DOREEN BLOG

HABARI, MICHEZO NA BURUDANI

Adbox

Monday, 27 October 2025

CWT YAWAHAKIKISHIA WATANZANIA USHIRIKI WA UCHAGUZI MKUU OKTOBA 29, 2025

10/27/2025 11:17:00 am

Chama cha waalimu nchini Tanzania CWT kimewataka waalimu kote nchini kuendelea na msimamo wao wa kujitokeza kwa wingi tarehe 29 Oktoba, 2025 kwenda kupiga kura kwani ndiyo msimamo wa Chama ambao ulikwisha tolewa na Msemaji wa Chama hicho ambaye ni Rais wa Chama Cha waalimu nchini Tanzania Bw. Suleiman Ikomba.

Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu wa CWT Mwalimu Joseph Misalaba kwenda kwa Makatibu wa CWT, Mikoa na Wilaya imesisitiza waalimu pia na umma kwa ujumla kuwa Mabalozi wazuri wa Upendo, amani, umoja na mshikamano kwaajili ya maendeleo thabiti ya Tanzania kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye, wakiishukuru pia serikali kwa kuendelea kutatua kero za waalimu kwa kushirikiana na CWT.

Taarifa ya Katibu Mkuu wa CWT imekuja baada ya kuzuka kwa uvumi mitandaoni zikieleza kuwa Chama Cha Waalimu kimesusia uchaguzi Mkuu wa Keshokutwa Jumatano, ambapo Mwalimu Misalaba amekanusha taarifa hizo na akitaka Watanzania wazipuuzie.

"Chama Cha Waalimu Tanzania kinapenda kukanusha kwa nguvu zote taarifa zinazosambaa kupitia Mitandao ya kijamii na kwenye baadhi ya Vyombo vya habari ikihamasisha walimu kutoshiriki kwenye shughuli za uchaguzi Mkuu ambazo baadhi ya waalimu hutumika kama wasaidizi wa shughuli za uchaguzi kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za serikali ya Tanzania." Amesema Katibu Mkuu huyo.

Mwalimu Misalaba pia ametoa rai kwa waalimu, wamachama wa CWT na watanzania wote kwa ujumla kupuuza taarifa hizo kwani hazina ukweli wala msingi wowote, akisema zinalenga kuleta taharuki, uzushi na uchonganishi ambao unapaswa kupingwa kwa nguvu zote ili kuendelea kulinda amani, umoja na utulivu ambao ni tunu ya Taifa.

CWT imewahakikishia waalimu, serikali na wananchi wote kuwa kitaendelea kushirikiana na mamlaka husika katika kuhakikisha kuwa tabia ya utoaji wa taarifa potofu inakomeshwa ili kulinda misingi na madhumuni ya uwepo wa vyama vya Wafanyakazi kwa mujibu wa sheria na kanuni za nchi.

VIONGOZI WA DINI SINGIDA NA DODOMA WAHIMIZA AMANI KUELEKEA UCHAGUZI MKUU

10/27/2025 11:15:00 am

Zikiwa zimesalia siku nne pekee kabla ya Watanzania kujitokeza kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, baadhi ya viongozi wa dini kutoka Mikoa ya Singida na Dodoma wamewataka vijana kuepuka vishawishi vyovyote vinavyoweza kusababisha uvunjifu wa amani, wakisisitiza kwamba utulivu wa Taifa ni msingi wa maendeleo na umoja wa kitaifa.
Wakizungumza leo jijini Dodoma katika kongamano la viongozi wa dini mbalimbali kutoka Kanda ya Kati, viongozi hao wamehimiza vijana na wananchi kwa ujumla kuendelea kutimiza majukumu yao ya kijamii na kidini, huku wakielimisha jamii kuhusu umuhimu wa kulinda amani kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi.

Akitoa wito huo, Askofu Evance Chande wa Kanisa la Carmel Assemblies of God alisema vijana ndio nguvu kazi ya Taifa, hivyo wanapaswa kutumia nafasi yao kujenga badala ya kubomoa.

“Tunapaswa kuikumbatia amani kama tunavyokumbatia imani zetu. Uchaguzi ukipita, Tanzania inabaki kuwa moja, hivyo tusikubali kugawanywa kwa misingi ya kisiasa,” alisema Askofu Chande.

Kwa upande wake, Sheikh Mustapha Rajab, Sheikh wa Mkoa wa Dodoma ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maridhiano Kanda ya Kati na mgeni rasmi wa kongamano hilo, aliwahimiza wananchi kutii mamlaka na kufuata taratibu zinazotolewa na Serikali pamoja na viongozi wa dini.

 “Amani si jambo la bahati mbaya, ni matokeo ya utii na hekima. Tukitii viongozi wetu na kuheshimu sheria, Taifa litaendelea kubaki salama,” alisema Sheikh Rajab.

Kongamano hilo lililolenga kuliombea Taifa amani na utulivu kuelekea uchaguzi, lilibebwa na kaulimbiu isemayo “Kupiga kura ni haki ya kila Mtanzania, amani na utulivu ni jukumu letu.
Viongozi hao walikubaliana kuwa jukumu la kulinda amani si la Serikali pekee, bali ni la kila mwananchi, na wakasisitiza umuhimu wa maombi, maelewano, na uvumilivu wakati wote wa mchakato wa uchaguzi.

Saturday, 25 October 2025

HAKI HAIPATIKANI KUPITIA VURUGU NA MAANDAMANO- TWARIQA TANZANIA

10/25/2025 05:22:00 pm

Kiongozi Mkuu wa Taasisi ya Twariqa Tanzania, Sheikh Said Hamis Migire, amesisitiza umuhimu wa Kila Mtanzania kuwajibika katika kudumisha amani na utulivu kabla, wakati wa upigaji wa kura na hata baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025 akifananisha amani na yai ambalo likivunjika ni vigumu kulirejesha katika hali yake ya awali.

Akizungumza na waandishi wa habari pembezoni mwa dua maalumu ya kuombea amani iliyofanyika katika Zawia Kuu, Makao makuu ya taasisi hiyo jijini Arusha, na kuhudhuriwa na mamia ya waumini kutoka maeneo mbalimbali nchini, Sheikh Migire amesema ni muhimu kila Mtanzania kujiepusha na vurugu na viashiria vingine vyovyote vyenye kutishia tunu za Taifa, akihimiza kutafakati kabla ya kuchukua hatua yoyote inayoenda kinyume na tamaduni na ustaarabu.

“Amani ni kama yai likivunjika ni ngumu sana kulirudisha. Tumeona mataifa mengi ya Afrika yaliyopoteza amani, na sasa wanajuta." Amesema.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Twariqa Taifa, Sheikh Haruna Hussen ametoa wito kwa viongozi wa dini nchini kuungana kwa pamoja katika maombi ya kuombea amani, akisisitiza kuwa jukumu la kulinda amani ni la kila Mtanzania.

“Na sisi kama viongozi wa dini tunao wajibu wa kuhubiri amani usiku na mchana. Amani ni msingi wa taifa.
Tunawaomba Watanzania wasidanganyike bali tushike amani yetu kwa mikono miwili." Amesema Sheikh Haruna.

TUKAE PAMOJA KUOMBEA AMANI- KARDINALI RUGAMBWA

10/25/2025 05:20:00 pm

Mwadhama Protase Kardinali Rugambwa, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora nchini Tanzania amesisitiza umuhimu wa Jamii kuombwa amani ya Tanzania na mshikamano Miongoni mwa watanzania kama ambavyo Vitabu vitakatifu vilivyoagiza kukaa pamoja kwa umoja.

Kardinali Rugambwa amebainisha hayo leo Oktoba 24, 2025 wakati wa Kongamano la maombi lililofanyika Tabora na kukusisha waumini wa dini na madhehebu mbalimbali Mkoani humo wakati huu wa kuelekea kwenye uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.

"Sisi ni watoto wa baba mmoja, tukae pamoja na kuwa tayari kufanya mambo pamoja ikiwemo amani, haki, upendo, ushirikiano, kwamba umoja ambao ni tunu ya Taifa letu idumu lakini pia uwepo wa mashirikiano na kukaa kwa pamoja kama ndugu kusikilizana pale kwenye matatizo na pale palipo na shida ama matatizo tuone namna gani ya kuyashughulikia." Amesema Kardinali Rugambwa.

Kiongozi huyo wa dini nchini Tanzania ameongeza pia kwamba kuombea amani ni maelekezo ya Baba Mtakatifu wa Kanisa Katoliki duniani Papa Leo, ambaye amekuwa akionesha kwa vitendo namna ambavyo amekuwa akishirikiana na Viongozi wa dini nyingine kukaa na kusali pamoja kwa kukuza imani zao kwa Mungu mmoja ambaye kila muumini wa dini amekuwa akimuamini pamoja na kuimarisha na kukuza maridhiano miongoni mwa jamii sambamba na kuombea amani.

MULIRO AONYA WANAOPANGA KUANDAMANA NA KUFANYA VURUGU DSM

10/25/2025 05:20:00 pm

Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro amewaonya wale wote wanaopanga, kuratibu ama kutaka kushiriki kwenye uvunjifu wa amani ikiwemo kufanya vurugu na maandamano Oktoba 29, 2025, akisema Jeshi hilo limekula kiapo kulinda nchi pamoja na raia na mali zao.

Kamanda Muliro ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Oktoba 24, 2025 wakati wa kongamano la Vyuo na Vyuo Vikuu kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, Kongamano lililofanyika kwenye Ukumbi wa Ubungo Plaza na kuwashirikisha wanafunzi wa shule za Sekondari, Vyuo na Vyuo Vikuu, akiwataka Vijana pia kuwa waangalifu na kutafakari kuhusu misukumo na mihemko yao kulingana na aina na makundi ama watu wanaoambatana nao.

"Tukiwa kama watu tuliokula kiapo tunawaleza kuwa tutatimiza jukumu letu la kuhakikisha kuwa watu wanakuwa salama, watu wajitokeze kwa wingi kupiga kura, wafuate sheria na sisi tutakuwepo barabara kuwalinda wote wanaoenda kutimiza jukumu lao la Kikatiba la kwenda kupigakura. Siku hiyo kutakuwa hakuna maandamano wala hakuna vurugu, siku hiyo ni ya upigaji wa kura bila hofu."Amesema.

Kama Muliro pia amesisitiza kuwa Vijana kuwa na fikra chanya ama hasi katika kujadili jambo fulani sio kitu kibaya ila kuipeleka mitazamo hasi kwenye vitendo vya vurugu ndiyo kosa kisheria, akiwataka pia Vijana kulinda hatma zao kwa kuhakikisha nchi inakuwa na amani ili kuwawezesha kutimiza malengo na ndoto zao kiuchumi, kisiasa na Kijamii.

Friday, 24 October 2025

DC KARANGA AWAHAKIKISHIA WANANCHI USALAMA, WALIOPOTEZA KADI ZA MPIGAKURA WAITWA VITUONI

10/24/2025 11:27:00 am

Mkuu wa Wilaya ya Karatu Mkoani Arusha Mhe. Dkt. Lameck Ng'ang'a Karanga, amewahakikishia usalama na mazingira tulivu wananchi wote wa Wilaya hiyi katika Kipindi cha lala salama cha Kampeni za Uchaguzi Mkuu, wakati wa Upigaji kura na hata baada ya Mchakato huo kukamilika, akiwataka wananchi kupuuza Taarifa za Mitandaoni za kutokuwa na uchaguzi Jumatano Ijayo Oktoba 29, 2025.

Dkt. Karanga ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake akisisitiza pia wapigakura wote kurejea Majumbani mara baada ya kukamilisha zoezi la Upigaji wa kura na kuachana na baadhi ya hamasa zinazofanywa kwenye Mitandao ya Kijamii kutoka kwa baadhi ya wanasiasa wanaohamasisha wafuasi wao kusalia vituoni kulinda kura suala ambalo ni jukumu la Polisi na Tume huru ya Taifa ya uchaguzi nchini Tanzania.

Kwa upande wake Bi. Farida Kimambo, Msimamizi wa uchaguzi Wilaya ya Karatu, ameeleza kuwa maandalizi ya uchaguzi Mkuu 2025 yamekamilika, akisema vituo vya kupigia kura ni vile vilivyotumika kujiandikishia, akiwataka wananchi kufika sasa kwenye Vituo hivyo kuhakiki Taarifa na Majina yao.

"Mpigakura ambaye kitambulisho chake kimepotea ama kuharibika anaweza kupiga kura kwa kutumia leseni ya udereva, pasi ya kusafiria au kitambulisho cha NIDA ili aweze kupiga kura lazima awe amejiandikisha kwenye daftari la mpigakura na lazima jina alilojiandikishia liwe limefanana na Jina la kwenye Kitambulisho, leseni au pasi yake ya kusafiria." Amesema Msimamizi huyo wa uchaguzi.

Bi. Kimambo pia ameeleza kuwa Oktoba 25, 2025 watakuwa na semina ya mafunzo kwa makarani waongoza wapigakura kura kwenye Vituo vya Kupigia kura na Oktoba 26 na 27 watafanya mafunzo mengine kwa wasimamizi wa Vituo na wasaidizi wasimamizi wa Vituo ili kuhakikisha wanakuwa na uelewa wa pamoja na kuyafahamu majukumu yao wakati wa zoezi la upigaji kura hapo Oktoba 29, 2025. 

Thursday, 23 October 2025

USAFIRI WA SGR DAR ES SALAAM- DODOMA WAREJEA, TRC YAOMBA RADHI KWA USUMBUFU

10/23/2025 04:35:00 pm

Shirika la reli Tanzania limeufahamisha umma wa Watanzania kuwa huduma za usafiri wa treni za SGR zimerejea na kuendelea kama kawaida, likiomba radhi kwa wateja wake kwa usumbufu uliojitokeza, shirika likiwashukuru pia Wananchi kwa uvumilivu wao katika kipindi ambacho huduma za usafiri huo zilipotatizika kutokana na hitilafu iliyotokea mapema leo Alhamisi Oktoba 23, 2025.

Mapema leo Shirika la Reli Tanzania lilitoa taarifa kwa Vyombo vya habari likieleza kuhusu ajali ya Treni ya EMU iliyokuwa ikisafiri kutoka Dar Es Salaam kwenda Dodoma majira ya saa mbili asubuhi kutokana na hitilafu za uendeshaji, tukio ambalo lilitokea Kituo cha Ruvu na kwa taarifa za shirika hilo hakukuwa na athari kubwa za ajali hiyo.

Timu ya wataalamu ikiongozwa na Katibu Mkuu wa uchukuzi, Mkurugenzi wa shirika la TRC, Vyombo vya ulinzi na usalama na menejimenti ya TRC ilianza haraka kushughulikia changamoto hiyo na kufanya na uchunguzi wa kina wa kuhakikisha kuwa huduma hizo zimerejea haraka.

RC Malima atoa Onyo kali kwa wanaoratibu vietendo vya uvunjifu wa Amani uchaguzi mkuu

10/23/2025 12:43:00 pm

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima, ametoa onyo kali kwa makundi au watu wenye nia ya kuanzisha fujo ama vurugu wakati wa kipindi cha uchaguzi Mkuu wa Tanzania, akisisitiza kuwa vyombo vya ulinzi na usalama vipo imara na makini kuhakikisha amani na utulivu vinaendelea kudumishwa nchini.

Malima ametoa kauli hiyo leo Jumatano Oktoba 22, 2025, wakati wa Kongamano la Amani kuelekea Uchaguzi Mkuu, lililoandaliwa na Taasisi ya Ukumbusho wa Zakkat Tanzania na kufanyika mkoani Morogoro, akisema kuwa baadhi ya watu wanaojaribu kuvuruga amani nchini ni watu wanaoshawishiwa na kuiga matendo kutoka nje, na hawana nia njema na Taifa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT), Sheikh Alhad Mussa , amesema watanzania wanapaswa kukataa kwa nguvu zote watu wanaoeneza chuki na kuhatarisha maisha ya wengine, hasa katika kipindi hiki nyeti cha uchaguzi.

Naye Askofu Mteule wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Morogoro, Dkt. George Pindua, ameahidi kuwa viongozi wa dini wataendelea kuhubiri amani, mshikamano na upendo ili kuhakikisha uchaguzi unafanyika katika mazingira ya utulivu.

NDANI YA MIAKA MINNE YA DKT. SAMIA MADARAKANI UCHUMI UMEPAA- PROF. ASSAD

10/23/2025 12:21:00 pm

 _Agusia tatizo la ukosefu wa Ujuzi kwa wahitimu_ 

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu Morogoro (MUM) na Mkaguzi Mkuu mstaafu wa hesabu za serikali (CAG)  Profesa Mussa Juma Assad, amesema hali ya uchumi wa Tanzania kwa sasa kwa miaka hii minne ya serikali ya awamu ya sita chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan ni nzuri ukilinganisha na miaka ya nyuma, huku ukuaji wa uchumi ukiendelea kwa kasi na mfumuko wa bei ukiwa katika viwango vinavyoridhisha.

Akizungumza na waandishi wa habari kando ya Kongamano la Kitaaluma la kujadili Utekelezaji wa Uchumi Jumuishi kuelekea Dira 2050, lililoandaliwa na MUM kwa ushirikiano na Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Binafsi (PPPC), Profesa Assad amesema uchumi wa nchi umekua kwa wastani wa asilimia 6 katika kipindi cha miaka minne iliyopita suala ambalo limesaidia watanzania kuendelea kupata mahitaji yao muhimu kama Vyakula, elimu ma mahitaji mengine.

“Kwa jumla uchumi wa Tanzania umekuwa kwa wastani wa asilimia sita. GDP, kupanda na kushuka kwa pato la taifa kumekaa vizuri ukilinganisha na nchi jirani. Hali ya kiuchumi ni nzuri zaidi kuliko Kenya na Rwanda,” amesema Profesa Assad.

Profesa Assad amesema kuwa vigezo vya kiuchumi vya sasa vinaonyesha uwezo bora zaidi wa wananchi kuendesha maisha yao ukilinganisha na miaka ya nyuma, jambo linalodhihirisha uimara wa uchumi wa nchi.

Aidha Profesa Assad ameeleza kuhusu changamoto ya vijana wanaohitimu vyuo vikuu kukosa ujuzi wa vitendo, akibainisha kuwa tatizo siyo kutokuwa sehemu ya uchumi, bali kukosa stadi za kazi, akisema Vijana wanaotoka Vyuoni wanapaswa kupewa mafunzo ya ujuzi kwa vitendo baada ya kumaliza masomo akisema jambo hili linapaswa kubebwa na serikali na sekta binafsi kwa kutoa kozi na fursa fupi za Vijana hao kujifunza zaidi kwa vitendo masuala mbalimbali ili kupata ujuzi.

Wednesday, 22 October 2025

WAHADZABE WA KARATU WAISUBIRI KWA HAMU OKTOBA 29

10/22/2025 12:32:00 pm

Jamii ya Wahadzabe wanaopatikana kwenye eneo la Mang'ola Wilayani Karatu Mkoani Arusha wameahidi kujitokeza kwa wingi kutimiza haki yao ya Kikatiba ya kuchagua Viongozi katika uchaguzi Mkuu wa Jumatano ijayo Oktoba 29, 2025.

Wananchi hao wametoa kauli hiyo leo Jumatano Oktoba 22, 2025, wakiishukuru serikali pia kwa kuwakumbuka na kuwajumuisha katika zoezi hilo la Kikatiba licha ya kuishi kwao maeneo ya pembezoni na Jamii nyingine, wakisema wanatarajia kushiriki kwenye uchaguzi huo kikamilifu ili kuwachagua Viongozi wanaoweza kuwaletea maendeleo.

"Kwaniaba ya wenzangu Jamii ya Wahadzabe niwahakikishie kuwa tutaenda kupiga kura tarehe 29 na tutachagua Viongozi watakaoenda kutuangalia sisi kwa ujumla Wahadzabe wote ili tufanikiwe kimaendeleo kwasababu sisi tunaishi porini na hatujui mengi yanayoendelea kwahiyo tutawachagua wanaoweza kutuletea maendeleo huku." Amesema mmoja wa wananchi wa Jamii hiyo.

Kwa upande wao Ruben Mathayo, Mwenyekiti wa Jamii ya Wahadzabe Tanzania na Mariam Anyanyire, Mhamasishaji ndani ya jamii hiyo, wameeleza kuwa muamko ni mkubwa kwa jamii hiyo kuelekea uchaguzi Mkuu wakiahidi kuwa kila mwenye haki na sifa ya kupiga kura atajitokeza siku hiyo kuwachagua Viongozi wanaowataka.

HATUTOWAACHA SALAMA WANAOPANGA KUVURUGA UCHAGUZI MKUU- RC SENDIGA

10/22/2025 10:58:00 am

Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Cuthbeth Sendiga ameonya Vikali wale wote ama Vikundi vinavyopanga au kuratibu kufanya vurugu na fujo wakati wa Oktoba 29, 2025, siku ya Uchaguzi Mkuu wa Tanzania,  akiwahakikishia wananchi wa Mkoa huo usalama na mazingira tulivu kuanzia sasa, siku ya upigaji kura na hata baada ya kukamilika kwa mchakato wa uchaguzi Mkuu.

Mhe. Sendiga ametoa kauli hiyo leo Jumanne Oktoba 21, 2025 wakati akizungumza na waandishi wa habari Mjini Babati kuhusu maandalizi mbalimbali ya kiserikali kuelekea uchaguzi Mkuu, akihimiza ushirikiano zaidi kati ya serikali, Wananchi, Vyama vya siasa na wadau wengine kuelekea kwenye uchaguzi huo Mkuu wa wiki ijayo Oktoba 29, 2025.

"Kama serikali tunawajibu wa kukemea mapema, yeyote ama kundi linalopanga kufanya vurugu kwa kujishawishi mwenyewe ama kushawishiwa kwa makusudi ama kwa bahati mbaya kwenda kutufanyia vurugu katika siku hii, sisi kama serikali tunatoa onyo kubwa na kali kabisa hatutokuacha salama na hatutakuvumilia. Amua mapema unakuja Mtaani tukutane ama tupige kura kwa amani turudi nyumbani.

"Hatutamvumilia atakayevuruga siku hii maalumu kwa upigaji wa kura. Mkoa wa Manyara ni "Wrong number",kamwe usijaribu kuvuruga siku hii ya neema na baraka kwa wananchi kuamua hatma ya miaka yao mitano ijayo." Amesema Mhe. Sendiga.

Mhe. Sendiga pia ametoa wito kwa wananchi wote wenye sifa kujitokeza kwa wingi kupiga kura na kusisitiza umuhimu wa kurejea nyumbani na kuendelea na shughuli nyingine badala ya kuendelea kujihusisha na uvunjifu wa sheria ikiwemo kusalia vituoni kama ambavyo baadhi ya Vyama vya siasa vinavyoshawishi wanachama wao kusalia vituoni ili kulinda kura suala ambalo ni kinyume na miongozo ya uchaguzi Mkuu.

Tuesday, 21 October 2025

WANNE JELA MIAKA SABA KWA JARIBIO LA KUMTEKA MFANYABIASHARA

10/21/2025 06:38:00 pm

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni, Kinondoni, Dar Es Salaam imewahukumu Vijana wanne wakiwemo Mabondud 3ia wawili kifungo cha miaka saba jela baada ya kupatikana na hatia ya kujaribu kumteka Mfanyabiashara Deogratus Tarimo, tukio lililoteka hisia za wengi Mitandaoni, wengi wakiwahusisha watu hao na Maafisa wa Vyombo vya ulinzi na usalama nchini.

Vijana hao waliohukumiwa ni Fredrick Nsato (21) Mkazi wa Kibamba, Isaack Mwaifuani (29) Mkazi wa Kimara, Benki Mwakalebela (40) na Bato Twelve (32) Mkazi wa Kimara Bonyokwa Mkoani Dar Es Salaam.

Kabla ya Hakimu Mkazi Mkuu Ramadhani Rugemalira kusoma hukumu hiyo, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Daisy Makakala amesema pamoja na kuwa hana kumbukumbu za makosa ya nyuma ya watuhumiwa wote wanne lakini anaiomba mahakama itoe adhabu sawa na kifungu cha sheria walichoshtakiwa nacho ili jamii ya Tanzania na dunia nzima ifahamu kuwa wanaotenda vitendo vya utekaji wa Raia wa makundi mbalimbali siyo Maafisa waJeshi la Polisi, bali ni watu wa kawaida ambao wamekuwa wakifanya vitendovya kiuhalifu kwa sababu mbalimbali.
"Naomba mahakama iwape adhabu kali washtakiwa kwa sababu vitendo vya utekaji vimeshamiri sana nyakati hizi, hali inayopelekea Jeshi la Polisi kulaumiwa kwa utekaji huo. Hawa watuhumiwa wangefanikiwa kumkamata Deogratius Tarimo akapotea asionekane Jamii ingeamini kuwa ni Polisi ndiyo wamempoteza hasa na vile wakati wanamkamata walikuwa wakijitambulisha kama Askari Polisi toka Kituo cha Gogoni wakati wakijua ni uongo. Hivyo ili kutoa fundisho kwa hawa watuhumiwa waliokutwa na hatia na jamii yote kwa ujumla mahakama iwape adhabu kali."amesema Wakili Makakala.

Kwa upande wao washtakiwa wao waliomba wapunguziwe adhabu na kudai kuwa wao walikuwa wanasaidia kumteka tu baada ya rafiki yao Frederick kuwaomba wamsaidie kumteka, kwa madai kuwa wanahisi Deo alitembea na mke wa rafiki yake Fredrick.

Kwa mujibu wa hati ya Mashtaka, Fredrick na wenzake walitenda kosa hilo Novemba 11, 2024 eneo la Kiluvya Madukani Lingwenye, lllilopo Wilaya ya Ubungo ambapo Ilielezwa kuwa siku hiyo ya tukio katika eneo hilo, washtakiwa kwa pamoja walijaribu kumteka mfanyabiashara Deogratius Tarimo kwa nia ya kumuweka kizuizini isivyo halali ambapo Kwa mara ya kwanza, washtakiwa hao walipandishwa kizimbani mahakamani hapo, Desemba 6, 2024 na kusomewa shtaka hilo.

TUNALAANI WOTE WANAOHAMASISHA MAANDAMANO- MALAIGWANAN K'NJARO

10/21/2025 04:27:00 pm

 _Waahidi kuwachagua walinda amani na mshikamano wa Taifa_ 

Viongozi wa Jamii ya Kimasai nchini Tanzania maarufu kama (Malaigwanan) wametoa tamko lao rasmi kwa nchi nzima, la kuunga Mkono kufanyika kwa uchaguzi Mkuu wa Tanzania wa Oktoba 29, 2025, wakilaani uwepo wa hamasa ya kufanyika kwa maandamano siku hiyo wakiwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kupiga kura kuchagua Viongozi wanaowataka.

Viongozi hao wametoa tamko hilo katika eneo la Donyomorwak Wilayani Siha Mkoani Kilimanjaro kwenye Mkutano wao wa kawaida wa Orkiama ambapo akisoma tamko hilo kwaniaba ya Viongozi hao, Bw. Jeremia Laizer, Katibu wa Malaigwanani Tanzania, ameeleza pia kwamba Jamii hiyo itamuunga Mkono Kiongozi mwenye kutanguliza mbele maslahi ya wananchi pamoja na kulinda amani na utulivu wa Tanzania.

"Tunawahimiza wananchi wote kudumisha amani, mshikamano na utulivu, kuanzia ngazi ya shina, kijiji, kata, tarafa, wilaya, mkoa, kanda hadi Taifa zima, tukiepuka maneno ya uchochezi, migawanyiko, na fitina. Tuchague maendeleo, umoja, na mustakabali mwema wa vizazi vya sasa na vijavyo. Tuwe nguzo ya amani, nuru ya matumaini, na urithi wa thamani kwa Taifa letu. Tanzania kwanza, amani kwanza." Amesema Bwana Laizer.

Kwa upande wake mgeni rasmi wa Mkutano huo ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Namelok Sokoine amewapongeza malaigwanani hao kwa msimamo wao huo pamoja na kuonesha kuridhika na utendaji wa serikali ya awamu ya sita, akiwataka kujitokeza kwa wingi kupiga kura ifikapo Jumatano ya Oktoba 29, 2025.

Aidha baadhi ya Viongozi wengine wa jamii hiyo pia wameahidi kuwa mabalozi wa kueneza amani katika maeneo yao katika kipindi hiki cha uchaguzi Mkuu, wakisisitiza athari za maandamano yasiyofuata taratibu kuwa ni pamoja na uharibifu na uvunjifu wa amani ambapo waathirika wakubwa mara zote wamekuwa wanawake, watoto pamoja na wazee.

Hakuna Maendeleo Bila Amani, Hakuna Taifa Imara Bila Mshikamano - Dkt. Judith

10/21/2025 04:26:00 pm


Wakati Tanzania ikielekea kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwanamke na Nguvu ya Kijani, Dkt. Judith Mhina Spendi, ametoa wito kwa Watanzania wote kusimama pamoja kulinda amani ya taifa. Akizungumza jijini Dar es Salaam, Dkt. Judith alitangaza kongamano la amani litakalofanyika kuanzia Oktoba 25 hadi 27 katika Viwanja vya Posta Kijitonyama, likiwakutanisha viongozi wa dini, vijana, wafanyabiashara na taasisi mbalimbali.
Dkt. Judith alisisitiza kuwa amani ndiyo msingi wa maendeleo, ikieleza kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa kiuchumi kutokana na utulivu uliopo. “Hakuna maendeleo bila amani, hakuna uchaguzi huru bila utulivu, na hakuna taifa imara bila mshikamano,” alisema. Akihitimisha hotuba yake, alitoa wito kwa Watanzania wote kuwa sauti ya amani, umoja na ukweli.

“Mimi naahidi amani, wewe je?” — Dkt. Judith Mhina Spendi

Viongozi wa Dini Mkoa wa Katavi waahidi Mshikamano uchaguzi mkuu 29 Oktoba

10/21/2025 04:26:00 pm

Viongozi wa dini Mkoa wa Katavi wamefanya Kikao maalumu kujadili kuhusu amani na Mshikamano wa Watanzania, wakihamasisha wananchi kuendelea kutunza na kudumisha amani hasa katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi mkuu Oktoba 29, 2025.
Viongozi hao Kwa pamoja wamesema kila Mtanzania anayo nafasi ya kuilinda tunu ya amani tukiyoachiwa na baba wa Taifa Mwl. Julius Kambarage Nyerere na uchaguzi usiwe sehemu ya kuleta mgawanyiko na kuvuruga amani kwani kukosekana kwa amani kwenye Jamii kunachangia Kwa kiasi kikubwa kurudisha nyuma maendeleo ya Tanzania.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na kamati ya amani ambaye pia ni Shekhe wa Mkoa waka Katavi Sheikh Mashaka Nassor Kakulukulu amesema katika kipindi hiki watanzania wanatakiwa kuungana na kuzika tofauti za udini ukabila na nyinginezo ili kuvuka salama katika kipindi cha uchaguzi na amani ndio nguzo ya maendeleo kwani hakuna maendeleo pasipo amani.

Saturday, 18 October 2025

WOTE WENYE HOMA ZA UCHAGUZI MSIKUBALI ZIKAPANDA KICHWANI, TUTAWADHIBITI- KANALI MTAMBI

10/18/2025 01:35:00 pm

Mkuu wa Mkoa wa Mara Kanali Evans Mtambi amewaonya wale wote watakaojaribu kuhamasisha ama kuleta uvunjifu wa amani wakati wa mchakato wa uchaguzi Mkuu hapo Oktoba 29, 2025 akitahadharisha wale wote wanaotaka kupandisha homa ya uchaguzi kutojaribu kufanya hivyo kwani watashughulikiwa ipasavyo kwa mujibu wa sheria za nchi.

Kanali Mtambi ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Oktoba 17, 2025 katika ukumbi wa Mwembeni Complex katika ufunguzi wa Mafunzo ya walimu kutoka mikoa minane ya Kanda ya ziwa na Kanda ya Magharibi, mafunzo yanayofanyika Mkoani humo, akiwahakikishia waalimu hao na wananchi wa Mkoa huo kuwa wamejipanga kikamilifu ,kuhakikisha kila mmoja anatumia haki yake ya kuchagua Kiongozi amtakaye katika mazingira tulivu na yenye amani na usalama wa kutosha.

"Huu ni mwaka wa uchaguzi na mwezi huu ndiyo hasa tumefika kunako sasa shughuli za kisiasa zimekuwa zikiendelea vizuri katika Mkoa wetu, Vyama vyote vimepata fursa sawa, Wagombea wamepata muda mzuri wa kunadi sera zao, Wananchi wamekuwa wakijitokeza kwa wingi kusikiliza Wagombea kupitia Vyama mbalimbali, demokrasia Mkoa wa Mara imekua na inaendelea kupevuka."

"Naomba pia nitumie fursa hii kama Mwenyekiti wa Kamati ya usalama Mkoa, niwatanabaishe wale ambao wakati wa uchaguzi homa ya uchaguzi inapopanda inakimbilia kichwani na kuleta mfetuko wa vichwa, sasa vichwa vikifetuka wengine hufanya mambo yasiyokubalika, nitumie fursa hii kutoa onyo kwao, homa ya uchaguzi ikikupanda tafakari vizuri sera na itkadi ya Chama chako, usiniletee fujo katika Mkoa wa Mara na kama utajaribu utakutana na moto mkali kweli kweli na hapa sipepesi macho, hatutamvumilia yeyote atakayechafua hali ya hewa kwasababu tu amepata homa ya uchaguzi akaamua kujifanya kuwa kichaa, naomba asiwepo yeyote mwenye wazo la namna hiyo." Amesema Mhe. Mtambi.

Mtambi Alisema Mkoa wa mara Vyama vyote katika Mkoa huo vinaendelea kufanya kampeni zake za Amani na Utulivu suala linalotoa fursa ya ushiriki wa wananchi kwenye mikutano ya Kampeni kwa Vyama mbalimbali vya siasa katika Mkoa huo.

VIONGOZI WA KIMASAI WAAHIRISHA TOHARA KWA VIJANA 2, 000 KUPISHA UCHAGUZI MKUU*

10/18/2025 01:35:00 pm


Laigwanani Mkuu wa Jamii ya Kimasai nchini TanzBania Bwana Isack Ole Kisongo Meijo ametangaza kusogezwa mbele kwa zoezi la tohara kwa Vijana wa kimasai lililokuwa lifanyike kuanzia Oktoba 21-30 mwaka huu ili kutoa fursa kwa Vijana zaidi ya 2, 000 waliokuwa washiriki kwenye zoezi hilo kwenda kushiriki kupiga kura Oktoba 29, 2025.

Ole Kisongo ametoa maelezo hayo leo oktoba 17, 2025 mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla wakati wa Baraza la Maigwanani Mkoa wa Arusha, akimuhakikishia Mkuu wa Mkoa kuwa wapo tayari kwa uchaguzi na kulinda kulinda amani wakati wote wa uchaguzi Mkuu kwenye jamii yao.

"Hiyo siku ni takatifu katika Taifa la Tanzania, Hiyo siku ni njema na tumeambiana jamii ya kimasai kuwa hatujawahi kushika mkia, tunataka kujitokeza kwa wingi kupiga kura katika Vijiji vyetu sasa Ukitahiri Vijana 1,000 leo utapunguza kura kwani Mgonjwa atashindwa kwenda kupiga kura. Tunataka kushiriki vyema kupiga kura sote." Amesisitiza Ole Kisongo.
Kwa upande wake Mhe. Makalla katika salamu zake amewapongeza na kuwashukuru Viongozi na Jamii nzima ya Kimasai kwa kutambua umuhimu wa amani na kuridhika na kazi nzuri ya kimaendeleo inayoendelea kutendwa na serikali ya awamu ya sita, akiwahamasisha kuwa mabalozi wazuri wa kuhamasisha wengine kujitokeza kupiga kura na kulinda amani ya nchi.

CPA Makalla pia amewataka wananchi mara baada ya kupiga kura kurejea majumbani mwao na kuachia mamlaka husika kuendelea na zoezi la usimamizi na ulinzi wa kura, akiwahakikishia kuwa Vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga kikamilifu kuhakikisha Mkoa unakuwa salama na tulivu kuanzia sasa, wakati wa kura na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.

Friday, 17 October 2025

TUME YA UCHAGUZI YAWATAHADHARISHA WANAOSHAWISHI KUTOPIGA KURA “NI KOSA KISHERIA’

10/17/2025 10:55:00 pm

Mkurugenzi wa Uchaguzi kutoka Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Ramadhan Kailima, amewatahadharisha wananchi na wadau wa siasa nchini kuwa kuhamasisha watu kutoshiriki kupiga kura ni kosa la kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2024.

Akizungumza katika mahojiano maalum na kituo cha televisheni cha UTV, Kailima amesema kifungu cha 129 cha sheria hiyo kinaeleza wazi kuwa mtu yeyote anayetumia nguvu, vitisho, au udanganyifu kumshawishi mpiga kura kuacha kupiga kura anatenda kosa la ushawishi mbaya, na anaweza kuchukuliwa hatua za kisheria.

Amefafanua kuwa kifungu hicho kinakataza mtu yeyote kutumia au kutishia kutumia nguvu, vurugu, au hila ya aina yoyote kwa lengo la kumshawishi mpiga kura kupiga au kuacha kupiga kura, akisisitiza kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa kwa watakaobainika kuvunja masharti hayo.

KAMANDA MULIRO "TUMEJIPANGA OKTOBA 29" | AWATOA HOFU WANANCHI "TIMIZENI WAJIBU WENU KIKATIBA"*

10/17/2025 10:55:00 pm
Na mwandishi wetu

Jeshi la Polisi nchini limesema litaendelea kufuatilia kwa kina, kuzuia, kubaini na kutanzua matishio ya Usalama siku ya Oktoba 29, .

Pia limetoa rai kwa Wananchi kujitokeza kushiriki ili kutimiza haki na wajibu wao wa Kikatiba bila ya kuwa na hofu yoyote.

Kauli hiyo imetolewa Jijini Dar es Salaam leo Oktoba 15, 2025 na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam Jumanne Muliro.

Wakazi wa Pwani wadai kusubiri uchaguzi mkuu 29 Oktoba kwa shauku kubwa"tutatoka na watoto wetu kupiga kura

10/17/2025 10:55:00 pm
TUNAAMINI UCHAGUZI UTAKUWA WA AMANI NA USALAMA UTAKUWEPO- WANANCHI WA KIBAHA

Wananchi wa Kibaha Mkoani Pwani wamesema wana uhakika kuwa uchaguzi Mkuu wa mwaka huu utakuwa wa amani na haki kwa kila mmoja anayeshiriki uchaguzi huo, wakiamini kuwa siku ya Oktoba 29, 2025 kutakuwa na amani na utulivu pia kutokana na uthibitisho na uhakika walioupata kwa Rais Samia Suluhu Hassan aliyesema kuwa serikali na Vyombo vya Dola vimejipanga kikamilifu kuhakikisha kila mwananchi anapata fursa ya kupiga kura katika mazingira salama na tulivu kote nchini.

Wananchi hao akiwemo Bi. Mwinyimvua Kasosoma na Mwanaidi Stephano, wakazi wa Kwa Mathias, Kibaha Mkoani Pwani wamesema hayo leo Oktoba 15, 2025 wakati wakizungumza na mwandishi wetu na kusisitiza kuwa wao na familia zao watajitokeza wote wenye sifa kwenda kupiga kura na kumchagua Kiongozi wanayeamini atawaletea maendeleo.

Aidha wamekumbusha umuhimu wa kuheshimu sheria na Miongozo yote ya Uchaguzi Mkuu, wakisema mara baada ya Kupiga kura ni muhimu kila mmoja kuondoka kwenye Vituo vya kupigia kura na kwenda kuendelea na shughuli nyingine za kiuchumi, wakijitenga na baadhi ya maneno ya wanasiasa wanaowataka wafuasi wao kusalia vituoni ili kuhakikisha ulinzi wa kura ama kuachana na upigaji wa kura na kuandamana ili kuitika hamasa ya baadhi ya wanaharakati na wanasiasa.

Uchaguzi Mkuu wa Tanzania wa kuwachagua Madiwani, Wabunge na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unafanyika Oktoba 29, 2025 ambapo Rais wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya ulinzi na usalama Dkt. Samia Suluhu Hassan tayari amewahakikishia wananchi wote usalama na utulivu wa kutosha siku hiyo, akionya wale wote wanaopanga kufanya vitendo vya uhalifu ama uvunjifu wa amani nchini.

RC MAKALLA AWAHAKIKISHIA USALAMA WAZEE WA MKOA WA ARUSHA SIKU YA UPIGAJI KURA OKTOBA 29.

10/17/2025 10:55:00 pm
Na mwandishi wetu , Arusha

Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla amewahakikishia wazee na wananchi wa Mkoa wa Arusha kuwa wamejipanga Vyema kuhakikisha siku ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 kutakuwa na amani na mazingira tulivu ya upigaji kura, akitoa wito kwa kila Mwananchi mwenye sifa kujitokeza kwa wingi kuchagua Viongozi wanaowataka ili kuwaongoza kwa miaka mitano ijayo.
CPA Makalla ametoa wito huo wakati wa matembezi ya amani ya Wazee wa Mkoa wa Arusha, waliofanya matembezi hayo Jijini Arusha kwaajili ya kuliombea Taifa amani kama sehemu ya kumuenzi Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Wakianzia matembezi hayo kwenye Viunga vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, kwenda Mnara wa saa, Metropole, Idara ya maji, kituo cha Mabasi Arusha na baadaye kumalizia tukio lao kwenye Viwanja vya Makumbusho Jijini Arusha.

"Kupiga kura ni haki ya Kikatiba ya kila Mtanzania. Wazee wangu mtukumbushe na kuwakumbusha Vijana kuitunza amani, kutumia vyema mitandao ya kijamii lakini Vijana wenye sifa za kupiga kura wajitokeze kwa wingi. Niwahakikishie mtapiga kura kwa amani na atakayeshinda atangazwe kushinda." Amesema.

Makalla amewahakikishia wananchi wote amani na usalama katika kipindi hiki cha lala salama za Kampeni, wakati wa upigaji kura na hata baada ya kura, akisema amani ni muhimu kwa maendeleo pamoja na ukuaji wa sekta ya utalii katika Mkoa huo ulio kitovu cha utalii kwa upande wa Tanzania bara.

Kwa upande wao baadhi ya wazee walioshiriki matembezi hayo kwaniaba ya wenzao wamewasihi wananchi wa Mkoa huo kujitokeza kwa wingi kupiga kura na kuhimiza kila mmoja kulinda amani ya Mkoa wa Arusha, wakisema amani imekuwa tunu muhimu ya maendeleo na ustawi wa watu wa Mkoa wa Arusha.

Wednesday, 15 October 2025

AFANDE SELE AWATAKA VIJANA KUACHA MIHEMKO NA KUTISHIA KUSUSIA UCHAGUZI MKUU OKTOBA MWAKA HUU

10/15/2025 08:22:00 pm
Mwanamuziki na mfalme wa mashairi Tanzania, Selemani Msindi maarufu kama Afande Sele,amewataka Watanzania hususan vijana kuacha kuwa na mihemko ya kususia kushiriki Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025.

 Aidha Afande Sele amesisitiza kuwa kutoshiriki ni kujinyima haki ya kikatiba jambo ambalo sio sahihi katika kulijenga Taifa la baadae.

 Akizungumza akiwa mkoani Morogoro, Afande Sele amesema vijana wanapaswa kutumia nguvu yao kwa kushiriki katika kupiga kura badala ya kujiingiza kwenye maandamano yanayoandaliwa na watu wasiolitakia mema taifa.

MUFTI ATAKA WAISLAMU KUZINGATIA MAFUNDISHO YA AMANI KUELEKEA UCHAGUZI MKUU OKTOBA 29.

10/15/2025 08:08:00 pm
Na mwandishi wetu. 

Mufti na Sheikh Mkuu wa Sheikh Mkuu wa Tanzania Sheikh Dkt. Abubakar Bin Zubeir Ally amewataka Waislamu na Watanzania kwa ujumla kuendelea kuwa mstari wa mbele katika kulinda amani na ustawi wa jamii hasa wakati huu ambapo Tanzania inaelekea kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025.

Mbele ya waumini wa kiislamu Katika Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma, Mufti Sheikh Abubakar amesema amani ndiyo msingi wa uislamu na chachu ya maendeleo ya jamii yoyote ile, akisisitiza kuwa waislamu wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika kuhakikisha utulivu na mshikamano vinaendelea kuwepo.

"Maandishi yanasema wala msieneze katika nchi uharibu wowote wa kuweza kuleta matatizo. Je uislamu umezungumza amani? Niwaambie kuwa Msaafu mzima tukiufasiri ni amani, amani tupu, Mtume kipindi chote anazungumzia amani. Kipindi hiki tufundishe na tutangaze juu ya amani na mmomonyoko wa maadili." Amesisitiza kusema Mufti huyo.

Mufti pia ameeleza kuhusu umuhimu wa malezi ya watoto katika misingi ya dini, akieleza kuwa hilo ndilo jambo la msingi katika kukabiliana na mmomonyoko wa maadili unaozidi kushika kasi katika jamii, akitoa rai kwa wazazi na walezi kuwalea watoto wao kwa maadili ya dini na kulinda maadili ya Taifa kwa vizazi vijavyo.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Mhe. Denis Masanja amewataka wananchi wote wa Wilaya hiyo wenye sifa na waliojiandikisha kwenye daftari na Mpigakura kujitokeza kwa wingi siku ya uchaguzi wa Oktoba 29, 2025 ili kutimiza haki yao ya Kikatiba ya kupiga kura.

TAASISI ZA KIDINI NA ELIMU WAFANYA MDAHALO KUSISITIZA AMANI NCHINI

10/15/2025 08:08:00 pm
Na mwandishi wetu. Dar es Salaam

Taasisi za kidini na kielimu kwa kushirikiana na Kituo cha Utamaduni cha Ubalozi wa Iran zimefanya mdahalo maalumu Jijini Dar Es Salaam wenye lengo la kusisitiza na kudumisha amani, mshikamano, utulivu na haki kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29 mwaka huu. 

Mdahalo huo umewakutanisha viongozi wa dini, wanazuoni, na wadau wa amani ambapo Kiongozi Mkuu wa Kanisa la Evangelical Fellowship Church Tanzania, Baba Askofu Charles Asher, amesema kuwa ni wajibu wa kila Mtanzania kutumia haki yao ya kikatiba kwa amani katika kuchagua viongozi wanaowataka, huku akisisitiza kuwa Tanzania imeendelea kuwa mfano wa utulivu barani Afrika tangu ilipopata uhuru.

Amesema uchaguzi siyo uwanja wa uhasama, bali ni fursa ya kuimarisha demokrasia na kujenga mustakabali wa taifa. “Kila mmoja wetu ana jukumu la kulinda amani. Tofauti za kisiasa haziwezi kuwa sababu ya kuvuruga umoja tuliojenga kwa miaka mingi,” amenukuliwa akisema Askofu Asher.

Kwa kadri teknolojia inavyozidi kukua na kadri uhuru unavyoongezeka wakati mwingine kumekuwa na hali za taharuki kwasababu ya kutokuwa na mwelekeo mmoja wa watu na sisi kama Viongozi wa dini ni kuileta jamii pamoja na kuwafundisha namna ya kuyapokea yaliyo mema. Tunawajibika pia kuwaweka pamoja na kutunza tunu ya umoja wa Watanzania." Amesema Askofu Asher.

Kwa upande wake Sheikh Mulasar Lulat, miongoni mwa waliohudhuria kongamano hilo ameeleza kuwa kuelekea uchaguzi mkuu ni muhimu kuendelea kudumisha na kuitunza amani na kulinda misingi ya amani nchini, akiwataka Watanzania kujiepusha na vurugu na uchochezi unaofanywa mitandaoni, akiwataka kutokubali kuyumbishwa na watu wasioheshimu na kuilinda misingi ya tunu za amani na mshikamano wa nchi.

Tuesday, 14 October 2025

Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania , Gerson Msigwa atoa kauli kali kwa Watanzania awatoa hofu uchaguzi mkuu.

10/14/2025 10:09:00 am
Na Mwandishi wetu

Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania Bw. Gerson Msigwa amewahakikishia Watanzania wote wenye sifa na waliojiandikisha kwenye daftari na mpiga kura kuwa serikali ya awamu ya sita inatambua kikamilifu wajibu wake wa kulinda haki ya kila Mtanzania ikiwemo haki ya Kikatiba ya Kuchagua na kuchaguliwa, akiwahimiza kujitokeza kwa wingi kupiga kura ifikapo Oktoba 29, 2025.

Msemaji huyo wa serikali amewatoa hofu pia Watanzania dhidi ya yale yanayosemwa mtandaoni kuelekea siku ya uchaguzi Mkuu wa Tanzania, akisema serikali na Vyombo vya Dola vimejipanga na kujiandaa kikamilifu kuhakikisha kuwa uchaguzi unafanyika kwa amani na katika mazingira tulivu na salama ili kutoa fursa ya kila mmoja kuitumia haki yake ya Kikatiba.

"Naomba niwahakikishie Watanzania wote kuwa amani ipo tena ya kutosha kwahiyo msiwe na wasiwasi wowote serikali hii ni makini, Vyombo vyetu vyote vya Dola vimejiandaa kikamilifu kuhakikisha utulivu na amani ya kutosha. Nenda kachague Kiongozi unayemtaka na hakuna mtu yoyote atakayefanya chochote. Achaneni na maneno yanayotengenezwa mtandaoni kuwatishia watu na kuwaaminisha vitu ambavyo havitatokea." Amesema Msigwa.

Aidha Msigwa pia amehimiza watanzania kuendelea kujiandaa na upigaji huo wa kura kwa kusikiliza mikutano ya Kampeni ya Wagombea Udiwani, Ubunge na Urais wa Tanzania ili kuwa na maamuzi sahihi ya kuchagua Kiongozi anayefaa badala ya kusubiri kuchaguliwa Kiongozi wa eneo lako na watu wengine.

Tazama Wakazi wa Mapinga waonesha hisia zao uchaguzi mkuu

10/14/2025 10:09:00 am
Na mwandishi wetu, Pwani

Wananchi wa Mapinga Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani wamehamasika kujitokeza kwa wingi kwenda kupiga kura kwenye uchaguzi Mkuu wa Tanzania unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025, wakihamasisha watanzania wote waliojiandikisha kwenye daftari la Mpigakura, kutumia haki yao ya Kikatiba kuweza kuchagua Viongozi sahihi watakaowaletea maendeleo.

"Tarehe 29 nitaamka asubuhi na familia yangu yote tutaenda kupiga kura na ninawasihi Watanzania wenzangu tutumie haki yetu ya Kikatiba na tujitokeze kwa wingi tukapige kura kuwachagua Viongozi tunaowataka na usipopiga kura utachaguliwa Viongozi usiowataka na matokeo yake ni malalamiko." Amekaririwa akisema Fatuma Mkumba, Mkazi wa Mapinga.

Wananchi hao kwa nyakati tofauti wakizungumza na Chombo hiki cha habari leo Jumatatu Oktoba 13, 2025 wamesisitiza pia umuhimu wa kila mmoja kupiga kura, wakisema Viongozi sahihi wanaochaguliwa na watu ndiyo wenye kuweza kuwaletea maendeleo katika ngazi mbalimbali na zaidi wakihamasisha kuchagua Viongozi kutokana na sera, ahadi na yale yote wanayoendelea kuyaeleza katika Mikutano yao ya Kampeni nchi nzima.

Kwa upande wake Bi. Tukae Rashid, Mkazi wa Mkoa wa Pwani amesisitiza pia umuhimu wa kuheshimu sheria na taratibu za uchaguzi, akiwashauri Wapigakura wengine kurejea majumbani na kwenye sehemu zao za kazi mara baada ya kumaliza kupiga kura badala ya kujiingiza kwenye Uvunjifu wa sheria ikiwemo kusalia Vituoni kulinda kura kama ambavyo baadhi ya wanasiasa na Vyama vya siasa vimekuwa vikishawishi wanachama wake kubakia Vituoni ili kulinda kura walizozipiga.

Tayari Rais wa Awamu ya sita ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya ulinzi na usalama amewahakikishia watanzania wotw utulivu, amani na usalama siku ya upigaji wa kura, akiwahimiza kujitokeza kwa wingi kwenye zoezi hilo la kidemokrasia na kutotishwa na yeyote wakiwemo wale wanaohamasisha kufanya vurugu na maandamano wakati wa Uchaguzi huo.

Monday, 13 October 2025

VIJANA WATAKIWA KUCHAGUA VIONGOZI WANAOWEZA KUTIMIZA MATARAJIO YAO

10/13/2025 01:13:00 pm
Na mwandishi wetu

Katibu Mkuu kutoka  Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Kazi, Vijana, Ajira na watu Wenye Ulemavu, Bi. Mary Maganga, amewataka vijana kote nchini Tanzania kutumia haki yao ya Kikatiba ya kupiga kura kwa kuchagua viongozi wanaoakisi matumaini, malengo na ndoto za taifa la Tanzania katika kipindi cha mitano ijayo.

Walakati wa ufunguzi wa Kongamano la Vijana Tanzania linalofanyika kwa siku mbili katika ukumbi wa City Park Garden, Jijini Mbeya na kuhudhuriwa na Vijana kutoka maeneo mbalimbali nchini, Maganga amesema vijana wana nafasi kubwa katika mabadiliko ya kijamii na kiuchumi, hivyo ni muhimu wakatumia fursa hiyo kuchagua viongozi wanaolenga ustawi wa taifa.

“Vijana ni nguvu ya mabadiliko na maendeleo katika jamii zetu, Hivyo ni lazima tutumie vyema nguvu hii kubadilisha dunia kuwa mahali bora kwaajili ya watu wote. Hivyo, ninawasihi mjitokeze kwa wingi kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, na kuchagua viongozi wenye dira sahihi kwa taifa letu,” amesema Bi. Maganga.

Katibu Mkuu huyo amesema Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea pia ya kuweka mikakati mbalimbali ya kuwawezesha vijana, ikiwamo mifumo ya kisera, kisheria, Kitaasisi pamoja na uwezeshaji wananchi kiuchumi kupitia utoaji wa Mikopo na usaidizi mwingine unayolenga kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Ameongeza kuwa kongamano hilo ni jukwaa muhimu kwa vijana wa Kitanzania kubadilishana mawazo, kujifunza na kujadili changamoto zinazowakabili, ili serikali iweze kuyatumia maoni yao katika kuboresha sera na miongozo ya vijana nchini.

Awali, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Rodrick Mpogolo, amewataka vijana kuendelea kuwa wazalendo na kujivunia taifa lao, akisema mchango wao ni muhimu katika kulijenga taifa lenye misingi imara ya maendeleo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Vijana, Ofisi ya Waziri Mkuu, Seleman Mvunye, amesema kongamano hilo limewakutanisha zaidi ya vijana 1,500 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, likiwa na lengo la kuwajengea uwezo wa kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi.

Sunday, 12 October 2025

Watu wenye ulemavu wapaza sauti zao tusishawishike na kurubuniwa kuchagua viongozi wa shinikizo la kupewa chochote.

10/12/2025 07:07:00 pm
Na mwandishi wetu ,Morogoro.

Kuelekea uchaguzi Mkuu wa Jumatano ya Oktoba 29, 2025 wa kuwachagua Madiwani, Wabunge na Rais wa Tanzania, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Morogoro imetoa rai kwa watu wenye ulemavu  kujitokeza kwa wingi kutimiza haki yao ya kikatiba ya kuwachagua viongozi wanaoweza kuwaletea maendeleo na kutetea maslahi ya kundi hilo.

Naibu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Morogoro Bw. Christopher Mwakajinga ametoa rai hiyo wakati akifungua mafunzo ya utoaji elimu ya kuwajengea uelewa juu ya masuala ya rushwa yenye kauli mbiu: ‘Kataa Rushwa katika Uchaguzi“ kwa viongozi wa vyama vya watu wenye ulemavu na mahitaji maalum mkoani Morogoro.

Mwakajinga amesema ushiriki wa makundi ya watu wenye mahitaji maalum katika uchaguzi si hisani bali ni haki yao ya msingi inayotokana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo wanapaswa kushiriki uchaguzi mkuu kikamilifu bila kuwa na vikwazo vyovyote.

Amesema katiba yetu inatoa fursa kwa watanzania wote ambao wametimiza miaka 18 kuwa na haki ya kushiriki kwenye uongozi wa nchi na imetolewa bila kujali ulemavu wa mtu ,vipato vyao, ,hivyo wanapaswa kuitumia sawa na watanzania wengine wasio na ulemavu.

“ Ni lazima tuwekeane mazingira huru na sawa ili muweze kulitumia zoezi hili la msingi la haki ya kupinga kura,“amesema Mwakajinga .

Nao baadhi ya viongozi wa vyama vya watu wenye ulemavu kwa nyakati tofauti wamewasihi wenzao wasishawishike na kurubuniwa kuchagua viongozi wa shinikizo la kupewa chochote, bali watumie haki yao kuchagua viongozi wanaowataka ili wawaletee maendeleo yao na Taifa na watakaodumisha amani ya Tanzania.

MAELFU YA WANANCHI WA MKURANGA "TUPO TAYARI KUSHIRIKI UCHAGUZI MKUU KWA AMANI"

10/12/2025 04:24:00 pm
PWANI

Wananchi wa Mkuranga Mkoani Pwani wamesema wapo tayari kwa ushiriki wa uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 wakiwahimiza pia Vijana kutumia fursa hiyo na haki ya kikatiba ili kuchagua Viongozi wanaoweza kuwaletea maendeleo kwa miaka mitano ijayo.
Wananchi hao akiwemo Mzee Maulid Mwigange na Mariam Ngayonga wakati wakizungumza na Vyombo vya habari, wamewatoa wasiwasi pia wananchi na kwa kuwaeleza kuwa Oktoba 29, 2025 kutakuwa na usalama na amani ya kutosha kutokana na namna ambavyo serikali imejipanga kuhakikisha kuwa kila mwananchi anapata nafasi kamili na usalama wa kushiriki kupiga kura.

"Tutachagua Kiongozi anayetufaa na tumehamasika kushiriki kwasababu ya maendeleo mengi tu tunayoyashuhudia Mkuranga ikiwemo stendi nzuri na hatubugudhiwi." Ameongeza kusema Mohamed Makame, mwananchi na mfanyabiashara mdogo wa Mkuranga.

Kwa upande wake Habiba Jasmin, Kijana na mjasiriamali mdogo wa Mkuranga ametoa wito wa Vijana kutumia vyema fursa ya upigaji kura kuamua kuhusu hatma yao ya miaka mitano ijayo, akiombea kheri uchaguzi huo ili ufanyike na umalizike kwa amani ili waweze kuendelea na shughuli zao za kila siku za uchumi.

BAKWATA MWANZA WAELEKEZA WAUMINI WAKE KUANZA MFUNGO KUOMBEA AMANI YA TANZANIA

10/12/2025 04:11:00 pm
Mwanza

Baraza la Waislamu wa Tanzania (BAKWATA) Mkoa wa Mwanza limewaelekeza waumini wake wa kufunga kwa maombi kuanzia Alhamisi ya Oktoba 23, 2025 hadi siku yatakapotangazwa matokeo ya uchaguzi Mkuu wa Tanzania wa Oktoba 29, 2025 na Tume huru ya Taifa ya uchaguzi.


Akizungumza wakati wa Kikao cha Baraza hilo Mkoa wa Mwanza Sheikh wa Mkoa huo wa Mwanza Hassan Kabeke amesema hatua hiyo inalenga kuiombea nchi amani na mshikamano, akisisitiza kuwa ni wajibu wa Kila Mtanzania kushiriki katika kuilinda amani hiyo ambayo imekuwa msingi wa maendeleo binafsi na ya Tanzania.

"Tarehe 23 Vituo vyetu vyote na misikiti yetu watafunga mpaka siku yatakapotangazwa matokeo. Ni maelekezo tumeyatoa. Hakuna kitu kigumu kama kukubali njaa lakini tutafunga kwaajili ya nchi hii kwani tunao wajibu wa kupigania amani ya nchi hii hasa kwa kurejea historia ya baadhi ya wazee wetu na wazee wa imani nyingine wameshiriki kuutafuta uhuru wa nchi hii." Amesema Sheikh Hassan Kabeke.

Kiongozi huyo pia wa imani amehimiza wananchi kujitokeza kwa wingi kupiga kura kwenye uchaguzi Mkuu ujao, akitaka Oktoba 29, 2025 kuwa siku ya Vikao vya familia ili kukumbushana umuhimu wa kupiga kura sambamba na masuala mengine ya kijamii na kuachana na baadhi ya hamasa za maandamano na ulinzi wa kura vituoni unaotolewa na baadhi ya wanasiasa kwenye Mitandao ya kijamii.

Katika hatua nyingine Kiongozi huyo wa dini amemtaja Dkt. Samia kama kiongozi hodari na aliyepokea nchi katika wakati ambao nchi iliandamwa na msiba na matatizo kadhaa ya kiuchumi, akiachiwa pia miradi mingi michanga iliyohitaji kuendelezwa, miradi ambayo sasa imekamilika na Taifa limeendelea kusalia tulivu, lenye amani pamoja na mshikamano.

Friday, 10 October 2025

MUFTI ABUBAKAR ATOA KAULI NZITO KWA WATANZANIA "TULINDE AMANI"

10/10/2025 06:22:00 pm
Na Mwandishi wetu, Njombe

Waumini wa dini ya Kiislamu na Watanzania kwa ujumla wamehamasisha kujitokeza kwa wingi hapo Jumatano ya Oktoba 29, 2025 ili kupiga kura na kuwachagua Viongozi sahihi wanaoweza kuwaletea maendeleo sambamba na wote kuwajibika kuitunza amani ya Tanzania.

Wito huo umetolewa na Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania Sheikh Abubakar Zubeir Ali Mbwawa wakati wa Mkutano maalumu wa viongozi na waumini wa dini ya Kiislamu Mkoani Njombe, Mkutano uliofanyika Masjid Taqwa, Mwembetongwa Mjini Makambako, akisema amani ndiyo nguzo muhimu ya maendeleo na ustawi wa Taifa, akiwataka waumini wa dini hiyo kuwa mfano wa kuigwa katika kudumisha utulivu na mshikamano.

"Niwakumbushe kuwa Mtume wetu ni mtume wa amani, ni Mtume wa Kheri, Mtume wa baraka na ameitangaza amani amani hiyo kama alivyoitangaza Mungu. Niwakumbushe Vijana amani ndiyo jambo kubwa kuliko yote asije mtu hapa akawadanganya kwaajili ya kuondosha amani halafu wewe ukakubali. Muislamu kila jambo ukiambiwa fikiria ujue linafaa au halifai. Lindeni amani. Chungeni amani na kila mkipata hadhara simamemi semeni na hubirini kuhusu amani." Amesisitiza Mufti Abubakar.

JESHI LA POLISI NCHINI KUWASHUGHULIKIA, WANAOTUMIA MITANDAO YA KIJAMII KUHAMASISHA CHUKI.

10/10/2025 01:01:00 pm
Na Mwandishi wetu.

Jeshi la Polisi nchini Tanzania kupitia msemaji wake DCP David Misime limesisitiza kuhusu matumizi sahihi ya mitandao ya Kijamii pamoja na ulinzi wa amani katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi Mkuu wa Tanzania, akibainisha kuwa Jeshi hilo limejipanga kikamilifu kushughulika kikamilifu na wote watakaohatarisha amani ya nchi.

Msemaji huyo pia ameonya kuhusu wanaotumia mitandao vibaya kuhamasisha chuki, uhasama na kusambaza taarifa za kuzusha, akisema sheria inatoa adhabu pia kwa mtumiaji wa mitandao ya kijamii atakayesambaza (kushare) taarifa ambazo hazina ukweli ama ambazo zine lengo la kuzua taharuki na uhasama.

"Mitandao ya kijamii tukiitumia vibaya inaweza kutufikisha pabaya ikiwemo kutumika kama silaha kuleta uhasama, uzushi na kusambaza uongo kama ambao tunauona kwenye mitandao na nitoe wito kwa jamii unaposambaza taarifa ambazo sio sahihi ni kosa pia kwako unayesambaza taarifa potofu." Amesema Kamanda Misime.

Akizungumza na chombo kimoja cha habari leo Oktoba 10, 2025, Misime pia ameeleza kuwa wamejipanga vyema kulinda raia na mali zao siku ya uchaguzi na baada ya uchaguzi Mkuu, akiwapongeza watanzania kwa kuendelea kuelimika na kukuza ustaarabu wao wakati wote wa kampeni, akiomba ushirikiano zaidi wa kufichua uhalifu na wahalifu kuelekea kwenye uchaguzi mkuu wa Tanzania.

Amewatoa hofu pia Watanzania kuhusu yanayoendelea mitandaoni, akisema nchi ni salama na hakuna tatizo lenye kutishia usalama na utulivu siku ya upigaji wa kura, akisema Jeshi la polisi linaendelea kuchukua hatua kwa wanaotumia mitandao hiyo vibaya na kuishukuru serikali kwa uwezeshaji wake mkubwa wa vifaa na vitendea kazi katika udhibiti wa uhalifu na wahalifu.

Amesema Jeshi hilo pia limesambaza Askari polisi zaidi ya 3,900 kwenye Kata zote za Tanzania bara pamoja na Askari 388 kwenye Shehia za Zanzibar wakitoa elimu kwa jamii kuhusu matumizi sahihi ya mitandao na kuwataka wazazi kuelimisha pia Vijana wao dhidi ya matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii na kuheshimu sheria za Tanzania.

KATIBU MKUU MKOMI,AWAHIMIZA WATUMISHI WA UMMA NCHINI KUJITOKEZA KUPIGA KURA OKTOBA 29

10/10/2025 12:55:00 pm
Na mwandishi wetu

Katibu Mkuu Ofsi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Juma Mkomi, amewahamasisha watumishi wa umma kote nchini kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, mwaka huu.

Akizungumza katika kikao cha tatu cha Baraza la Nane la Wafanyakazi kilichofanyika jijini Dodoma kwa siku mbili, Mkomi alisema licha ya kutokuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa, ana mapenzi na ustawi wa taifa, hivyo ni muhimu kwa kila Mtanzania mwenye sifa ya kupiga kura, hasa watumishi wa umma, kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika mchakato huo wa kidemokrasia.

"Nawaomba wenzangu watumishi wa umma tujitokeze kwa wingi siku ya Oktoba 29 kwenda kupiga kura huu ni wajibu wetu wa kikatiba na njia ya kushiriki moja kwa moja katika maamuzi ya nchi yetu," alisema Mkomi.

Aidha, alibainisha kuwa hata viongozi wa kisiasa wamekuwa wakihamasisha familia zao kujitokeza kupiga kura, hivyo ni vyema pia kwa wafanyakazi wa umma kuwa mstari wa mbele katika kushiriki kwa amani na utulivu.

 "Niwaombe wajumbe wa baraza hili na watumishi wote, tusiwe nyuma. Tuwe mfano wa kuigwa katika kujenga demokrasia kwa kushiriki uchaguzi," alisisitiza.

Kauli hiyo imekuja wakati nchi ikijiandaa kwa uchaguzi ambao unatarajiwa kushirikisha wananchi katika kuchagua viongozi watakaowakilisha maeneo yao, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha utawala bora na ushirikishwaji wa wananchi katika masuala ya maendeleo.

Mwisho.
Adbox