Adbox

Tuesday, 24 February 2026

AMANI YATAJWA KAMA CHACHU YA MAENDELEO NA DEMOKRASIA NCHINI

2/24/2026 04:21:00 pm

Watanzania wamehimizwa na kukumbushwa  wajibu wao mkubwa katika kuhakikisha kuwa tunu adhimu  ya amani iliyopo nchini inaendelea kudumu kama nguzo kuu ya maendeleo yetu ya taifa na ustawi wa kila Mtanzania, ikielezwa kuwa bila ya amani na umoja hakuna maendeleo, demokrasia, wala ustawi wa kijamii unaoweza kupatikana.

Akizungumza kuhusu umuhimu amani, baadhi ya wananchi akiwemo Bw. Manase Zebedayo amesisitiza kuwa wazi kwamba amani ndio chachu ya uwekezaji, elimu bora, huduma bora za afya na ustawi wa wananchi wote, akibainisha kuwa mitandao ya kijamii na siasa za ushindani, tuziepuke na kuziogopa  kauli za uchochezi, misimamo mikali ya kisiasa na mgawanyiko wa kijamii kwani ni miongoni mwa mambo yanayoweza kuharibu misingi ya amani na utulivu nchini.

"Amani ni hali ya mtu kuwa na uhuru wa kufanya jambo lolote lile halali kisheria, amani tafsiri yake pia ni upendo pia, tunapopendana ndio amani yenyewe na kubwa zaidi tuendelee kushikamana, tudumishe hiki tulichonacho kwani sisi nchi yetu ni kisiwa cha amani." Amesema Bw. Zebedayo.

Mwananchi huyu anaungana na kauli ya Rais Samia Suluhu Hassan wakati wa salamu zake za mwaka mpya ambapo pamoja na mambo mengine, Rais Samia aliwasihi Watanzania kutokubali tofauti za kiitikadi au kimtazamo kutokuwagawa na kuwapotezea malengo yao ya maendeleo na ustawi wa Taifa kwanj tofauti imekuwa ni sehemu ya demokrasia lakini tofauti hizo hazipaswi kuwagawa kwa namna yoyote ile.

Aidha katika salamu zake hizo, Rais Dkt. Samia alieleza kuwa Tanzania ni moja na wananchi wake wamejengwa na itikadi ya kuamini kuwa amani, umoja na mshikamano hujenga uzalendo na ndio virutubisho vinavyoiletea maendeleo endelevu na ustawi wa Watanzania.

Monday, 23 February 2026

POLISI YAONYA WANAOSAMBAZA VIDEO ZA KUZUA TAHARUKI KWA JAMII

2/23/2026 01:02:00 pm
POLISI YAONYA WANAOSAMBAZA VIDEO ZA KUZUA TAHARUKI KWA JAMII

Jeshi la Polisi nchini Tanzania limesema picha Mjongeo inayosambazwa kwenye Mitandao mbalimbali ya Kijamii si za matukio ya hivi karibuni bali ni tukio lililotokea Mkoani Dodoma mwaka 2023.

Taarifa kwa Vyombo vya habari iliyotolewa leo Jumapili Februari 22, 2026 na Msemaji wa Jeshi la Polisi Tanzania Naibu Kamishna wa Polisi DCP David Misime imesema tayari Polisi kwa kushirikiana na mamlaka nyingine imechukua hatua stahiki kwa kila mmoja kwenye video hiyo kwa alivyokiuka sheria, kanuni na taratibu za nchi.

Polisi pia imetoa wito kwa wananchi kuacha kutumia au kusambaza picha za matukio yaliyopita na kuwaaminisha wananchi kuwa ni tukio la hivi karibuni, likisisitiza kuwachukulia hatua kali za kisheria wale wote watakaobainika kufanya hivyo vyenye kuleta taharuki kwa jamii.

Sunday, 22 February 2026

POLISI YAANZA MSAKO KWA ANAYEJIITA 'TFF', YAWATOA HOFU WANANCHI

2/22/2026 06:24:00 pm

Jeshi la Polisi nchini Tanzania limesema linawafuatilia kwa karibu baadhi ya watu wanaohamasisha kujiingiza kwenye vitendo vya kihalifu pamoja na matamshi na jumbe zinazotengenezwa na baadhi yao na kuzisambaza mtandaoni kwa lengo la kuleta taharuki kwa jamii.

Msemaji wa Jeshi la Polisi Tanzania Naibu Kamishna wa Polisi DCP David Misime ameviambia vyombo vya habari leo Jumapili Februari 22, 2026 kuwa ufuatiliaji huo unafanyika usiku na mchana, akiwataka wananchi kutokuwa na hofu na kuendelea na shughuli zao za kiuchumi na kijamii kama kawaida.

Polisi pia imetoa wito kwa wananchi kuendelea kuwapuuza watu hao na wengineo pamoja na taarifa na jumbe zao kwani watu hao hawapo ndani ya mipaka ya nchi na hata wanachokihamasisha hawatashiriki na hawatokuwa na uwezo wala mwanya wa kushiriki.

"Wananchi watambue lengo la watu hao ni kutaka kutuchonganisha, kutujengea chuki ili tuhamasike kujiingiza kwenye uhalifu na vitendo vya vurugu. Jeshi la polisi halitasita kumchukulia hatua yeyote yule atakayeendelea kujihusisha na vitendo kama hivyo au kujiingiza katika uhalifu wa aina yoyote ile kwani ni kinyume cha sheria." Amesema Kamanda Misime.

Polisi imewataja baadhi ya watu wanaoshawishi uhalifu kuwa ni pamoja na anayejitambulisha kwa jina la TFF ambaye amekuwa akitoa taarifa mbalimbali ikiwemo kufanya mazoezi porini na kwamba wameshafanya matukio kadhaa ya kijinai ambapo Polisi imekanusha taarifa hizo zote zinazotolewa na mtu huyo kwenye mitandao.

Dean Rev. Stanley Tabulu akikagua jengo la utawala Shule ya Sekondari Embeko atoa pongezi

2/22/2026 06:23:00 pm
Kondoa

Matukio mbalimbali yakimuonesha Msaidizi wa Askofu wa Kanisa la KKKT Dayosisi ya Dodoma Mchungaji Stanley Tabulu  akikagua jengo la utawala Shule ya Sekondari   Embeko iliyopo Jimbo la Kondoa Dayosisi ya Dodoma. 

Akizungumza mara baada ya ukaguzi wa Jesho hilo Mchungaji Tabulu ameupongeza  uongozi wa Shule chini ya Mkuu wa shule hiyo ,l Christian Siara kwa usimamizi mzuri wa mradi huo kwa weledi Mkubwa. 

Aidha amesema kuwa Uongozi wa Dayosisi upo nao bega kwa bega katika kulijenga Taifa ambapo ameahidi kupitia Ofsi ya Dayosisi watahakikisha wanaunga mkono jitihada zao za ujenzi wa jengo hilo.

 Nae Mkuu wa shule ya Sekondari Embeko Mwalimu Christian Siara amesema ujenzi huo ambao umefikia hatua ya lenta  ni nguvu ya shule bila kutegemea michango kutoka nje ya nchi. 

amesema kumalizika kwa jengo hilo itakuwa faraja kwa walimu na wanafunzi kwani ni jengo la kisasa ambalo limekidhi vigezo vyote na litasaidia kufanya kazi katika mazingira rafiki. 


Saturday, 21 February 2026

(IAA) imeongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya Kimkakati

2/21/2026 11:10:00 am

Na Doreen Aloyce, Dodoma

TAASISI ya Uhasibu Arusha (IAA) imeongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati inayolenga kuimarisha ubora wa elimu, kukuza uchumi wa kidijitali na kuboresha kwa kiwango kikubwa mazingira ya kufundishia na kujifunzia, kwa kuwekeza zaidi ya shilingi bilioni 42 katika ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya chuo katika kampasi zake mbalimbali nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma Februari 20,2026, Prof. Eliamani Sedoyeka, Mkuu wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), amesema uwekezaji huo unahusisha utekelezaji wa Madarasa Janja Mahiri ya Akili Unde (AI Smart Classrooms), ujenzi wa Kituo cha Kisasa cha Data, utoaji wa Elimu Mseto, ongezeko la uwezo wa intaneti, muunganisho wa MPLS pamoja na ujenzi wa Kituo cha Umahiri cha TEHAMA.

Amesema hatua hiyo inalenga kuongeza ubunifu, ajira na ushindani wa taifa kimataifa. 

"Mbali na uwekezaji wa teknolojia, IAA inaendelea na ujenzi wa majengo ya taaluma, hosteli na utawala katika kampasi za Arusha, Babati, Dodoma na Songea," Amesema


Na kuongeza " Zaidi ya shilingi bilioni 18 zimetumika kujenga hosteli katika kampasi za Arusha na Babati ili kuwahakikishia wanafunzi, hususan wa kike, malazi salama na rafiki, " Amesema Prof. Sedoyeka

Aidha amesema Kupitia Mradi wa HEET, taasisi hiyo pia inanufaika na ujenzi wa majengo ya taaluma katika kampasi za Babati na Songea yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 32 kwa pamoja, hatua inayotarajiwa kuongeza ubora wa mazingira ya kufundishia na kujifunzia.

Friday, 20 February 2026

POLISI YAFANYA MSAKO, IKIOMBA WENYE TAARIFA ZA WALIOMUUA MFANYABIASHARA WA MADINI

2/20/2026 06:27:00 pm
Na Mwandishi Wetu. 


Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha kupitia kwa Kamanda wa Polisi Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, SACP Justine Masejo limetoa wito kwa yeyote mwenye taarifa ambazo zinaweza kusaidia kufanikisha kukamatwa kwa waliohusika na mauaji ya Mfanyabiashara wa madini Abdillah Musa Mollel 'Banjo', kuziwasilisha kwa Jeshi la Polisi ili zifanyiwe kazi.

Kamanda Masejo amebainisha hayo katika taarifa yake kwa Vyombo vya habari leo Ijumaa Februari 20, 2026 ikiwa ni siku moja mara baada ya Jeshi hilo kupata taarifa za Mwili wa mfanyabiashara huyo kuonekana katika Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma.

"Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha Februari 13, 2026 lilipokea taarifa kuhusu kupotea kwa mtu mmoja aitwaye Abdilah Musa Mollel maarufu kama Banjo na kuanzia hapo tulianza uchunguzi na wakati uchunguzi ukiendelea Tarehe 19, 02, 2026 taarifa zilipokelewa kuwa ameonekana huko Kondoa Mkoani Dodoma akiwa amefariki." Imesema taarifa ya Kamanda Masejo.

Mfanyabiashara huyo wa madini Mkoani Arusha aliyekuwa akiishi eneo la Sanawari Jijini Arusha inadaiwa kuwa mara ya mwisho kuonekana hadharani ni wakati akifanya mazoezi ya mwili kwenye jengo moja katikati ya Jiji la Arusha   na mwili wake umewasili leo Mkoani Arusha na taratibu za mazishi zinafanyika leo nyumbani kwake Sanawari.

Wednesday, 18 February 2026

AMANI NI MUHIMILI WA UHAI NA MAENDELEO YA BINADAMU- MWAIKASU

2/18/2026 05:56:00 pm

Wito umetolewa kwa Jamii kuafikiana na kupendelea njia ya mazungumzo katika utatuzi wa migogoro mbalimbali, Vijana wakitakiwa pia kujiepusha na vikundi visivyokuwa na tija kwa ustawi wao pamoja na kukataa kujihusisha na maneno na matendo yenye kuashiria uvunjifu wa amani kwani amani ndio muhimili wa uhai na maendeleo ya binadamu.

Aidha Watanzania pia kwa imani zao tofauti wamesisitizwa umuhimu wa kumshirikisha na kumuomba Mwenyenzi Mungu aendelee kuibariki na kuidumisha amani ya Tanzania, mifano ikitolewa kwa namna ambavyo baadhi ya Mataifa duniani yalivyopitia madhila makubwa ya kijamii na kiuchumi kutokana na kutoweka kwa amani katika mataifa hayo licha ya jitihada nyingi zilizoshindwa za kuirejesha amani katika mataifa hayo.

Akizungumza na Waandishi wa habari leo Jumanne Februari 17, 2026 Bi. Aneth Dickson Mwaikasu, Mkazi wa Kigogo Fresh, Jijini Dar Es Salaam amekumbusha pia umuhimu wa amani katika maendeleo na ustawi wa Jamii, akisema amani ni tunu muhimu na ya mfano ambayo Tanzania imebarikiwa kuwa nayo na hivyo ni muhimu kuilinda na kuiendeleza.

"Sisi kama binadamu tunamuhitaji Mungu sana ili amani yetu aliyoitunuku Tanzania yetu iendelee kuwepo na cha pili lazima tuafikiane kama binadamu kwamba tufanye nini ili amani iendelee kuwepo kwasababu amani hainunuliwi na ikipotea kuirudisha haijawahi kuwa rahisi ama kuwezekana hata kidogo." Amesema Bi. Mwaikasu.

Serikali ya Tanzania inaichukulia amani si dhana pekee bali kama hitaji la msingi ambalo bila hilo hakuna anayeweza kupata maendeleo ambapo msingi huo pia unaungwa mkono na Umoja wa Mataifa ambapo kulingana na malengo ya maendeleo endelevu, amani ni kigezo cha kwanza cha kufikia malengo mengine yote duniani, ikisema jamii zenye amani ndizo zinazoweza kupunguza rushwa, kutoa haki sawa kwa wote na kukuza uwajibikaji kwa jamii.

TUJIIMARISHE KIUCHUMI KAMA NGUZO YA AMANI NA UTULIVU- MAZENGO

2/18/2026 05:47:00 pm

Watanzania wametakiwa kushiriki kikamilifu katika kulinda na kudumisha amani ya Tanzania kwa ustawi na maendeleo binafsi na ya Taifa, Wito ukitolewa kwa jamii hususani Vijana kuwekeza katika ujuzi ili kuwawezesha kujikita katika shughuli za kiuchumi na uzalishaji mali ili kujiingizia kipato na kujiletea maendeleo yao binafsi na ya Taifa kwa ujumla.

Wito huo umetolewa wakati huu ambapo Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imetangaza na kuanza uwekezaji mkubwa wa kuwezesha wananchi kiuchumi hususan Vijana, kwa kutoa mabilioni ya fedha kupitia wizara mbalimbali ikiwemo ahadi ya utoaji wa Shilingi Bilioni 200 za Mikopo kwa makundi ya wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo, Bilioni 2 za watengeneza maudhui mtandaoni, mikopo ya Halmashauri pamoja na kuundwa kwa Wizara maalumu ya maendeleo ya Vijana iliyojikita katika kusimamia fursa za Vijana na kutatua changamoto zilizopo.

"Amani ni muhimu kwasababu bila amani huwezi kufanya chochote na amani huvunjika pale ambapo tunakuwa na Vijana wasiokuwa na ajira ama ujuzi wowote ule ni lazima ataenda ndivyo sivyo na kuvunja amani aidha kwa kuiba ama kushiriki katika matukio mengine ya uvunjifu wa amani." Amesema Bw. Dickson Mazengo, Mkazi wa Ubungo, Dar Es Salaam.

Akieleza zaidi kuhusu umuhimu wa kulinda amani, Bw. Mazengo amesisitiza umuhimu pia wa kushirikisha ujuzi mbalimbali kwa watu wengine kwenye jamii, akisema kupitia hilo anaamini kuwa kila mmoja atapata shughuli ya kufanya na hivyo kunufaisha mnyororo mzima unaomtegemea na kutengeneza utulivu wa jamii unaozalisha amani kwenye Taifa.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa amani inatajwa kama zaidi ya kutokuwepo fujo, ikielezwa kuwa ni utaratibu wa kihamii unaojengwa juu ya msamaha na ushirikiano na kusisitiza jukumu la kila mwananchi kuwa balozi wa amani kuanzia ngazi ya familia, jamii na Taifa ili kuunda ulimwengu bora kwa kila mmoja kwani amani husaidia katika maboresho ya huduma na ujenzi wa miundombinu msingi ya kijamii na kiuchumi kwa kila mmoja.

Tuesday, 17 February 2026

WATANZANIA TUNA WAJIBU WA KULINDA NCHI NA RASILIMALI ZAKE-WAZIRI KATAMBI

2/17/2026 11:07:00 am

Waziri wa Mambo ya Ndani Nchi, Mhe. Patrobas Katambi amesisitiza na kuwakumbusha Watanzania kuwa wanawajibika katika kulinda nchi na rasilimali za Tanzania pamoja na kuhakikisha Tanzania inaendelea kubakia salama na yenye amani kwa mustakabali wa maendeleo ya Taifa na ustawi wa jamii na kila Mtanzania.

Waziri Katambi amebainisha hayo Mkoani Tanga wakati wa muendelezo wa ziara ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, akisisitiza kuwa bila amani na usalama hakuna shughuli yoyote ya kijamii ama kiuchumi inayoweza kuendelea.

"Niwakumbushe Watanzania wenzangu kwamba sisi wote Watanzania tunao wajibu wa kuilinda nchi yetu. Jukumu la ulinzi na usalama wa rasilimali, raia wote ni wajibu wetu sote. Haya yote hayawezekani pia kama hakuna usalama kwani kupoteza usalama maana yake hakuna ulinzi, hakuna amani na kama hakuna amani hakuna shughuli  yoyote inayoweza kuendelea."

"Leo tupo hapa tuna amani kwasababu hakuna hata mmoja aliyepigiwa simu na kuambiwa nyumbani kwake wamevamia majambazi, hakuna aliyepigiwa simu na kuambiwa kuwa kuna vurugu mahali na hii ni kwasababu vyombo vyetu vimejidhatiti kiutaalamu na kiteknolojia kuhakikisha nchi yetu inakuwa salama." Ameongeza kusema Waziri Katambi

POLISI YAWASAKA "WALIOMVUTISHA" SIGARA MTOTO, KUMREKODI NA KUSAMBAZA MTANDAONI

2/17/2026 11:04:00 am

Msemaji wa Jeshi la Polisi Tanzania Naibu Kamishna wa Polisi DCP David Misime leo Jumapili Februari 15, 2026  amesema Jeshi la Polisi limeanza uchunguzi na kuwafuatilia watu ambao wamesikika kwenye Kipande cha Video kilichosambaa kwenye Mitandao ya Kijamii, wakimuhamasisha mtoto mdogo wa kiume kuvuta sigara kwani kitendo hicho ni kinyume na sheria, kanuni na taratibu za kijamii.

Taarifa iliyotolewa kwa Vyombo vya habari na Msemaji huyo wa Polisi imesema uchunguzi utakapokamilika hatua za kisheria zitachukuliwa, akitoa wito kwa yeyote anayewafahamu watu hao au mtoto huyo kulisaidia Jeshi la Polisi ili kuwafikia na kuokoa afya ya mtoto huyo aliyehamasishwa kuvuta sigara.

"Tunatoa onyo pia kwa watu wenye tabia za kufanya vitendo vya kikatili na vya unyanyasaji kama hivyo na vinavyofanana na hivyo kwa watoto kwa lengo lolote lile." Imesema taarifa ya Polisi.

Kulingana na Polisi Makao Makuu, Dodoma, wapo wanaofanya hivyo kwa watoto wadogo kwa msukumo wa kupata wafuasi kwenye mitandao ya kijamii (followers) kwaajili ya mitandao yao, likiwataka wanaofanya hivyo kuacha mara moja kwani hatua zitakazofuata ni kukamatwa na kuchukuliwa hatua kwani matendo hayo ni uvunjifu wa sheria, kanuni na taratibu za nchi.

Thursday, 12 February 2026

UMIKIDO WASHIRIKI MKUTANO MKUU WA MWAKA WA VYOMBO VYA UTANGAZAJI

2/12/2026 08:01:00 pm
UMIKIDO WASHIRIKI MKUTANO MKUU WA MWAKA WA VYOMBO VYA UTANGAZAJI

Umoja wa Vyombo vya Habari vya Mitandao ya Kijamii Mkoa wa Dodoma (UMIKIDO) umeshiriki Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji nchini.

Mkutano huo wa siku mbili unafanyika katika Ukumbi wa New Generation jijini Dodoma, ukianza leo Februari 12, 2026. Mkutano huo umeandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).

Katika mkutano huo, mada na mafunzo mbalimbali yanawasilishwa kwa waandishi wa habari pamoja na wadau wa sekta ya utangazaji. 

Aidha, kunafanyika mijadala mbalimbali inayolenga kujadili masuala muhimu yanayohusu maendeleo na uboreshaji wa vyombo vya utangazaji nchini.

Mkutano huo umefunguliwa rasmi na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma.

TAZAMA MATUKIO, UMIKIDO WASHIRIKI MKUTANO MKUU WA MWAKA WA VYOMBO VYA UTANGAZAJI

2/12/2026 05:23:00 pm
Matukio mbalimbali katika picha ikiwaonesha wanachama waliohudhuria Mkutano Mkuu wa Mwaka wa vyombo vya utangazaji jijini Dodoma

katika Mkutano huo ulioenda sambamba na kauli mbiu ya Matumizi ya Teknolojia katika kupanua na kuboresha Huduma za Utangazaji Vijijini,  Mgeni Rasmi ni Naibu waziri wa Habari ,sanaa,utamaduni na Michezo Hamis Mwijuma.

Mwenyekiti wa Umikido Benny Majata akiteta jambo na Katibu wa Umikido Emmanuel Charles katika mkutano huo.


DKT. MWIGULU AMWAKILISHA RAIS DKT. SAMIA MAADHIMISHO YA MIAKA 30 YA OCEAN ROAD

2/12/2026 11:04:00 am
*DKT. MWIGULU AMWAKILISHA RAIS DKT. SAMIA MAADHIMISHO YA MIAKA 30 YA OCEAN ROAD*

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba leo Februari 12, 2026 amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika maadhimisho ya miaka 30 ya  Taasisi ya Saratani Ocean Road.

Maadhimisho yanayofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar es Salaam yanatoa fursa kwa Taasisi hiyo pamoja na wadau wengine kutafakari kwa pamoja safari ya mapambano dhidi ya saratani kwa kuangalia walipotoka, walipo na wapi  wanaelekea.


IGP WAMBURA AKAGUA UJENZI WA NYUMBA NA MABWENI SHULE YA POLISI MOSHI

2/12/2026 10:43:00 am

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Tanzania IGP Camillus wambura akiambatana na maafisa wengine wa Polisi Makao Makuu Dodoma, wamefanya ukaguzi wa maendeleo ya mradi wa ujenzi wa nyumba za wakufunzi na familia zao pamoja na ujenzi wa mabweni ya wanafunzi kwenye shule ya Polisi Moshi, Mkoani Kilimanjaro.

Ujenzi huo unatekelezwa na serikali ya awamu ya sita chini ya Amiri Jeshi Mkuu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha na kuboresha upatikanaji wa miundombinu ya ujenzi wa miradi mbalimbali inayoendelea kutekelezwa ndani ya Chombo hicho cha ulinzi na usalama.

Kukamilika kwa miradi hiyo katika shule hiyo ya Polisi Moshi kunatarajiwa kuongeza morali katika utendaji kazi kwa Maafisa wa Polisi sambamba na kukuza ustawi wa askari kwa kukaa na kuishi kwenye mazingira bora na ya kisasa jambo litakalowawezesha kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi katika kuwalinda wao na mali zao.

Kando ya maboresho na ujenzi wa miundombinu, Kumefanyika pia maboresho katika mitaala ya mafunzo kwa Askari Polisi sambamba na Shule hiyo kuingia kwenye mikataba na vyuo vya ndani na nje ya nchi ili kuendana na utekelezaji wa mapendekezo ya Tume ya Haki jinai iliyopendekeza askari Polisi kujengewa uwezo wa kitaaluma na utendaji kazi.

Kulingana na taarifa ya Polisi kwa Vyombo vya habari jana Februari 11, 2026, katika utekelezaji wa pendekezo hilo jumla ya askari 111 wamefanikiwa kuhitimu masomo katika ngazi ya uzamili (Masters) kwa mwaka 2025 kutokana na uwepo wa Tawi la Chuo cha uhasibu Arusha (IAA) katika shule hiyo ya Polisi Moshi, ambao wanaendesha kozi mbalimbali za kuwajengea uwezo na ujuzi Askari kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi nchini.

Wednesday, 11 February 2026

AMANI NDIO MSINGI WA BIASHARA ZETU- MWINYIMVUA

2/11/2026 01:52:00 pm

Utulivu na amani vimetajwa kama misingi muhimu katika kuwezesha maendeleo na ustawi wa jamii kiuchumi, msisitizo na tahadhari ikitolewa kwa Watanzania kuhakikisha amani hiyo inasalia nchini, amesema Bi. Mosi Mwinyimvua, Mkazi wa Mvuti Mkoani Dar Es Salaam.

"Amani ni kila kitu kwetu na kama unavyojua sisi akinamama wajasiriamali lazima tutoke tukapate riziki, tunasomesha, tunalea watoto na wengine tumeachiwa watoto bila baba zao sasa bila kutoka kujishughulisha watoto wetu wataishi vipi? Amani ni muhimu."amekaririwa Bi Mwinyimvua.

Mwananchi huyo mjasiriamali akizungumza nasi mapema leo Jumatano Februari 11, 2026, amesisitiza kwamba shughuli za kiuchumi na kijamii bila ya amani huathirika na kuleta hofu kwa jamii, akisisitiza umuhimu wa kila Mtanzania kushiriki katika kulinda na kudumisha amani.

Hali ya amani kulingana na maandiko mbalimbali inatajwa kuwezesha maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kiutamaduni kwa kuwa inawapa watu uhuru wa kufanya shughuli zao za kila siku bila wasiwasi na hivyo kutajwa kama msingi wa mafanikio ya jamii yoyote, faida zake zikidhihirika katika kila nyanja ya maisha ya binadamu.

Tuesday, 10 February 2026

NDUGU WASHIKILIWA KWA KUMUUA SHEMEJI YAO 'KISA MGOGORO WA MASHAMBA'

2/10/2026 11:34:00 pm
WASHIKILIWA NA POLISI MBEYA KWA KUINGILIA MFUMO WA UKOPESHAJI SIMU

NDUGU WASHIKILIWA KWA KUMUUA SHEMEJI YAO 'KISA MGOGORO WA MASHAMBA'

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Benjamin Kuzaga amesema wanamshikilia Bw. Charles Oden Mwakasege (32) fundi simu Mkazi wa Meta Jijini Mbeya na Bw. Isack Charles 'Bebwa' mkazi wa Shewa, kwa tuhuma za kuingilia mdumo wa kibiashara wa makampuni ya ukopeshaji wa simu.

Kulingana na Kamanda Kuzaga katika taarifa yake ya leo Jumanne Februari 10, 2026 kwa Vyombo vya habari, watuhumiwa hao walikamatwa katika msako uliofanyika kuanzia Januari 27, 2026 katika maeneo mbalimbali Mkoani humo ambapo watuhumiwa wanadaiwa kubadili simu zilizokopwa na watu mbalimbali kutoka katika makampuni ya ukopeshaji na kuondoa mfumo uliowekwa ili waliokopeshwa wasiweze kufuatiliwa katika kulipa fedha walizokubaliana na makampuni hayo.

"Baada ya watuhumiwa hao kufanyiwa upekuzi kwenye ofisi zao walipatikana wakiwa na simu aina ya Samsung 53, Infinix 21, Tecno 13, Itel 11, Yas 1. Pia walikutwa na vifaa vya kuflash simu ambavyo ni Infinix Box Nongle Cm2 moja, Jtag Adapter Isp 4bit 02, F64 flash ultra box 02, Easy Jtag Plus box 02 Ufi box 01 na Laptop 03." Amesema Kamanda kuzaga.

Polisi ya Mbeya pia imetangaza kuwashikiliwa watuhumiwa wanne (Wilfred Komba (24), Mwanachuo wa mwaka wa kwanza Chuo Kikuu Iringa, Lenad Shamba (21) mkazi wa Tarime, James Mwakalebela (26) mkazi wa Kyela na Joseph Mkwara (26) kwa tuhuma za kusafirisha dawa za kulevya aina ya Bhangi zikiwa na uzito wa Kilo 45 na gramu 785 katika nyakati tofauti kwenye mabegi, wakidaiwa kuingiza dawa hizo kutoka nchi jirani.

Aidha Kamanda Kuzaga amesema wanawashikilia ndugu wa familia moja ambao ni Solomon Mwambyale (68) na watoto wake wawili, Stephano Mwaisango (32) na Emmanuel Mwaisango (36), kwa tuhuma za mauaji ya Jenti Segelela (87) ambaye alikuwa shemeji yake na mtuhumiwa Solomon, wakidaiwa kumkata na kitu chenye ncha kali kisogoni na kisha kukimbia, chanzo kikiwa ni mgogoro wa mashamba ya ukoo na tamaa ya kujipatia mali kwa njia isiyo halali.

RC SENYAMULE AUKARIBISHA UMIKIDO, AITAKA KUWA CHACHU YA MAWASILIANO KATI YA SERIKALI NA WANANCHI

2/10/2026 03:09:00 pm

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ameukaribisha Umoja wa Vyombo vya Habari vya Mitandao ya Kijamii Mkoa wa Dodoma (UMIKIDO) na kuutaka kuwa chachu ya kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na wananchi kupitia utoaji sahihi wa taarifa pamoja na ubunifu wa maudhui.

RC Senyamule ametoa kauli hiyo leo Februari 9, 2026, mara baada ya viongozi wa UMIKIDO kufika ofisini kwake kwa lengo la kujitambulisha na kuomba ushirikiano na Serikali ya Mkoa wa Dodoma.

“Hongereni kwa kuanzisha umoja huu. Nimefurahishwa sana kwani utarahisisha kazi na kuwa kiunganishi muhimu kati ya Serikali ya Mkoa na vyombo vya habari vya mitandaoni. Tulitamani kupata watu wanaozungumza lugha moja na Serikali, na tunaamini ninyi ni wazalendo,” amesema Mhe. Senyamule.

Ameeleza kuwa uwepo wa umoja huo utaisaidia Serikali kufikisha taarifa kwa wananchi kwa ufanisi zaidi, sambamba na kuongeza uelewa wa umma kuhusu shughuli na miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

“Ni muhimu Watanzania wakaendelea kufahamu kazi zinazofanywa na Serikali. Nina imani mtakuwa wabunifu katika kuandaa na kusambaza taarifa kwa njia zitakazowafikia wananchi kwa urahisi,” ameongeza.

Aidha, RC Senyamule amewataka wanachama wa UMIKIDO kuzingatia kutangaza miradi ya kimkakati na mipango ya maendeleo, ikiwemo uhifadhi wa mazingira, matumizi ya nishati safi ya kupikia, sekta ya utalii na michezo, pamoja na kuhamasisha matukio mbalimbali kuelekea mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027.

Awali, viongozi wa UMIKIDO walieleza dhamira na malengo ya kuanzishwa kwa umoja huo, ikiwa ni pamoja na kuimarisha maadili ya uandishi wa habari za mitandaoni na kushirikiana kwa karibu na Serikali katika utoaji wa taarifa sahihi kwa umma. Pia waliomba ushirikiano kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ili kutimiza malengo hayo.

Viongozi walioshiriki ziara hiyo ni (Mwenyekiti wa UMIKIDO Bw.Benny Majata,Katibu  Emmanuel Charles, Zena Chitwanga (Mhasibu), Daniel Mkate (Afisa Mahusiano), Alex Sonna (Kamati ya Ufuatiliaji), Henry Masanja (Kamati ya Nidhamu) na Ronald Sonyo (Kamati ya Fedha na Mipango).

JESHI LA POLISI KUENDELEA KUWEKA JITIHADA ZA KUNUNUA MBWA WAPYA WA KISASA.

2/10/2026 11:11:00 am

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura, amesema Jeshi la Polisi litaendelea kuweka jitihada mbalimbali za kununua mbwa wapya wa kisasa na wenye uwezo ili kuboresha muonekano wa mbwa wa Polisi mwenye umbo lenye kumdhoofisha mhalifu.

IGP Wambura, ameyasema hayo wakati wa Ufunguzi wa Kikao Kazi cha Wakuu wa Kikosi cha Mbwa na farasi wa Mikoa na Wataalam Waongoza Mbwa na Farasi kikao kilichofanyika jijini Dar es salaam Februari 9,2026 huku akiweka msisitizo kwenye eneo la utoaji wa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kuwatumia Wanyama kazi katika kudhibiti uhalifu kwenye maeneo yao.

Akizungumza na Watendaji hao IGP Wambura, amebainisha kuwa, Kikosi hicho kina umuhimu mkubwa kiusalama kwa kuwa Doria za mipakani na maeneo mengine muhimu hulazimika kutumia mbwa na farasi kwani ni rahisi kupenya kwenye maeneo ambayo gari haliwezi kupita kwa urahisi.

Amesema, Jeshi la Polisi lina Mbwa na Farasi wanaofanya kazi katika bandari, viwanja vya ndege na mipakani kwa lengo la kuzuia biashara za magendo na usafirishaji haramu wa silaha pamoja na dawa za kulevya, hivyo amewataka kuendelea  kuweka nguvu ya kutosha kuhakikisha kuwa, muda wote mipaka yetu inakuwa salama kwa kushirikiana na askari kutoka vikosi vingine ili kudhibiti uhalifu.

Aidha, IGP Wambura, ametoa wito kwa Watendaji wa Kikosi hicho hususani tunapojiandaa na mashindano ya AFCON 2027 ambapo Tanzania ni mojawapo ya nchi Mwenyeji wa Mashindano hayo, kuhakikisha wanakuwa na mbwa na farasi bora wenye mafunzo ya viwango vya kimataifa ili waweze kutoa huduma bora isiyokuwa na mashaka na ambayo itasaidia kuiletea sifa nchi yetu.

Nae Kamishna wa Operesheni na Mafunzo CP Awadhi Juma Haji, amempongeza Mkuu wa Jeshi la Polisi kwa kuendelea kuboresha kikosi cha Mbwa na Farasi na kuhakikisha kikosi kinatekeleza majukumu yake ipasavyo ya kukabiliana na matukio mbalimbali ya kihalifu ikiwemo udhibiti wa dawa za kulevya, silaha haramu pamoja na bidhaa nyingine za magendo.

Kamishna Awadhi amesema kikosi hicho kimeweza kushiriki kwenye operesheni za matukio mbalimbali ikiwemo mikutano ya kitaifa na kimataifa ili kuimarisha amani na utulivu wa kutosha na kudhibiti viashiria vyovyote vya kihalifu.

Kwa upande wake Mkuu wa Kikosi cha Mbwa na Farasi Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Namsemba Mwakatobe, amesema kikao kazi hiki kitawezesha kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo wa kiutendaji hivyo washiriki wa kikao kazi hicho wataenda kuleta mabadiliko ya kiutendaji kwenye maeneo yao kwa kuhakikisha wanadhibiti uhalifu.

Monday, 9 February 2026

UMIKIDO WATINGA OFSI YA TCRA KUJITAMBULISHA

2/09/2026 12:55:00 pm
Na Mwandishi wetu,Dodoma

Viongozi wa Umoja wa Vyombo vya Habari vya Mitandao ya Kijamii Mkoa wa Dodoma (UMIKIDO) wakiongozwa na Mwenyekiti Ben Majata, wamefanya ziara ya kujitambulisha katika Ofisi za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) – Kanda ya Kati zilizopo jijini Dodoma.

Katika ziara hiyo, iliyofanyika leo Februari 9, 2026 viongozi wa UMIKIDO walifanya mazungumzo na Meneja wa TCRA Kanda ya Kati  Mhandisi Asajile John na kueleza malengo ya kuanzishwa kwa umoja huo pamoja na dira ya kukuza taaluma na uendeshaji wa vyombo vya habari vya mitandao ya kijamii kwa kuzingatia sheria na maadili ya uandishi.

Kwa upande wake, Meneja wa TCRA Kanda ya Kati, Mhandisi John, ameukaribisha UMIKIDO kwa ushirikiano wa karibu, ikiwemo kuandaa mafunzo kwa wanachama na kuwahimiza kufanya kazi kwa kuzingatia sheria, sambamba na kusajili vyombo vyao na kupata leseni rasmi kutoka mamlakani.

Aidha, ameeleza kuwa maboresho mbalimbali yanayoendelea kufanywa na TCRA yanalenga kupunguza malalamiko ya waendeshaji wa vyombo vya habari mitandaoni na kuboresha mazingira ya kazi katika sekta hiyo.

Pia amewahimiza kuchangamkia fursa zinazotolewa na Serikali ili kujiimarisha kitaaluma na kiuchumi.

Viongozi wengine walioshiriki ziara hiyo ni Emmanuel Charles (Katibu wa UMIKIDO), Zena Chitwanga (Mhasibu), Daniel Mkate (Afisa Mahusiano), Alex Sonna (Kiongozi wa Kamati ya Ufuatiliaji), Henry Masanja (Kiongozi wa Kamati ya Nidhamu) na Ronald Sonyo (Kiongozi wa Kamati ya Fedha na Mipango).

Saturday, 7 February 2026

UPENDO NA MAELEWANO VYATAJWA KUWA MSINGI WA AMANI NCHINI

2/07/2026 05:38:00 pm

Adam Seleman, Mkazi wa Msongora Jijini Dar Es Salaam amesema tafsiri halisi ya amani ni pamoja na kuelewana na kupendana miongoni mwa Watanzania, akihimiza upendo na maelewano kama msingi wa kudumisha amani na utulivu nchini.

Bw. Selemani amebainisha hayo leo Jumamosi Februari 07, 2026 wakati akizungumza na mwandishi wetu wa habari kuhusu umuhimu wa amani kwa ustawi na maendeleo, akisema familia, Jamii na Nchi yoyote inahitaji amani na utulivu ili kuweza kutimiza majukumu na wajibu walionao.

"Maana halisi ya amani ni ile hali ya mtu kuwa na uhuru wa kufanya jambo ambalo linaruhusiwa Kikatiba na pia amani tafsiri yake ni upendo, tukipendana ndio amani yenyewe kuanzia ndani ya nyumba. Nawaomba sana tuendelee kushikamana na kudumisha hiki tulichonacho kwani sisi nchi yetu ni kisiwa cha amani." Amesema Bw. Selemani.
Adbox