Adbox

Monday, 22 December 2025

POLISI YAJIIMARISHA KULINDA RAIA MSIMU HUU WA KRISMASI NA MWAKA MPYA

12/22/2025 07:43:00 pm

Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, (DCP) David Misime, amesema Jeshi hilo kwa kushirikiana na Vyombo vingine vya ulinzi na usalama vitaendelea kuimarisha ulinzi na usalama wakati na baada ya sikukuu za Krismasi na Mwaka mpya, wito ukitolewa kwa kila mwananchi kutambua na kuheshimu thamani na umuhimu wa amani na usalama kwa kila mmoja.

Taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Disemba 22, 2025 na Jeshi la polisi imewataka pia wale wote watakaokuwa wakisafiri kutoka eneo moja kwenda jingine kuzingatia sheria za usalama barabarani kama sehemu ya kuepuka ajali za barabarani, wakikumbusha kuhusu kaulimbiu ya wiki ya nenda kwa usalama isemayo "endesha salama, familia inakusubiri."

"Maisha yetu na shughuli zetu wakati wa hizi sikukuu yanahitaji mazingira ya amani ili kila mmoha aweze kushiriki kwenye ibada za kumshukuru Mungu, kukaa na familia na marafiki bila ya bugudha yeyote ile hivyo tuilinde amani kwa ushirikiano na kwa nguvu zetu zote." Imesema taarifa hiyo.

"Aidha wito unatolewa kwa wananchi wote na kwa wote watakaokuwa nchini kuwa kinachohitajika ni kila mmoja wetu kutambua thamani na umuhimu wa amani na usalama, ni wakati muafaka pia kuendelea kuyakataa yale ambayo yana malengo ya kuvuruga amani kipindi hiki cha sikukuu na baada." Imeongeza kusema taarifa hiyo ya polisi.

Polisi pia imeeleza kuwa hali ya usalama nchini ni shwari licha ya matukio machache ya uvunjifu wa amani yaliyojitokeza, likisema hali hiyo imetokana na Watanzania kufahamu umuhimu wa kila mmoja kulinda na kuimarisha amani, utulivu na usalama kama nyenzo kuu ya kuwawezesha kushiriki katika shughuli za kijamii na kiuchumi.

Friday, 19 December 2025

KIKAO CHA KAMATI YA WATAALAM YA KITAIFA YA USIMAMIZI WA MAAFA CHAPITISHA MIONGOZO YA KUKABILIANA NA MAAFA NCHINI*

12/19/2025 09:49:00 pm

Na mwandishi wetu, Dodoma.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi ameongoza Kikao cha Kamati ya Wataalam ya Kitaifa ya Usimamizi wa Maafa leo 19 Desemba,2025 kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano uliopo Ofisi ya Waziri Mkuu Ngome, Jijini Dodoma.

Katika kikao hicho, Mpango wa Taifa wa dharura wa  kukabiliana na Ukame, Mafuriko na Majanga mengine yanayohusiana kwa kipindi cha Novemba 2025 hadi Juni 2026 umejadiliwa na kupokelewa na wajumbe wa kikao.

Aidha, Miongozo ya uanzishwaji na Uendeshaji wa kituo cha operesheni na Mawasiliano ya dharura na Timu ya kukabiliana na Dharura ngazi ya Taifa na Mkoa imejadiliwa na kupitishwa na wajumbe wa kikao.

Miongozo iliyojadiliwa na kupitishwa ni pamoja na, Mwongozo wa Uanzishaji wa kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Mwongozo wa Uendeshaji wa kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Ngazi za Mikoa, Mwongozo wa Uanzishaji na Uendeshaji wa Timu ya Mkoa ya kukabiliana na Dharura.

Pia, Muongozo wa Uanzishaji na Uendeshaji wa Timu ya Taifa ya kukabiliana na Dharura, Muongozo wa Uendeshaji wa Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Muongozo wa kuandaa Mpango wa Mkoa wa kujiandaa na kukabiliana na Maafa.

Pamoja na hayo, Wajumbe wa kikao hicho walipokea na kuridhia Mkakati wa Utekelezaji wa Mpango wa Utoaji wa Huduma za Tahadhari ya mapema kwa wote kwa kipindi cha miaka Mitano (2026-2030).

Awali, Dkt Yonaz ametoa Pongezi kwa Taasisi na Sekta mbalimbali zinazokabiliana na Maafa kwa kuendelea kufanya vizuri na kutoa Elimu ya maafa Nchini na Nchi Jirani.

=MWISHO=

Dkt,MWIGULU AKAGUA MAENDELEO YA UJENZI WA MADARAJA LINDI.*

12/19/2025 07:25:00 pm

_Asisitiza Rais Dkt. Samia amedhamiria kushughulika kwa vitendo na umasikini wa watanzania_

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Desemba 19, 2025 amekagua maendeleo ya ujenzi wa Madaraja na Ukarabati wa barabara kuu ya Marendego-Nangurukuru-Lindi-Mingoyo

Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewaambia wakazi wa Somanga mkoani Lindi kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatekeleza miradi ya kimkakati ili kushughulika kwa vitendo na umasikini wa Watanzania

Amesema kuwa Rais Dkt. Samia alisimamia ukamilishaji wa Bwawa la Kuzalisha Umeme la Julius Nyerere ili kuhakikisha kila mtanzania ananufaika na huduma ya nishati ya umeme. 

“Tumeshuhudia Rais Dkt. Samia namna anavyotekeleza miradi kwenye sekta mbalimbali ikiwemo uvuvi, maji, kilimo, afya, elimu na hata uwezeshaji wananchi kiuchumi”

TARURA YAPEWA TUZO KUTAMBUA MCHANGO WAKE KATIKA SEKTA YA UCHUKUZI

12/19/2025 06:46:00 pm

Arusha

Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imepewa tuzo ya  kutambua mchango wake katika maendeleo ya sekta ya uchukuzi nchini. 

Tuzo hiyo imekabidhiwa na Mkuu wa Wilaya ya Arusha Mhe. Joseph Mkude akimwakilisha Waziri wa Uchukuzi na kupokelewa na Mkurugenzi wa Mipango ya Miundombinu, Mhandisi Edward Amboka.

Tuzo hiyo imetolewa katika Mkutano wa 18 wa Tathmini ya Utendaji wa Sekta ya Uchukuzi uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (AICC) jijini Arusha.

TARURA imeshiriki Mkutano huo ikiwa ni mdau wa sekta ya uchukuzi, ambapo ilitumia Mkutano huo kwa kuwasilisha utekelezaji wa shughuli za Wakala kwa mwaka wa fedha 2024/2025 na kutoa elimu kwa wadau kuhusu majukumu na kazi mbalimbali zinazofanywa na Wakala.

Mpango wa Elimu kwa Umma Kuhusu Muungano utakuwa endelevu

12/19/2025 02:06:00 pm
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema Mpango wa Elimu kwa Umma Kuhusu Muungano utakuwa endelevu ili kuhakikisha elimu hiyo inamfikia kila mmoja. 

Ameyasema hayo Desemba 19, 2025 wakati akizungumza katika kipindi cha Asubuhi Njema kinachorushwa na ZBC ambapo amesema Waandishi wa Habari wanayo nafasi kubwa katika utoaji wa elimu kwa umma ndio maana Ofisi ya Makamu wa Rais imewapa nafasi na itakuwa ikishirikiana nao kwa asilimia kubwa.

“Katika kuhakikisha hilo leo tumeandaa Semina ya Wahariri wa Vyombo vya Habari Zanzibar kisha tutaifanya kwa Wahariri Bara na baadaye tutaandaa makongamano mbalimbali.”
 
Amesema Mpango wa Elimu kwa Umma kuhusu Muungano,  wanufaika wakubwa watakuwa vijana ambao ndio walengwa kutokana na wengi wao kuwa wamezaliwa baada ya Muungano(1964).

Tuesday, 16 December 2025

Watanzania naomba tulinde Amani kwa maendeleo yetu Binafsi

12/16/2025 07:27:00 pm

Watanzania wamehfgimizwa kulinda na kuitunza miundombinu inayojengwa katika maeneo mbalimbali nchini ili iweze kudumu na kutumika kwa muda mrefu zaidi na kuwanufaisha zaidi, wakihimizwa pia kulinda amani kwa maslahi ya ustawi na maendeleo binafsi na ya Taifa kwa ujumla.

Wito huo umetolewa na Bi. Fatuma Ramadhan Mchekwa, Mkazi wa Temeke Jijini Dar Es Salaam wakati akizungumza na chombo chetu cha habari leo Jumanne Disemba 16, 2025, akisisitiza kuwa uharibifu wa Miundombinu umekuwa ukiligharimu taifa fedha nyingi.

"Tunachoomba sisi ni amani, amani iendelee na tusifanye fujo kwasababu tunapoharibu miundombinu ikiwemo ya mwendokasi hizi ni kodi zetu wenyewe kwahiyo tunajikomoa wenyewe. Tunafanya biashara  tunalipa ushuru na kodi zetu ndizo zinazoleta maendeleo ila leo badala ya kusema tuendelee kuleta maendeleo tunarudi kukarabati miundombinu iliyoharibiwa." Amesema Bi. Fatuma.

Katika hatua nyingine Bi. Fatuma amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa ujenzi wa miundombinu mbalimbali ikiwemo ujenzi wa barabara ya Mbagala- Kariakoo, ujenzi wa shule ya msingi Kidugulo pamoja na kufikisha umeme kwenye maeneo yote ya Chanika, suala ambalo limeboresha maisha ya wananchi kupitia sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii.L

Wafugaji Chanika waishukuru Serikali ujio wa miradi mikubwa ya ufugaji.

12/16/2025 04:31:00 pm

Wafugaji wa Kata ya Chanika, Wilayani Ilala Mkoani Dar Es Salaam wameishukuru serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa mapinduzi na ujio wa miradi mikubwa ya ufugaji iliyowasaidia kujikwamua na umaskini na kuongeza kipato.

Kwaniaba ya wafugaji hao, Bw. Hamim Idrisa, Katibu wa Wafugaji Kata ya Chanika, ameeleza kuwa ipo miradi mitatu iliyozinduliwa katika Kata ya Chanika katika kipindi cha miaka minne ya awamu ya kwanza ya Rais Samia, ambayo imewaneemesha wafugaji ikiwemo mradi wa kuku wa Mayai na mradi wa kukabiliana na usugu wa madawa ya mifugo.

"Mradi wa kwanza ni ufugaji wa kuku bila dawa ambao umekuwa msaada mkubwa sana kwetu, upo pia mradi wa kukabiliana na usugu wa madawa dhidi ya vimelea vya magonjwa na mradi wa mwisho ni huu wa kuku wa mayai ambapo serikali inatupa nyenzo, madawa na elimu kupitia Maafisa tulionao kwenye Kata yetu." Amesema Bw. Idrisa.

Katika upande wa maendeleo ya Jamii na ustawi, Bw. Idrisa amezungumzia sekta ya afya, akiishukuru serikali kwa ujenzi wa Chumba cha kuhifadhia maiti kwenye Hospitali ya Nguvu Kazi pamoja na kuanza kwa mradi wa Zahanati ya Kidugilo, ambapo fedha na eneo la utekelezaji wa mradi huo imeshapatikana.

Monday, 15 December 2025

Chanika yapaa kimaendeleo miaka minne ya Rais Samia

12/15/2025 10:44:00 pm
CHANIKA WAMSHUKURU RAIS SAMIA KWA UJENZI WA SHULE NA MOCHWARI

CHANIKA YAPAA KIMAENDELEO, MIAKA MINNE YA RAIS SAMIA

Wananchi wa Kata ya Chanika, Ilala Mkoani Dar Es Salaam wamemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa maboresho makubwa ya huduma za afya na elimu Wilayani humo, wakisisitiza umuhimu wa wazazi kuwaandikisha watoto wao katika msimu ujao wa masomo 2026, ili waweze kunufaika na uwekezaji mkubwa uliofanywa ndani ya Wilaya ya Temeke na Tanzania kwa ujumla.

Wananchi hao wameeleza namna ambavyo walilazimika kusafirisha miili ya wapendwa wao wanaofariki kwenda kuhifadhiwa Wilayani Kisarawe kutokana na kukosekana kwa Vyumba vya kuhifadhia maiti katika Kata yao ya Chanika kwenye Hospitali ya Nguvukazi.

Akizungumza na mwandishi wetu wa habari Bi. Jaliah Kabeya, Mkazi wa Chanika Jijini Dar Es Salaam amesema kwasasa katika sekta ya elimu na afya hakuna changamoto yoyote, akishukuru pia kwa ujenzi wa barabara za ndani ya Wilaya yao ikiwemo changamoto ya mafuriko Tazara suala ambalo lilikuwa likikwamisha shughuli za usafiri na usafirishaji ndani ya eneo hilo.

"Tunamshukuru Mungu na Mama Samia kwa hili, tumuombee dua ili aendeleze pale alipobakiza kwasababu yeye si malaika na hawezi kufanya yote kwa wakati mmoja na kwa haya aliyoyafanya pia ni muhimu kuwa na roho shukrani." Amesema Bi. Jaliah.

Mwananchi huyo pia ameshukuru kwa usimamizi wa mikopo ya Asilimia kumi ya Halmashauri inayotolewa kwa wanawake, Vijana na wenye ulemavu, akisema suala hilo limesaidia pakubwa kuwakwamua wananchi na umaskini, akisifu pia michakato yake na mikopo kuwa rahisi.

WAMSHUKURU RAIS SAMIA KWA KUBORESHA HUDUMA ZA KIJAMII NCHINI

12/15/2025 10:37:00 pm


RAIS SAMIA AMETUONDOLEA UKATILI WA KIJINSIA NCHINI- BI. MAPUNDA0

WANAWAKE WAMSHUKURU RAIS SAMIA KWA KUWAENZI NA KUWAPATIA MAHITAJI

Bi. Sikitiko Casian Mapunda, Mkazi wa Nguvu Mpya Jijini Dar Es Salaam amemtaja Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kama Kiongozi na Mama jasiri na shujaa, akimshukuru kwa kuwekeza katika masuala ya Kijamii ikiwemo yanayowahusu wanawake pamoja na watoto.

Bi. Mapunda amebainisha hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Disemba 15, 2025, akisema huko nyuma baadhi ya Makundi yalisahaulika ikiwemo wanawake na Vijana, akisema ni mara ya kwanza kuona Rais akiwaita Vijana na kuwasikiliza kero na changamoto walizonazo.

"Nimshukuru pia sana Mama kwa namna alivyoifanya miundombinu ya GongolaMboto kupitika tofauti kabisa na zamani ilivyokuwa. Sasa hivi barabara ya Gongolamboto ni tofauti kabisa na ilivyokuwa miaka mitano iliyopita, ni kama barabara za Ulaya, tuna Mahospitali na mpaka barabara za ndani nazo zinapitika wakati wote." Amesema Bi. Mapunda.

Amemshukuru Rais Samia pia kuhusu usimamizi wake wa mikopo ya asilimia kumi inayotolewa na Halmashauri kwaajili ya wanawake, Vijana na wenye ulemavu, akimuomba pia kushughulikia masharti magumu ya upatikanaji wa mikopo hiyo.

Katika hatua nyingine Bi Mapunda pia akizungumza na mwandishi wetu wa habari, ameeleza na kushukuru kupungua kwa matukio ya ukatili wa kijinsia nchini ikiwemo matukio ya ubakaji kwa wasichana na wanawake, akisema huko nyuma kabla ya ujio wa Rais Samia udhalilishaji ulikuwa mkubwa na wanawake wengi wa Mijini na Vijijini walikuwa na hofu kubwa ya kupita katika baadhi ya maeneo kwa kuhofia matukio ya ubakaji yaliyokuwepo.

KIKUNDI CHA WAMANDA WAMSHUKURU RAIS SAMIA KWA MAONO YAKE

12/15/2025 12:33:00 pm

Kikundi cha Akinamama wanaonufaika na Mikopo ya asilimia kumi ya Halmashauri cha Wamanda kilichopo Nzega Mkoani Tabora wamemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa usimamizi na maboresho makubwa ya mfumo wa Mikopo hiyo, wakisema imewasaidia kiuchumi na kuwaongezea kipato kwa asilimia kubwa.

Bi. Stellah William, Kwa niaba ya wanakikundi wenzake amesema kupitia kipato wanachokipata sasa kupitia kikundi hicho, ameweza kusomesha watoto, kuendesha maisha pamoja na kumpa ujasiri mkubwa wa kuweza kutafuta fedha na kujiendeleza kiuchumi.

"Kwakweli kikundi hiki kimeninufaisha kwenye kusomesha watoto na wajukuu wangu, naendelea pia kunufaika na mambo mengi sana na zaidi kimenifanya niwe jasiri wa kutafuta fedha nikiwa peke yangu."

Nimpongeze pia Mama Samia kwa kuwa na maono yake ya kuona kuwa hata Kijijini kuna watu wanahitaji msaada wake na nimuombe Mama Samia asituchoke, tunamuhitaji sana na atuangalie kwa macho yake yote sisi akinamama wa Vijijini." Amesisitiza Bi. Stellah William.

Saturday, 13 December 2025

E- MREJESHO KUKUZA UWAJIBIKAJI KWA WATUMISHI WA UMMA

12/13/2025 12:21:00 pm

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema Wizara hiyo imefanya maboresho mbalimbali ya mifumo yake ikiwemo mfumo wa e- mrejesho, ili kutoa fursa zaidi kwa wananchi wa pembezoni kutoa maoni, malalamiko na pongezi kuhusu huduma zinazotolewa na serikali na Taasisi zake.
Mhe. Ridhiwani amebainisha hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar Es Salaam, akisema mfumo huo unapatikana kwenye simu za mkononi kupitia nambari *152*00#, ukiwa na module ya sema na Kiongozi, sehemu inayomruhusu mwananchi kutoa maoni kwa Waziri, Mkuu wa Mkoa ama Kiongozi mwingine, akisema mfumo huo utakusanya maoni na kisha kuchakatwa na kufanyiwa kazi.

"Mfumo huu wa e- mrejesho ni kiunganishi cha moja kwa moja cha mwananchi na Kiongozi na hii itatusaidia pale tunapojadili namna ya kuboresha mifumo ya utumishi wa umma na ni mfumo wa kweli huu, hata kama kuna Kiongozi hatojibu sisi tutasimamia kuhakikisha majibu yanapatikana." Amesema Mhe. Ridhiwani.

Aidha Mhe. Ridhiwani amehimiza wananchi kuutumia mfumo huo katika kutoa maoni yao, akisisitiza kuwa maboresho hayo yanaenda sambamba na utengenezaji wa Aplikesheni itakayowezesha wananchi kutoa mrejesho wa haraka na wa uwazi ili kuimarisha uwajibikaji wa watumishi wa serikali.

POLISI YASISITIZA KILA MMOJA KUWAJIBIKA KULINDA AMANI NCHINI

12/13/2025 07:01:00 am

Jeshi la Polisi nchini Tanzania limetoa wito kwa Kila Mwananchi kuendelea kutii sheria sambamba na kushirikiana na kila mmoja kwa nafasi yake katika kulinda na kuimarisha amani, hasa kwa kuzingatia umuhimu wa amani katika maisha na shughuli za kila siku za kijamii na kiuchumi.

Polisi pia kupitia kwa Msemaji wake David Misime, limesisitiza kuendelea kuelimishana na kuhimizana katika kuyakataa yale yote yanayohamasishwa kwa njia mbalimbali ili kuwachonganisha na kuwajengea chuki Watanzania, lengo likiwa ni kuwaingiza Watanzania katika vurugu ambazo mara zote zimekuwa si nzuri kulingana na kile kinachoshuhudiwa kwenye Mataifa mengine duniani.

"Jeshi la Polisi pia kwa kushirikiana na Vyombo vingine vya ulinzi na usalama vinaendelea kuwaahidi kuwa tutaendelea kulinda usalama wa nchi yetu sote, maisha na mali za kila mmoja ndani ya Taifa letu la Tanzania." Amesema Msemaji huyo wa Jeshi la Polisi Tanzania Naibu Kamishna wa Polisi DCP David Misime.

Katika hatua nyingine, Polisi imeeleza kuwa nchi bado ni salama na shughuli za kiuchumi na za kijamii zinaendelea vyema katika kipindi cha saa 24 zilizopita, likishukuru pia kwa ushirikiano wanaoendelea kuupata kutoka kwa wananchi wa Tanzania.

Thursday, 11 December 2025

MARIDHIANO YATATUPA AMANI YA KUDUMU- WANANCHI

12/11/2025 11:03:00 pm

Watanzania wamehimiza utayari wa Jamii na makundi mbalimbali kushiriki katika mchakato wa maridhiano, wakisisitiza kuwa maridhiano ni silaha muhimu ya utatuzi wa migogoro mbalimbali inayotokea katika jamii kwani maridhiano ndiyo kitovu cha upatanishi kwa Taifa.

Wito huo umetolewa kufuatia kauli zilizotolewa mara kadhaa na Rais Samia Suluhu Hassan, aliyesisitiza kuongoza mchakato wa maridhiano ya Kitaifa ili kuwa na mwelekeo wa pamoja kama Taifa na zaidi katika mchakato wa upatikanaji wa Katiba mpya ya Tanzania.

Baadhi ya wananchi hao akiwemo Bw. Ridhiwan Hamidu Muhimu na Mansour Bakari, wakazi wa Ilala Jijini Dar Es Salaam wamezungumza nasi na kusisitiza kuwa chuki na magomvi si utamaduni wa Watanzania na maridhiano yatamfanya kila mmoja kupata kile anachostahili.

"Maridhiano yatapelekea kila mmoja kupata kile anachokistahili. Bila ya mazungumzo hatutoweza kufikia kwenye hali nzuri, bila ya maridhiano hatutakuwa na amani ya kudumu nchini." Amesisitiza Bw. Ridhiwan.

Bw. Bakari pia amezungumzia kuhusu ghasia za Oktoba 29, 2025 akisema maandamano haramu hayawezi kusaidia katika utatuzi wa changamoto na badala yake huzaa athari nyingi zaidi ambazo zimekuwa zikiwaathiri wananchi wa kawaida badala ya kuleta jawabu kwenye changamoto.

POLISI YAWATAKA WATANZANIA KUJIEPUSHA CHUKI NA UCHONGANISHI

12/11/2025 03:17:00 pm

Jeshi la Polisi nchini Tanzania limewataka Wananchi kuendelea kuwakataa na kuyakataa yale yote yenye mwelekeo wa kichonganishi, uzushi, uongo, yenye kujenga chuki pamoja na yenye kuhamasisha kufanya vurugu na matukio yote yenye viashiria vya kuvunja sheria za nchi.

Taarifa kwa Vyombo vya habari iliyotolewa mapema leo Alhamisi Disemba 11, 2025 na Msemaji wa Jeshi la Polisi, Naibu Kamishna wa Polisi David Misime imesisitiza pia kutosambaza ujumbe wenye kuleta chuki na uchochezi kwa jamii na badala yake kufuta ujumbe wa namna hiyo kwenye Mitandao ya kijamii ikiwemo WhatsApp.

"Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na   usalama vina wahakikishia kuwa vitaendelea kulinda amani na usalama wa nchi pamoja na maisha na mali zenu na tuendelee kutoa wito wa kuzingatia kanuni za kiusalama zinazotakiwa zianze na kila mmoja wetu kwanza sambamba na sisi sote kutii sheria." Imesema taarifa hiyo.

Katika hatua nyingine Polisi imeeleza kuwa kila mmoja aendelee kufanya shughuli zake halali bila hofu kutokana na usalama kuendelea kuimarika kote nchini Tanzania kutokana na ushirikiano mkubwa unaoendelea kutolewa kwa Vyombo vya ulinzi na usalama katika kulinda  na kuimarisha amani, utulivu na usalama nchini Tanzania.

Wednesday, 10 December 2025

RC MAKALLA AWAPONGEZA WANANCHI KWA KUYAKATAA MAANDAMANO YA DISEMBA 09

12/10/2025 04:55:00 pm

 *_Awahamasisha wananchi kujikita kwenye shughuli za kiuchumi_* 

 *_Awataka kujenga utamaduni wa kudumu wa kulinda amani na kuyakataa maandamano_* 

Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla leo Jumatano Disemba 10, 2025, amewapongeza wananchi kwa kuyakataa maandamano ya Disemba 09, 2025, akiwataka kujenga utamaduni wa kudumu wa kukataa maandamano na matukio yote yenye viashiria vya uvunjifu wa amani Mkoani Arusha.

Mhe. Makalla amebainisha hayo wakati wa ziara yake ya kukagua shughuli za kibiashara  kwenye soko la Kilombero Jijini Arusha, akiahidi kuwa serikali na Vyombo vya ulinzi na usalama Mkoani Arusha vitaendelea kuhakikisha usalama na amani inakuwepo.

"Dunia imeona na watanzania wameithibitishia dunia ya kwamba wakiamua kulinda amani wanailinda, wasiotutakia mema jana wameaibika. Watanzania wanapenda amani na hawajazoea mambo ya maandamano na uvunjifu wa amani na wale wote waliokuwa wanataka vurugu leo wamejifungua- wana maumivu kwani hawakufanikiwa." Amesema Mhe. Makalla.

Mhe. Makalla kadhalika kando ya kuwahakikishia wananchi ulinzi na usalama muda wote, amehimiza pia umuhimu wa wananchi kujikita katika shughuli zao za kiuchumi na kijamii, akionya na kutangaza utimamu wa Vyombo vya ulinzi na usalama katika kukabiliana na wote wanaopanga kufanya vitendo vya uhalifu na uvunjifu wa amani katika Mkoa wa Arusha.

POLISI YAONYA WANAOENDELEA KUHAMASISHA MAANDAMANO

12/10/2025 09:22:00 am
POLISI YAONYA WANAOENDELEA KUHAMASISHA MAANDAMANO

Jeshi la Polisi nchini Tanzania kwa kushirikiana na Vyombo vingine vya ulinzi na usalama nchini wamewahakikishia wananchi kuwa wataendelea kulinda usalama wa Tanzania sambamba na maisha na mali za wananchi ili waweze kuendelea na shughuli zao kwa amani, utulivu na usalama.

Taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi Makao Makuu, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) David Misime leo Disemba 10, 2025, limeonya pia kuhusu wanaopanga kujitokeza leo kwenye Mitaa mbalimbali ili kufanya kile kinachoitwa maandamano ya amani kutokana na kushindwa kuyafanya jana Oktoba 29, 2025.

"Jeshi la Polisi linaendelea kuwakumbusha, kuwasisitiza na kuwaonya wasifanye hivyo kwani wanachokiita maandamano ya amani yasiyo na kikomo yalipigwa marufuku kutokana na kukosa sifa kulingana na matakwa ya Katiba na sheria ya Polisi na Polisi wasaidizi sura 322." Amesema Misime.

Polisi pia imeeleza kuwa kwa ambaye atakaidi kutii sheria za nchi kwa lengo la kuhatarisha usalama wa nchi ili kusimamisha shughuli za kiuchumi na kijamii zisiendelee,  watadhibitiwa ili nchi ibaki salama na watanzania wema na wapenda amani wabaki salama.

Aidha Taarifa ya Polisi imetoa wito pia kwa wananchi kuendelea kufanya shughuli zao na kufuata maelekezo watakayokuwa wanapewa na Vyombo vya ulinzi na usalama katika maeneo yote nchini sambamba na kutii sheria za nchi ili taifa liendelee kuwa salama na kila mmoja kuweza kuendelea na shughuli zake.

Tuesday, 9 December 2025

TUNAIMARISHA ZAIDI ULINZI NA USALAMA USIKU HUU- POLISI

12/09/2025 10:42:00 pm
TUNAIMARISHA ZAIDI ULINZI NA USALAMA USIKU HUU- POLISI

Jeshi la Polisi nchini Tanzania limetoa taarifa yake kwa Vyombo vya habari kuhusu hali ya usalama nchini kwa kipindi cha saa sita tangu ilipotoka taarifa ya awali majira ya saa 6 mchana leo Jumanne Disemba 09, 2025.

Kulingana na Msemaji wa Polisi, Makao Makuu Dodoma, David Misime amesema hali ya usalama nchini imeendelea kuwa shwari na Vyombo vya Ulinzi na Usalama vimeendelea kuimarisha usalama nchini, pamoja na kulinda raia na mali zao hadi muda huu wa jioni.

"Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Vyombo vingine vya ulinzi na usalama vingependa kuwahakikishia kuwa kuanzia majira haya vitaimarisha zaidi ulinzi na usalama tunapoelekea usiku ili kuzuia na kudhibiti vitendo vyovyote vinavyoweza kuwa ni tishio la kiusalama." Amesema Kamanda Misime.

Katika hatua nyingine, Jeshi la Polisi limetoa wito kwa kila mwananchi kuendelea kuzingatia kanuni za kiusalama na kuendelea kutii sheria za nchi kwani kila mmoja anahitaji kuwa salama wakati wote.

JESHI LA POLISI LAKANUSHA TAARIFA ZA UPOTOSHAJI MTANDAONI, LATHIBITISHA USALAMA NCHINI KUWA SHWARI

12/09/2025 02:29:00 pm


Na Mwandishi wetu, Dodoma

Jeshi la Polisi nchini limekanusha taarifa zinazoenezwa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu kuwepo kwa maandamano leo Desemba 9, 2025, na kusisitiza kuwa hadi majira ya mchana hali ya usalama nchini kote ni shwari.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi, Makao Makuu ya Polisi Dodoma,David Misime vyombo vya ulinzi na usalama vinaendelea kuimarisha ulinzi na kulinda maisha ya wananchi pamoja na mali zao kama ilivyo jukumu lao la msingi.

Polisi imeeleza kuwa picha na video zinazosambazwa mitandaoni zikidaiwa kuonyesha maandamano yanayoendelea leo si sahihi, bali ni matukio ya zamani na kwamba baadhi ya picha hizo zinatoka katika matukio ya Oktoba 29, 30 na 31 mwaka 2025, huku zingine zikitoka miaka ya nyuma ikiwemo tukio la Juni mwaka huu ambalo lilihusisha sherehe za jando za jamii ya Wamaasai zilizofanyika katika msitu wa TANAPA jijini Arusha.

Jeshi hilo limekumbusha kuwa maandamano yaliyokuwa yanatajwa kama “maandamano ya amani” yalipigwa marufuku tangu Desemba 5, 2025, baada ya kubainika hayakukidhi matakwa ya kisheria ikiwemo Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Sheria ya Polisi na Polisi Wasaidizi, Sura ya 322.

Aidha, Polisi imetoa wito kwa wananchi kuendelea kufuata sheria za nchi na kupuuza taarifa za upotoshaji, kwa manufaa ya amani na usalama wa Taifa.

WAFUNGWA 1,036 WAPATA MSAMAHA WA RAIS SAMIA

12/09/2025 11:44:00 am

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan leo Disemba 09, 2025, Tanzania ikiadhimisha miaka 64 ya uhuru wa Tanzania bara, ametangaza kuwasamehe wafungwa 1,036, wafungwa 22 kati yao wakiachiliwa huru na wengine 1,014 wakipunguziwa adhabu zao.

Kulingana na taarifa iliyosainiwa na Waziri wa mambo ya ndani ya nchi Mhe. George Simbachawene, Ikulu imeeleza kuwa ni matarajio ya serikali kuwa wafungwa walioachiwa huru watarejea tena katika jamii kushirikiana na wananchi katika ujenzi wa Taifa na kujiepusha kutenda makosa ili wasirejee tena gerezani.

Miongoni mwa waliosamehewa  ni wafungwa wagonjwa wenye magonjwa ya kudumu au sugu ambao wapo katika hatua za mwisho pamoja na wafungwa wazee wenye umri wa miaka 70 au zaidi- Vyote vikitakiwa kuthibitishwa na jopo la waganga wa Wilaya na Mikoa.

Aidha wengine walionufaika na msamaha huo ni wafungwa wa kike walioingia na ujauzito gerezani au wenye watoto wanaonyonya au wasionyonya waliohukumiwa kifungo cha mwaka mmoja na kuendelea pamoja na wafungwa wenye ulemavu wa mwili na akili wasio na uwezo wa kufanya kazi.

Aidha wamesamehewa pia wafungwa waliohukumiwa adhabu ya kuwekwa kizuizini (under president's pleasure) ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka kumi au zaidi

Prf. Kitila :Serikali imepanga kufanya mageuzi makubwa katika uongozi wa mashirika ya umma

12/09/2025 11:43:00 am

Serikali imepanga kufanya mageuzi makubwa katika uongozi wa mashirika ya umma, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa watendaji wakuu na wajumbe wa bodi za wakurugenzi wanapatikana kwa njia ya ushindani ili kuongeza uwazi, uadilifu na ushiriki mpana wa Watanzania wenye sifa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, amesema mfumo huo mpya utaanza kutumika kuanzia Julai 1, 2026 mara baada ya kupitishwa kwa sheria mpya inayoandaliwa na serikali.

Amesema uamuzi huo ni sehemu ya mpango mpana wa kuboresha utendaji wa mashirika ya umma, kuweka uwazi katika uteuzi wa viongozi, na kuondoa utaratibu wa uteuzi wa moja kwa moja uliokuwa ukilalamikiwa na wadau kwa kukosa ushindani wa wazi. 

“Kama ni Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO utaomba, uta-apply, na utashindanishwa. Kama unataka kuwa mjumbe wa bodi ya TPA au TISEZA utapitia mchakato wa ushindani. Watanzania wote wenye sifa wataomba, na uchaguzi utafanywa kwa ‘competitive recruitment,” amesema.
Katika maelezo yake kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Prof. Mkumbo amesema mageuzi hayo yanakwenda sambamba na hatua kadhaa zinazolenga kuongeza tija ya mashirika ya umma na kuimarisha mchango wake katika uchumi wa taifa na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Prof. Mkumbo amesema serikali inaunda mfumo mpya na imara wa kupima maendeleo ya mashirika ya umma kwa kuzingatia tija ya kiuchumi na ubora wa huduma. Mashirika hayo yatapewa vigezo vipya vya kupimwa na kila moja litahesabiwa kwa kiwango kinachochangia kwenye uchumi na ustawi wa wananchi.

Amesema sheria mpya itayataka baadhi ya mashirika ya umma ya kibiashara kujisajili katika Soko la Hisa  ili Watanzania waweze kununua hisa na kumiliki mashirika yao, kupanua uwazi katika uendeshaji, na kuongeza uwajibikaji kwa menejimenti na bodi.
Adbox