miaka mingi,huku akisisitiza kuwa vyombo vya habari vinapaswa kujikita kuandika habari ambazo zitaleta umoja na mshikamo sio kuchochea mgawanyiko na uhasama kwa taifa.


“Hii ndiyo Tanzania, sisi ndiyo Watanzania,tukiruhusu nchi yetu ikawaka moto hatuna pa kwenda.Wapo wanaolaumu na kuona kama vyombo vya habari havijatimiza wajibu wake Oktoba 29,2025 wakati wa uchaguzi, na kusahau kuwa vyombo vya habari havilengi kwenye kuiboa jamii bali kuijenga ,”amesema Soko.

Pia Soko ametumia fursa hiyo,kusisitiza umuhimu wa waandishi na vyombo vya habari kuwa uhuru na kufanya kazi zao kwa kufuata maadili ya uandishi bila msukumo au shinikizo kutoka kwa watu binafsi.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha SAUT Mwanza, Dkt. Dotto Bulendu, akizungumza wakati akiwasilisha mada kuhusu umuhimu wa uandishi wa habari jengefu,amesema jamii inahitaji taarifa zenye mizania sahihi pia sauti za vijana zishirikishwe na zisikike katika mambo ya kitaifa.


“Nadhani uandishi huu utatusaidia kuondoka hapa tulipo,wananchi wanataka kuona serikali ikiwajibika na ikija na majibu pia wanahitaji kusikilizwa. Kwa maana hiyo waandishi tunatakiwa kuwa kiunganishi cha makundi yote na kuepuka habari zinazoibua taharuki,”amesema Bulendu 

Kwa upande wake Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini,DCP David Misime,akiwasilisha mada ya wajibu wa vyombo vya habari katika kukuza amani amesema ni pamoja na kuandaa na kutangaza taarifa nyingi zenye maudhui ya kuhımıza na kuimarisha umoja, mshikamano, amanı,utulivu na upendo utakaowezesha maridhiano.


“Yaliyotokea Oktoba 29,2025 hakuna ambaye hakuonja machungu yake.Tumejifunza,binafsi nimejifunza namna ya umuhimu wa amani,”amesema Misime.

DCP.Misime amesema, waandishi wanapaswa kubuni na kukuza majadiliano yanayojenga badala ya kugawa wananchi na taifa,kuzingatia ukosoaji wa kihabari unaojenga na wenye lengo la kuboresha,kuripoti mapungufu bila kuchochea migogoro,kuchambua masuala kwa uadilifu pamoja na kutoa majibu mbadala

Amesema,waandishi wa habari ni watu muhimu na wana mchango mkubwa katika kukuza na kuimarisha usalama, utulivu na amani.


Mwisho.


Saturday, 29 November 2025

HATUTORUHUSU KUTOKEA TENA KWA VURUGU NCHINI- SIMBACHAWENE

11/29/2025 01:28:00 pm

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. George Boniface Simbachawene ametoa wito kwa wananchi na hususani Vijana wa Tanzania kudumisha amani na kuepuka kupanga, kuratibu ama kushiriki kwenye maandamano, akisema kwamba Tanzania bado inakabiliwa na athari kubwa zilizosababishwa na matukio ya Uvunjifu wa amani ya siku ya uchaguzi Mkuu na baada ya uchaguzi huo wa Oktoba 29, 2025.

Waziri Simbachawene amesema hayo usiku wa Ijumaa Novemba 28, 2025 katika burudani ya amani iliyofanyika kwenye Soko la Nyama Choma la Kumbilamoto, Kata ya Vingunguti wilayani Ilala mkoani Dar es Salaam akibainisha kuwa maandamano hayo yalisababisha vifo, uharibifu wa mali za serikali na mali binafsi pamoja na kusimama kwa shughuli za kiuchumi katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Simbachawene ameonya kuwa zipo taarifa za mipango ya maandamano mapya yanayotarajiwa kufanyika Desemba 9, 2025, akisisitiza kuwa Serikali haitaruhusu kutokea kwa vurugu nyingine na kuwaomba wananchi kutotumika na kuchochewa kurudia makosa yaliyopita.

Akirejea athari za maandamano ya Oktoba 29, Waziri Simbachawene amewataka vijana kufahamu gharama kubwa za uharibifu wa miundombinu, ikiwemo kuchoma vituo vya mabasi ya mwendokasi- mradi alioutaja kuwa umejengwa kwa ajili ya wananchi wasio na uwezo wa kumiliki magari. Amefafanua kuwa miradi hiyo inagharimiwa na kodi pamoja na mikopo ambayo vizazi vijavyo vitapaswa kuilipa.

Akizungumzia umuhimu wa amani, Waziri Simbachawene amesema Tanzania inaonekana kuonewa wivu kutokana na mafanikio yake, hivyo wananchi wanapaswa kuepuka kuvuruga misingi ambayo imeijengea nchi heshima na utulivu wa miaka mingi. Ameongeza kuwa baadhi ya majirani wa Tanzania wamekumbwa na migogoro kwa muda mrefu, akisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kujifunza kutokana na changamoto za mataifa hayo.

“Na leo hii nilikuwa na mkutano mkubwa sana wa utatu kati ya Tanzania, Burundi na UNHCR (Shirika la kuhudumia wakimbizi duniani), tunafikiria namna ya kuwarudisha wakimbizi wale wa Burundi kurudi kwao maana wamekaa hapa karibu miaka 40…sasa tunafikiria warudi kwao kwa sababu masharti ya ukimbizi yameisha hawataki kuondoka, tunafikiria kutumia ushawishi wa nguvu ili waweze kuondoka. Kama wakimbizi hawataki kuondoka kwetu halafu sisi hatuienzi na kuiheshimu amani ya nchi yetu tutakuwa sisi ni wajinga wa mwisho kwa sababu tunaona na kusikia kwa wenzetu kinachotokea”, ameeleza.

Katika hatua nyingine, Waziri pia amewasisitiza wananchi kushirikiana na Jeshi la Polisi, akisema polisi ni sehemu ya jamii na wana jukumu la kulinda usalama wa raia na mali zao.

“Shirikianeni na jeshi la polisi, Jeshi la polisi na wananchi ni familia moja kwasababu kazi ya jeshi la polisi ni kulinda usalama wa raia na mali zake, polisi wawe marafiki zetu…ni marafiki zetu sio marafiki zetu? polisi ni watoto wetu, ni ndugu zetu. Tusigombanishwe na polisi, Polisi ni marafiki zetu na nimewaambia polisi, sasa tunataka tuoneshe aina ya jeshi la polisi ambalo linajenga urafiki na wananchi”, amesisitiza Mhe. Simbachawene.

Friday, 28 November 2025

KILA MMOJA YUPO HURU, HATUINGILIWI NA MAAMUZI YA BUNGE LA ULAYA- SERIKALI

11/28/2025 07:47:00 pm

Serikali ya Tanzania imetoa ufafanuzi kuhusu azimio lililopitishwa na Bunge la Umoja wa Ulaya (EU) Novemba 26, 2025, ambalo lilizungumzia madai ya ukiukwaji wa haki za binadamu nchini na kusababisha Kamisheni ya EU kusubirisha kwa muda utiaji saini wa Programu ya Ushirikiano ya Mwaka 2025 (AAP 2025) yenye thamani ya Euro milioni 156.


Serikali imesisitiza kuwa madai hayo hayana uthibitisho wa kuaminika na yametokana na taarifa za upande mmoja ambazo hazikupata fursa ya kupingwa au kupewa ufafanuzi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo, Novemba 27, 2025, na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imeeleza kuwa Serikali ya Tanzania inaheshimu uhusiano baina yake na EU, ambao ni wa kihistoria, wenye zaidi ya nusu karne, na umejengwa juu ya misingi ya mazungumzo, kuheshimiana na kutokuingiliana katika masuala ya ndani ya kila upande.

Imeendelea kueleza kuwa imesikitishwa na hatua ya Bunge la EU kujadili na kupitisha azimio dhidi ya Tanzania bila kuipa Serikali fursa ya kusikilizwa, jambo ambalo linakwenda kinyume na kanuni ya haki ya kusikilizwa (Principal of Natural Justice) inayotambuliwa katika mifumo yote ya utawala bora duniani.

Aidha, Serikali imefafanua kuwa Tanzania ni Taifa huru linaloongozwa kwa misingi ya mamlaka kamili ya kitaifa, hivyo halifungwi na maamuzi ya Bunge la EU na kwamba  kwa mujibu wa taratibu za kidiplomasia, uhusiano rasmi kati ya Tanzania na EU unasimamiwa na Kamisheni ya Umoja wa Ulaya na si Bunge lake, hivyo maazimio ya chombo hicho hayawi maagizo ya moja kwa moja kwa Serikali.

Kuhusiana na mijadala iliyoibuka kuhusu hatima ya misaada ya EU kwa Tanzania, Serikali imeweka wazi kuwa hakuna misaada iliyositishwa; badala yake, Kamisheni ya EU imesubirisha kwa muda utiaji saini wa Programu ya AAP 2025 ili kutoa nafasi ya mashauriano ya ziada.

Serikali imebainisha kuwa programu nyingine zote zilizokwishaidhinishwa na zinazoendelea kutekelezwa hazijaathiriwa na uamuzi huu; hivyo, taarifa zinazoenezwa kuhusu kusitishwa kwa misaada kwa ujumla wake hazina ukweli wowote.

Aidha, Serikali imetoa wito kwa Watanzania kupuuza taarifa potofu zinazoenezwa mitandaoni kuhusu suala hilo.

RIDHIWANI KIKWETE: NIKO TAYARI KUHOJIWA KUHUSU TUHUMA ZA LAKE OIL

11/28/2025 07:39:00 pm

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amesema yuko tayari kuitwa na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ili kujibu tuhuma zinazomhusisha na umiliki wa vituo vya mafuta vya Lake Oil.
Amesema hayo alipokuwa akizungumza na watumishi wa wizara hiyo Novemba 26, 2025, akibainisha kuwa ni muhimu taarifa za watumishi wa umma kuwa wazi. Alisisitiza kuwa pale panapojitokeza sintofahamu, viongozi wanapaswa kuhojiwa na taarifa kuwekwa hadharani ili wananchi wapate ukweli.

“Malalamiko juu ya viongozi yamekuwa mengi sana; haijulikani lipi ni kweli na lipi si kweli,” amesema.

Akitoa mfano, Ridhiwani alisema maandamano yaliyotokea hivi karibuni yalihusisha malalamiko kuhusu maadili ya viongozi, ambapo ilidaiwa kuwa vituo vya mafuta vinavyojulikana kama Lake Oil vinamilikiwa naye.
“Kuna mtu mmoja anaitwa Ali Edha; ana vituo vya mafuta vinavyoitwa Lake Oil, lakini vimechomwa kwa madai kuwa ni vya Ridhiwani,” amesema.
Ridhiwani aliitaka tume hiyo kumuita bila hofu ili kumhoji, huku akipendekeza uchunguzi ufanyike kwanza na baada ya kukamilika waandaliwe waandishi wa habari. Pia alishauri tume iombe ushahidi wa ziada kutoka kwa umma ili kuweka ukweli hadharani.

Thursday, 27 November 2025

MWIGULU AAGIZA MADEREVA WA SERIKALI KUHESHIMU SHERIA ZA BARABARANI

11/27/2025 10:00:00 am

Waziri Mkuu Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba ameonesha kukasirishwa na namna ambavyo Magari ya serikali yanaongoza katika kuvunja sheria za usalama barabarani, akiagiza Maafisa wa serikali kufuata sheria hizo ama kutoa mapendekezo ya sheria hizo kubadilishwa.

Mhe. Nchemba amebainisha hayo leo Jumatano Novemba 26, 2025 wakati wa Kilele cha Maadhimisho ya kwanza ya wiki ya usafiri endelevu ardhini, Hafla iliyofanyika Jijini Dar Es Salaam, akibainisha tabia ya mwendokasi na kutoheshimu sheria na alama za barabarani kwa madereva wa magari ya serikali.

"Mhe. Waziri wa uchukuzi kaeni wadau wote mnaohusika ikiwemo Polisi, kama tunaona Vibao, spidi na sheria nyingine za usalama barabarani zimepitwa na wakati tuzibadilishe kama hazitekelezeki ili tuweke zile tunazotumia." Amesema Dkt. Mwigulu.

Waziri Mkuu ametaka kusiwe na sheria za wananchi wa kawaida na kuwa na sheria ama taratibu za serikali barabarani, akihoji ikiwa sheria na taratibu za barabarani zinakera madereva na watumiaji wengine wa barabara ni nani atakayepaza sauti kueleza changamoto hizo za sheria za usalama barabarani.

WAZIRI SIMBACHAWENE ATEMBELEA VITUO VYA POLISI VILIVYOCHOMWA MOTO OKTOBA 29 DAR ES SALAAM

11/27/2025 09:58:00 am
 
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. George Simbachawene, amewasihi wananchi kudumisha amani na kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kuhakikisha usalama wa Taifa unaendelea kuimarika.

Mhe. Simbachawene ameyasema hayo leo Novemba 25, 2025 katika ziara yake ya kutembelea baadhi ya vituo vya Jeshi la Polisi vilivyochomwa moto jijini Dar es Salaam, ikiwemo vya Ubungo, Temboni, Mbezi Juu na Salasala, kufuatia madhara yaliyotokana na vurugu za Oktoba 29, 2025.

Waziri amesisitiza kuwa uharibifu wa miundombinu ya vituo hivyo umekwamisha utendaji kazi wa baadhi ya vituo, jambo lililosababisha wananchi kushindwa kupata huduma za kawaida kupitia vituo hivyo.

Aidha, Mhe. Simbachawene amewaomba wananchi kuendeleza mshikamano na Polisi, akibainisha kuwa mshikamano huo ndio msingi wa kudumisha amani na usalama wa Taifa.

Ameongeza kuwa uharibifu wa mali za Serikali na wananchi si hasara kwa Taifa tu, bali pia ni upotezaji wa rasilimali muhimu zinazotumika kutoa huduma kwa wananchi.

Aidha, Waziri amesisitiza kuwa Serikali imeanza hatua za haraka kuhakikisha miundombinu ya Jeshi la Polisi inarejeshwa kwa ufanisi, ili usalama wa wananchi udumishwe.

Vilevile, Mhe. Simbachawene amewaomba wananchi kudumisha mshikamano na Polisi na kushirikiana kwa karibu na Jeshi hilo ili kuhakikisha upendo, amani na utulivu wa jamii vinaimarishwa.

Wednesday, 26 November 2025

DKT. MWIGULU AWAONYA WAVUNJIFU WA SHERIA

11/26/2025 06:43:00 pm

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amevitaka vyombo vinavyosimamia usalama barabarani vitekeleze sheria hizo bila upendeleo kwani tabia ya kuogopana na kuoneana aibu imechangia baadhi ya watu kukwepa wajibu wakati wengine wakibebeshwa mzigo wa sheria. 

“Yeyote atakayevunja sheria akamatwe na hatua zichukuliwe kwa usawa. Huyu mmoja anavunja sheria anakamatwa, analipa. Huyu mwingine anavunja mbele yake anaachwa. Kama una haraka, toka mapema zaidi si kufidia kwa kuvunja sheria.”

Ametoa kauli hiyo leo (Jumatano, Novemba 26, 2025) wakati akifungua Maadhimisho ya Kimataifa ya Wiki ya Usafiri Endelevu Ardhini katika ukumbi wa Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.

Amesema kuwa haitakuwa uungwana kuona baadhi ya watu wakilipa adhabu papo hapo wanapokosea ilhali wengine wakiachwa kupita bila kuchukuliwa hatua.

Amewaonya baadhi ya viongozi na madereva wa Serikali ambao wanaelewa sheria vizuri lakini bado wanazikiuka kwa makusudi. “Ni muhimu kuwasaidia watumiaji wa vyombo vya usafiri kama bodaboda na bajaji ambao kwa sehemu kubwa wanaweza kuwa hawazielewi sheria kikamilifu, badala ya kuwaadhibu kwa upendeleo.” 

Dkt. Mwigulu amesisitiza umuhimu wa kuwapa Watanzania wote heshima na kuhakikisha sheria zilizowekwa zinatekelezwa kwa maslahi ya wote na kuongeza kuwa endapo zipo sheria ngumu kutekelezeka, basi zibadilishwe ili kila Mtanzania anufaike. 

Ameviagiza vyombo vya usimamizi wa sheria vihakikishe kuwa watumiaji wote wa vyombo vya usafiri wanazingatia usimamizi wa sheria na kuchukua hatua kwa yoyote anayevunja sheria akamatwe na kuchukuliwa hatua bila kuonewa aibu.

“Inaudhi mtu amebeba mgonjwa anafuata sheria, halafu mwingine anapita tu anavunja sheria, hapati adhabu. Mlalahoi akivunja sheria anapata adhabu, tunawapa kazi watekeleza sheria kuwaomba radhi watu waliovunja sheria. Naelekeza kila mtu afuate sheria, uwe wa serikalini ama uwe binafsi, tumeweka sheria, zifuatwe kama zilivyo.”

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa maadhimisho hayo, Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa alisema sekta ya uchukuzi ni mojawapo ya sekta wezeshi za uchumi duniani kota na kwamba watu wanahitaji njia za uchukuzi ili kusafiri kutoka sehemu moja kwenda nyingine. 

Alisema wizara yake itaendelea kushirikiana na wadau wa usafirishaji nchini ili kuhakikisha masuala ya nishati safi yanapewa kipaumbele. Akitoa mfano, Waziri Mbarawa alisema: “Uendeshaji wa reli ya kisasa (SGR) unatumia nishati ya umeme, mabasi ya mwendokasi njia ya Mbagala yanatumia gesi asili na baadhi ya taxi na bajaji zinatumia gesi asili.”

UJUMBE WA RAIS DKT. SAMIA CHUO CHA MAFUNZO YA KIJESHI MONDULI ARUSHA.

11/26/2025 05:59:00 pm
"Leo nimetunuku Kamisheni kwa Maafisa Wanafunzi 296 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kundi la 06/2022 waliohitimu Shahada ya Sayansi ya Kijeshi (BMS) na Kundi la Kawaida la 72/2024  kwa Cheo cha Luteni Usu katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi, Monduli mkoani Arusha.

Ustawi wetu na maendeleo ya nchi yetu vinategemea sana uwepo wa amani, usalama na utulivu ndani na nje ya nchi, kazi ambayo jeshi letu linaifanya kwa mafanikio makubwa. Nguvu kazi hii mpya ya maafisa itaimarisha zaidi uwezo wetu wa kukabiliana na changamoto za kiusalama zinazoendelea kubadilika.

Ninawapongeza wahitimu wote kwa kukamilisha safari ya mafunzo. Ni imani yangu kuwa mtaendeleza misingi inayolipambanua jeshi letu ya utii, uchapakazi, uhodari, uaminifu na uzalendo.

Mungu Ibariki Tanzania."Amesema Rais Dkt. Samia. 

Tuesday, 25 November 2025

HAYAKUWA MAANDAMANO, ILIKUWA NI HUJUMA ZA KIUCHUMI- DKT. MWIGULU

11/25/2025 05:20:00 pm

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba amesisitiza umuhimu wa kila Mtanzania kuilinda nchi yake, akisisitiza kuwa uharibifu uliofanyika Oktoba 29, 2025 ni zaidi ya maandamano, akiita vurugu hizo kama hujuma za kiuchumi.

Waziri Mkuu Mwigulu amebainisha hayo leo Jumanne Novemba 25, 2025 wakati akizungumza na wahariri na waandishi wa Habari Jijini Dar Es Salaam, akieleza kuwa miundombinu iliyoharibiwa si mali ya serikali bali ni miundombinu yenye kutumika na Kila Mtanzania katika kurahisisha shughuli za kiuchumi na kijamii kote nchini.

"Miundombinu hii si mali ya serikali, zahanati si mali ya serikali, barabara pia hivyo hivyo ndiyo maana hata ukinunua shati la mtoto wako mchanga, ipo sehemu unachangia miundombinu hii." Amesisitiza Dkt. Mwigulu.

Katika hatua nyingine ametaja sehemu ya uharibifu huo uliotokea Oktoba 29, 2025 kuwa ni pamoja na ofisi za serikali 756, Vituo vya mabasi ya Mwendokasi 27,kituo cha uzalishaji Maji safi na salama DAWASCO pamoja na mabasi sita yaendayo haraka Jijini Dar Es salaam.

Aidha uharibifu mwingine ni nyumba binafsi 273, Vituo vya Polisi 159, Vituo binafsi ya uuzaji wa mafuta 672, magari ya watu binafsi 1642, Pikipiki binafsi 2268, pamoja na magari ya serikali 976 ikiwemo magari ya kubebea wagonjwa na ya kutoa huduma nyingine kwa umma.

Kulingana na Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu, wahusika pia walikuwa wamepanga kuchoma kituo kikuu cha Mabasi cha Magufuli Jijini Dar Es Salaam, kuchoma kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi pamoja na maeneo mengine muhimu, akisema rasilimali na mali zote hizo si mali ya serikali, hivyo kila Mtanzania anawajibika kulika rasilimali hizo kwa mustakabali wa maendeleo na ustawi wa kila Mwananchi.

UKOSEFU WA AMANI HUSABABISHA UGUMU WA MAISHA- SONGORO

11/25/2025 03:20:00 pm

Lucas Hamis Songoro, Mkazi wa Ilala Dar Es Salaam amesema Tanzania haikuwahi kuzoea maandamano, fujo na matukio ya uvunjifu wa amani, akitahadharisha athari za Machafuko na ukosefu wa amani kwa maendeleo na ustawi wa wananchi na Taifa kwa ujumla.

"Ni vizuri tukatulia, tukapambana na maisha yetu kwasababu maandamano ya Oktoba 29, 2025 yalitukosesha amani na maisha yakawa magumu hasa katika utafutaji kutokana na kushinda tu nyumbani, kiufupi ni kwamba maisha yalikuwa magumu sana." Amesema Songoro.

Songoro anayejihusisha na biashara ya usafirishaji abiria kwa kutumia pikipiki, maarufu kama bodaboda, amehimiza pia kutumia vyombo rasmi vya kudai haki na usimamizi wa haki zao ikiwemo Wizara mpya ya Maendeleo ya Vijana iliyoundwa, akimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kufungua milango ya maridhiano na kusema suala hilo litumike vyema kupata suluhu ya changamoto zinazowakabili wananchi hususani Vijana.

Songoro anaungana na maelfu ya wananchi wengine wanaolaani matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea wakati na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, wakihimiza amani kama jambo muhimu zaidi na kusema pasipo amani haki haiwezi kupatikana kwa wananchi.

KILICHOTOKEA OKTOBA 29 NI UHALIFU NA UHARAMIA- DKT. MSENGI

11/25/2025 10:39:00 am

Mkuu wa Mkoa mstaafu Dkt. Ibrahim Msengi kwaniaba ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Dar Es Salaam ameeleza kusikitishwa na uvunjifu wa amani uliotokea  siku na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, akiwataka wale wanaodai haki kutekeleza wajibu wao kwanza, huku pia akimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuunda Tume ya uchunguzi kufuatia vurugu za Oktoba 29, 2025.

Dkt. Msengi amebainisha hayo leo Jumatatu Novemba 24, 2025 Jijini Dar Es Salaam wakati wa Mapokezi ya Waziri Mkuu wa Tanzania Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Mkoani humo akisema kilichotokea siku hiyi haikuwa maandamano bali ni uhalifu ulioandamana na ugaidi na kila aina ya uharamia nchini.

"Nishukuru kuwa Mwenyekiti wetu wa CCM Taifa ameshaunda Tume ambayo tunaiamini na ninaamini italeta majibu mazuri na hatua zitachukuliwa. Suala la usalama kwenye Ilani yetu ni suala la msingi na kama hakuna amani na usalama hakuna maendeleo."

"Lakini nikumbushe tu kwamba katika mambo mengi tunayoyasikia mtandaoni, linazungumziwa suala la haki pamoja na kuguswa kidogo suala la amani lakini sijasikia popote wakizungumzia suala la uwajibikaji. Unapotafuta haki lazima uwajibike kama mwananchi, kama raia. Sasa wote waliojitokeza na wale waliowatuma katika vurugu zile sijasikia wakizungumzia suala la uwajibikaji." Amesema   Dkt. Msengi.

Kiongozi huyo mstaafu na Daktari bingwa wa magonjwa ya binadamu kwaniaba ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Dar Es Salaam,  akisisitiza suala la haki kuendana na uwajibikaji, amesema ikiwa kila mmoja atawajibika suala la amani na haki litakuwa na kudumu nchini, akitaka hatua za uwajibikaji zaidi zichukuliwe ili kudumisha tunu hizo za Taifa.

Saturday, 22 November 2025

IGP Wambura awataka Watanzania kutokubali kugawanyika kwa sababu yoyote ile, iwe ya kidini, kisiasa au rasilimali

11/22/2025 01:39:00 pm
Ataka Upendo na mshikamano vidumu kama Desturi ya Watanzania

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Camillus Wambura amewataka Watanzania kutokubali kugawanyika kwa sababu yoyote ile, iwe ya kidini, kisiasa au rasilimali na badala yake waendeleze upendo na amani ya taifa.

IGP Wambura aliyasema hayo Novemba 21, 2025 wakati akifunga rasmi Mafunzo ya Awali ya Askari Polisi Kozi Namba 1/2024/2025 katika Shule ya Polisi Tanzania - Moshi, Kilimanjaro.

IGP Wambura amesema amani ya nchi ni jambo la muhimu hivyo kila mmoja anawajibu wa kuendeleza amani na usalama wa nchi ambayo imedumu kwa muda mrefu tangu tumepata uhuru.

Pia, amewataka watanzania kuendeleza ushirikiano, umoja na mshikamano na Jeshi la Polisi kwa maslahi ya taifa letu.

Aidha, IGP Wambura amewataka askari wahitimu kwenda kutekeleza kwa vitendo yale waliyojifunza kwa kuhakikisha kuwa wanaimarisha usalama wa raia na mali zao kwa kudhibiti vitendo vya kihalifu.

Vilevile, amemshukuru Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, kwa kuendelea kutoa ajira ndani ya Jeshi la Polisi pamoja na kuboresha vitendea kazi, makazi, ofisi na kuboresha maslahi ya askari Polisi.

Jumla ya Askari 4826 wamehitimu mafunzo hayo ya awali yaliyodumu kwa muda wa miezi kumi na mbili ambapo wahitimu hao wamejengewa uwezo katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha usalama wa raia na mali zao unaendelea kuimarika nchini.

4,826 WAHITIMU MAFUNZO YA POLISI MOSHI, IGP AKIONYA KUHUSU UGAIDI NA DAWA ZA KULEVYA

11/22/2025 10:26:00 am

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini Tanzania IGP Camillus Wambura amesema miongoni mwa changamoto watakazokutana nazo wahitimu wapya wa mafunzo ya awali ya Polisi ni pamoja na matishio ya ugaidi wa dunia, uwepo wa dawa za kulevya, usafirishaji haramu wa binadamu na uhamiaji haramu.

IGP Wambura amebainisha hayo  Moshi Mkoani Kilimanjaro alipokuwa akifunga mafunzo ya awali ya Polisi kwa Kozi namba moja ya mwaka 2024/25, akisema kazi za Polisi zinahitaji ushirikiano wa dhati na wa karibu ili kuweza kuzuia na kupambana na changamoto hizo.

IGP Wambura pia akisisitiza kuhusu umuhimu wa usalama kama nyenzo ya maendeleo na ustawi wa Binadamu, ametoa wito kwa wananchi kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi ili kuweza kudhibiti uhalifu na wahalifu kote nchini Tanzania.

" Tusikubali pia kugawanyika kutokana na sababu yeyote ile iwe ya kisiasa, kidini au rasilimali. Tuendelee kutunza tunu yetu ya usalama na amani ya nchi yetu iliyodumu takribani kwa miongo mingi sasa. Tushirikiane popote kuhakikisha tunakuwa salama." Amesisitiza IGP Wambura.

Awali wakati wa maelezo yake, Mkuu wa Chuo hicho Ramadhan Mungi  amesema askari wapya 4, 826 wakiwemo wanaume 3, 436 na wanawake 1, 390 wamehitimu mafunzo hayo, huku wanafunzi 217 wakiondolewa chuoni hapo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ukosefu wa nidhamu na uwezo mdogo katika kujifunza.

Friday, 21 November 2025

ZAIDI YA WAGENI 500 WAHUDHURIA KONGAMANO LA DINI ARUSHA, WASIFU AMANI NA UTULIVU

11/21/2025 08:50:00 pm

 Wakaribisha wengine nchini wakiwataka kuachana na upotoshaji wa Mtandaoni* 

Zaidi ya Wageni 500 kutoka kwenye Mataifa mbalimbali ya Barani Afrika na nje ya Afrika wamekutana kwa siku mbili Mkoani Arusha kwenye Kongamano la kujadili kuhusu mchango wa dini katika uchumi na maendeleo, wengi wakifurahia amani na utulivu walioushuhudia nchini tangu kuwasili kwao siku tano zilizopita.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, miongoni mwa washiriki hao kutoka nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na nchini Senegal, wameeleza kuwa Kongamano hilo lilitaka kuahirishwa kutokana na kile walichokuwa wakikiona kwenye Mitandao ya Kijamii.

"Wakati tunakuja Tanzania tulisikia vitu vingi, tukaangalia kwenye runinga na tukaona habari za uwepo wa machafuko, tukawa na wasiwasi wa Kongamano letu kiasi cha kuanza kufikiria kuahirisha lakini tunamshukuru Mungu tumefika na tumekuta amani ya kutosha na Mungu ni mwema sana kwasababu amewezesha amani Tanzania, tunamshukuru sana Mungu." Amesema Joela Athumani, Raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Bi. Joela amewataka watanzania kuishikilia kwa nguvu baraka ya amani waliyobarikiwa na Mwenyenzi Mungu, akiwataka wale wote waliokuwa wamepanga kuja nchini kutokuwa na wasiwasi wowote wa kiusalama kwani hali ni shwari na shughuli zinaendelea kama kawaida.

Kwa upande wake Bw. Ogi Kabongo, Mkazi wa Kinshasa nchini DRC,  ameeleza athari za ukosefu wa amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, akiwataka Watanzania kudumisha amani ya Tanzania kwa gharama yoyote ile kwani ukosefu wa amani unadhorotesha na kuua kabisa ustawi na maendeleo ya wananchi.

Aidha Bw. Fransis Owusu, Raia wa Senegal na Rais wa Full Gospel Business Men's Fellowship International ameitaka Jamii kuendelea kuiombea amani ya Tanzania, akisema amani hiyo mara zote imekuwa msingi muhimu wa maendeleo na kiwezeshi kikubwa cha mafanikio katika shughuli za kiuchumi

UVUNJIFU WA AMANI USIWEPO TENA TANZANIA- MATUKU

11/21/2025 01:28:00 pm

Bi. Zawadi Matuku, Mfanyabiashara wa Chanika kwa Ngwale Mkoani Dar Es Salaam ameishukuru serikali na Vyombo vya ulinzi na usalama kwa udhibiti wa amani na utulivu nchini, akisema kilichotokea wakati na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 hakuwahi kukizoea kwani Tanzania inasifika kwa amani na utulivu kote duniani.


Matuku ameyasema hayo wakati akieleza uzoefu wake dhidi ya uvunjifu wa amani uliojitokeza, akisema kwamba aliamini siku hiyo ya upigaji kurwa ungekuwa wa amani na wafanyabiashara wangeendelea na shughuli zao kama kawaida baada ya kupiga kura.

Ameomba suala hilo kutokujirudia tena, akiwahamasisha Vijaba kujiepusha na mikumbo na kuwataka kutumia muda wao mwingi katika kujiendeleza kiuchumi na kusimamia ustawi wa maisha yao badala ya kutumika na makundi yasiyoitakia mema Tanzania.

Vijana wazidi kupaza sauti kukemea maovu na wanaotishia amani ya Nchi.

11/21/2025 01:19:00 pm

Vijana wamehamasishwa kuwa mstari wa mbele katika kukemea maovu na kulinda amani na utulivu uliopo nchini pamoja na kujiepusha na makundi yenye kutenda Vitendo visivyokubalika kisheria na vyenye kuhatarisha amani ya Tanzania.

Kauli hiyo imetolewa kufuatia matukio ya uvunjifu wa amani yaliyojitokeza kwenye Miji mbalimbali ya Tanzania wakati na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, suala ambalo limemlazimu Rais Samia Suluhu Hassan kuunda Tume maalum kufuatilia chanzo cha vurugu kutokana na kuwa tukio lililowagharimu wengi.

Akizungumza na waandishi wa habari, Bw. Hamis Jumanne, Mkazi wa Kichangani, Temeke amewaomba Vijana kuyakataa makundi yanayotishia amani ya Tanzania, akiwataka kutumia muda wao mwingi kujiendeleza kiuchumi badala ya kutumika kuharibu amani.

Jumanne amesisitiza kutafuta namna nzuri ya kushughulikia matatizo na mapungufu yaliyopo kwa namna ifaayo na isiyoharibu tunu za Taifa, akihimiza mazungumzo zaidi kati ya wananchi na Viongozi katika kutatua kero zilizopo.

TIRA YAITAKA JAMII KUONDOA DHANA POTOFU KWAMBA BIMA NI YA MATAJIRI"

11/21/2025 11:12:00 am
MAMLAKA ya Usimamizi wa Bima Tanzania(TIRA)imetoa rai kwa vyombo vya habari nchini kuunga mkono jitihada za TIRA katika kutoa elimu ya bima kwa umma ili kuondoa dhana ya upotoshaji kuhusu ukubwa wa gharama za bima,ucheleweshaji wa malipo pamoja na dhana ya kuwa bima ni kwajili ya matajiri tu kitu ambacho siyo kweli.

Wito huo umetolewa jijini hapa jana na Kamishna wa Bima Dkt.Baghayo Saqware wakati akifungua mafunzo ya Wahariri wa Habari Tanzania kuhusu masuala ya Bima na Umuhimu wa Taarifa ya Soko la Bima.

Dkt.Baghayo alisema Elimu ni ufunguo wa kuongeza uelewa na matumizi ya bima nchini hivyo alitoa wito kwa wahariri 
Kuongeza weledi katika uandishi wa masuala ya bima.

"TIRA ipo tayari kushirikiana nanyi katika kutoa mafunzo na taarifa muhimu,Toeni kipaumbele kwa habari za bima. Haya ni masuala yanayogusa maisha ya wananchi wote kutoka mfanyabiashara mdogo hadi mwekezaji mkubwa.

"Fichueni Wadanganyifu katika bima kwa kufuatilia kwa karibu kesi mbalimbali zinazoendelea kwenye Mahakama zetu. Endeleeni kutumia Taarifa ya Soko la Bima kama nyenzo ya uchambuzi wa habari na  taarifa hizi ni msingi mkubwa wa uandishi wenye tija,"alisema Dkt.Baghayo.

Aidha alisitiza kuwa ushirikiano kati ya TIRA na vyombo vya habari ni muhimu sana katika kuifanya sekta ya bima kuwa chachu ya maendeleo ya taifa.

Hivyo alisema Kupitia majadiliano kama hayo,wanaweza kujenga taifa lenye uelewa mpana wa bima, kuongeza matumizi ya huduma hizi, na hatimaye kuimarisha ustawi wa wananchi.

Kwa upande wake Msuluhishi wa Migogoro ya Bima Tanzania kutoka Ofisi ya Usuluhishi wa Migogoro Tanzania(TIO),Margaret Mngumi alisema kuwa TIO imekuwa kiungo muhimu kati ya wananchi, kampuni za bima na Serikali, na imechangia kwa kiasi kikubwa katika kuimarisha uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika utatuzi wa migogoro ya bima hapa nchini.

Huku akitaja lengo kuu la uwepo wao katika mafunzo hayo kuwa ni kuweka msingi imara wa ushirikiano kati ya TIO na vyombo vya habari ili kwa pamoja kuijenga Tanzania yenye uelewa mpana zaidi kuhusu haki, wajibu na taratibu za kudai fidia za bima.

"Vyombo vya habari vina nafasi ya kipekee katika,Kufikisha elimu sahihi kwa wananchi kuhusu hatua za kudai fidia,Kusaidia kupunguza malalamiko yasiyo na msingi kwa kutoa taarifa sahihi, Kuelimisha umma dhidi ya udanganyifu wa madai ya bima (insurance fraud) na Kuimarisha uwajibikaji wa kampuni za bima kupitia uandishi wa uwazi na wa haki,

"TIO inatambua nguvu mlizo nazo, na tungependa leo tuanzishe ukurasa mpya wa ushirikiano, ili kuboresha zaidi mazingira ya utatuzi wa migogoro ya bima kwa maslahi ya Watanzania,"alisema Mngumi. 

Pamoja na hayo Mngumi alisema kuwa 
Kwa niaba ya Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima,wako tayari kufanya kazi bega kwa bega na waandishi, wahariri na vyombo vya habari vyote katika kusambaza elimu, kutoa taarifa za kitaalamu na kushirikiana katika kutatua changamoto zinazoathiri sekta ya bima.

Mwisho.
Adbox